.

.

.

.

.

.

.

.
KARIBUNI TUHABARIKE, TUELIMISHANE, TUPEANE HABARI ZA KUKUFANYA UTABASAMU KIDOGO NA MATUKIO YALIYOFANYIWA UCHUNGUZI WA KINA TOKA KILA PEMBE CONTACTS: +255 787 377 722 Email: drweyunga@gmail.com PIA UNAWEZA KUNI FOLLOW KUPITIA INSTAGRAM YANGU @drweyunga | TANGAZA NASI ILI UWAFIKIE WATU WENGI ZAIDI.

Jumamosi, 23 Agosti 2014

VIFAA VYA KUBAINI DALILI ZA AWALI ZA UGONJWA WA EBOLA KUPITIA JOTO LA MWILI VYAWASILI NCHINI, KUANZA KUTUMIKA VIWANJA VYA NDEGE.

Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dkt. Kebwe Steven Kebwe (kulia) akimkabidhi Mkurugenzi wa Afya na Usafi wa Mazingira wa Wizara ya Afya na Ustawi Dkt. Elias Chinamo moja ya kifaa (kamera) itakayotumika kupima dalili za ugonjwa wa Ebola kwa wasafiri wanaoingia nchini kupitia viwanja vya ndege ili kuhakikisha kuwa wananchi wanakuwa salama kwa kuuzuia ugonjwa huo kuingia nchini.
Mkurugenzi wa Ugavi wa Bohari ya Dawa Tanzania (MSD),Heri Mchunga (kushoto) akimpima Mkurugenzi wa Afya na Usafi wa Mazingira wa Wizara ya Afya na Ustawi Dkt. Elias Chinamo (kulia) kuonyesha namna moja ya kifaa cha kupimia joto la mwili wa Binadamu kinavyofanya kazi kwa kubaini dalili za Ugonjwa wa Ebola eneo la uwanja wa ndege wa Mwalimu Julius Nyerere jijini Dar es salaam.

Moja ya kifaa (kamera) nne zilizoagizwa na Serikali kupimia dalili za ugonjwa wa Ebola maeneo ya viwanja vya ndege. Kifaa hicho kina uwezo wa kutunza picha na kumbukumbu za msafiri, muda , joto la msafiri, tarehe aliyoingia nchini pia uwezo wa kupata takwimu kutoka kwenye hali ya majimaji au jasho la Binadamu pindi kinapoelekezwa kwake.

Naibu Waziri wa Afya Dkt. Kebwe Steven Kebwe akiongea na waandishi wa habari eneo la uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere wakati wa kupokea na kukabidhi vifaa vya kupima dalili za ugonjwa wa Ebola. Wengine ni Mkurugenzi Msaidizi wa Kitengo cha Dharula na Maafa (kulia) na Kaimu Mkurugenzi wa Bohari ya Dawa (MSD), Cosmas Mwaifani.

Naibu Waziri wa Afya Dkt. Kebwe Steven Kebwe akiangalia kwa karibu taarifa zilizorekodiwa na moja ya kifaa (kamera) nne zilizoagizwa na Serikali kupimia dalili za ugonjwa wa Ebola maeneo ya viwanja vya ndege.
Picha na Aron Msigwa –MAELEZO.

Na. Aron Msigwa –MAELEZO, Dar es salaam.

Sehemu ya vifaa vya kubaini hatua za awali za ugonjwa wa Ebola kwa kupima hali ya joto la mwili kwa wasafiri kutoka nje nchi wanaotumia viwanja vya ndege vilivyokuwa vimeagizwa na Serikali vimewasili jijini Dar es salaam.

Vifaa hivyo vinavyohusisha kamera 4 zenye uwezo wa kubaini joto la mwili wa msafiri kwa umbali wa mita 100 bila kumgusa muhusika vimewasili leo katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere jijini Dar es salaam kutoka nchini Afrika ya Kusini vilikonunuliwa.

Akikabidhi vifaa hivyo kwa wataalam wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dkt. Kebwe Steven Kebwe amesema kuwa kuwasili kwa vifaa hivyo ni moja ya juhudi za Serikali za kuhakikisha kuwa wananchi wanakuwa salama kwa kuuzuia ugonjwa huo kuingia nchini.

Amesema vifaa hivyo vitapelekwa katika maeneo ya viwanja vya ndege na maeneo yanayotumiwa na raia wa kigeni kuingia nchini vikiwemo vya Dar es salaam, Zanzibar, Kilimanjaro,Mbeya na Mwanza.

Ameongeza kuwa Serikali inaendelea na mpango wa kuagiza vifaa zaidi vya kuwezesha shughuli ya upimaji wa afya kwa wasafiri wanaotembea (scanners) zitakazowezesha kubaini afya za wasafiri wengi zaidi kwa wakati mmoja bila kulazimu kuwasimamisha.

Aidha, amewataka wataalam hao wa afya kufanya kazi zao kwa weledi mkubwa kwa kuhakikisha wanawapima abiria wote wanaotoka nje ya nchi bila kujali hadhi walizonazo ili kuweza kubaini kama wana maabukizi au dalili za ugonjwa wa Ebola.

“Nataka mfanye kazi yenu kwa kuzingatia weledi wa taaluma yenu na kwa kuzingatia yale mliyojifunza,mvitumie vifaa hivyo kupima kila abiria ili kubaini joto lake bila kujali cheo wala hadhi yake maana janga hili ni kubwa” Amesema Dkt. Kebwe.

Kuhusu utunzaji wa vifaa hivyo amewataka wataalam hao kuhakikisha wanavitunza vifaa hivyo ili viweze kudumu na kutimiza malengo yaliyokusudiwa ya kuwasaidia wananchi kutokana na vifaa hivyo kugharimu fedha nyingi kila kimoja.

Katika hatua nyingine Mh. Kebwe amefafanua kuwa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii inaendelea na shughuli ya utoaji wa Elimu ya Afya kuhusu ugonjwa wa Ebaola ili kuwawezesha wananchi kuchukua tahadhari na kuzielewa dalili za ugonjwa huo na namna ya kujingika endapo utagundulika nchini.

Amesema tayari kamati mbalimbali za wataalam zimeshaundwa ili kuwezesha zoezi la utoaji wa elimu na mafunzo kwa wataalam wa ndani ili kuwajengea uwezo wa kukabiliana na janga hilo.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Bohari ya Dawa nchini (MSD), Cosmas Mwaifwani ambaye ofisi yake imehusika katika uagizaji wa vifaa hivyo nchini Afrika ya Kusini amesema kuwa mahitaji ya vifaa hivyo kwa sasa yameongezeka kutokana na umuhimu wake na jinsi vinavyofanya kazi kwa ufanisi mkubwa.

Amesema upimaji kwa kutumia vifaa hivyo unatumia teknolojia ya kubaini mionzi ya joto kutoka katika mwili wa binadamu pindi vinapoelekezwa katika maeneo ya macho na masikio ya mwili wa binadamu.

Amefafanua kuwa vifaa hivyo vinauwezo wa kutunza picha na kumbukumbu za msafiri, muda , joto la msafiri na tarehe aliyoingia nchini na kuongeza kuwa vifaa hivyo vina uwezo wa kupata takwimu kutoka kwenye hali ya majimaji au jasho la Binadamu pindi kinapoelekezwa kwake.

Mwaifwani ameeleza kuwa MSD inaendelea kuimarisha uwezo wake kwa kuongeza vifaa zaidi kutoka Ubelgiji na China na kufafanua kuwa Bohari hiyo imejiandaa kukabiliana na ugonjwa wa Ebola kwa kujenga uwezo wa kuwa na dawa za kutibu hali ya magonjwa yanayoambatana na homa hiyo.

Naye Mkurugenzi wa Viwanja vya ndege nchini, Moses Malaki akizungumza kwa niaba ya Viwanja vya ndege nchini ameielezea hali hiyo ya upatikanaji wa vifaa katika maeneo hayo kuwa itaongeza ufanisi wa uchunguzi wa afya kwa wasafiri na kuondoa usumbufu kutokana na uwezo wa vifaa hivyo kumpima msafiri akiwa mbali.

Hakuna maoni :

Chapisha Maoni