.

.

.

.

.

.

.

.
KARIBUNI TUHABARIKE, TUELIMISHANE, TUPEANE HABARI ZA KUKUFANYA UTABASAMU KIDOGO NA MATUKIO YALIYOFANYIWA UCHUNGUZI WA KINA TOKA KILA PEMBE CONTACTS: +255 787 377 722 Email: drweyunga@gmail.com PIA UNAWEZA KUNI FOLLOW KUPITIA INSTAGRAM YANGU @drweyunga | TANGAZA NASI ILI UWAFIKIE WATU WENGI ZAIDI.

Ijumaa, 12 Septemba 2014

JK ATAKA MSAADA ESRF KUONDOA UMASKINI KWENYE UCHUMI UNAOKUA KWA KASI KUBWA

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi Huru ya Utafiti wa Uchumi na Jamii (ESRF), Dk. Hoseana Lunogelo akisalimiana na Mratibu Mkazi wa mashirika ya Umoja wa Mataifa na mwakilishi wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) nchini , Alvaro Rodriguez nje ya ukumbi wa mikutano kabla ya mgeni rasmi kuwasili kwenye mkutano mkubwa wa tatu wa ESRF unaozungumzia ukuaji wa uchumi kwa kutumia fursa zilizopo na maendeleo yanayogusa jamii uliofanyika jana jijini Dar katika hoteli ya Hyatt Regency, Kilimanjaro.(Picha zote na Zainul Mzige)
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete akilakiwa na Mwenyekiti wa Bodi ya ESRF, Philemon Luhanjo mara baada ya kuwasili kwenye hoteli ya Hyatt Regency, Kilimanjaro kufungua mkutano mkubwa wa tatu wa Taasisi Huru ya Utafiti wa Uchumi na Jamii (ESRF) unaozungumzia ukuaji wa uchumi kwa kutumia fursa zilizopo na maendeleo yanayogusa jamii.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete akisalimiana na Mratibu Mkazi wa mashirika ya Umoja wa Mataifa na mwakilishi wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) nchini, Alvaro Rodriguez.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete akitoa mkono wa pongezi kwa Mkurugenzi Mtendaji wa ESRF, Dk. Hoseana Lunogelo mara baada ya kusikiliza taarifa ya maendeleo ya ESRF.

Mwenyekiti wa Bodi ya ESRF Philemon Luhanjo, akizungumza neno fupi kabla ya kumrabisha mgeni rasmi Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kufungua rasmi mkutano huo.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete akifungua rasmi mkutano mkubwa wa tatu wa ESRF unaozungumzia ukuaji wa uchumi kwa kutumia fursa zilizopo na maendeleo yanayogusa jamii uliofanyika jana jijini Dar katika hoteli ya Hyatt Regency, Kilimanjaro.

Mwenyekiti wa Bodi ya ESRF, Philemon Luhanjo (kushoto) akiteta jambo na Mratibu Mkazi wa mashirika ya Umoja wa Mataifa na mwakilishi wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) nchini, Alvaro Rodriguez nje ya ukumbi wa mikutano kwenye hoteli ya Hyatt Regency, Kilimanjaro.


Mkurugenzi Mtendaji wa ESRF Dk. Hoseana Lunogelo (kushoto) akiongozana na Mratibu Mkazi wa mashirika ya Umoja wa Mataifa na mwakilishi wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) nchini , Alvaro Rodriguez kuelekea kwenye ukumbi wa mkutano.

Wageni waalikwa wakipitia ripoti mbalimbali zilizoandaliwa na ESRF nje ya ukumbi wa mikutano kabla ya kuwasili kwa mgeni rasmi.
Mratibu wa Programu kutoka ESRF, Yasser Manu (kulia) akibadilishana mawazo na baadhi ya wafanyakazi wenzake nje ya ukumbi wa mikutano kabla ya kuwasili kwa mgeni rasmi.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete akiwasili ukumbini kufungua mkutano mkubwa wa tatu wa Taasisi Huru ya Utafiti wa Uchumi na Jamii (ESRF) unaozungumzia ukuaji wa uchumi kwa kutumia fursa zilizopo na maendeleo yanayogusa jamii. Katikati ni Mratibu Mkazi wa mashirika ya Umoja wa Mataifa na mwakilishi wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) nchini, Alvaro Rodriguez.

Mkurugenzi Mtendaji wa ESRF, Dk. Hoseana Lunogelo akibadilishana mawazo na Balozi wa Japan nchini Tanzania,Mh. Masaki Okada wakati wakimsubiri mgeni rasmi kuwasili ukumbini hapo.

Na Mwandishi wetu

RAIS Jakaya Kikwete amewataka nguli wa masuala ya uchumi na maendeleo ya binadamu kuisaidia serikali kufanikisha azma yake ya maendeleo kwa wananchi hasa ikizingatiwa kwamba zipo raslimali za kutosha, uchumi unakua lakini umaskini haupungui.

Rais alisema hayo jana wakati akifungua mkutano mkubwa wa tatu wa Taasisi Huru ya Utafiti wa Uchumi na Jamii (ESRF) unaozungumzia ukuaji wa uchumi kwa kutumia fursa zilizopo na maendeleo yanayogusa jamii uliofanyika hoteli ya Hyatt Regency, Kilimanjaro.

Katika hotuba yake kwa wataalamu nguli hao ambao wanaangalia athari za kisera na kutoa ushauri katika masuala ya maendeleo yenye kulenga kunufaisha jamii, alisema katika miaka 10 iliyopita uchumi wetu umekua ukikua kwa kasi lakini hali hiyo haikuweza kusaidia kupunguza umaskini kama ulivyolengwa na serikali.

Alisema moja ya malengo ya millennia yalikuwa ifikapo mwaka wa kesho hali ya umaskini ipunguzwe angalua nusu yake, kwa kuongeza pato la mtu binafsi lakini hali sivyo ilivyo.

Rais ambaye alitumia muda mwingi kueleza maendeleo ya kiuchumi yaliyofikiwa katika hatua ya kuifikisha nchi hii miongoni mwa mataifa yenye kipato cha kati ifikapo mwaka 2025, alisema zinatakiwa juhudi kubwa ili kuondoa umaskini wa kipato kwa mtu mmoja mmoja.

“Pamoja na mafanikio makubwa yaliyopatikana katika ustawi wa jamii kama uandikishaji wa watoto shule, uzazi na upunguzaji wa vifo vya watoto, taifa bado linakabiliwa na changamoto kubwa ya ubora wa elimu, upunguzaji wa vifo kwa wanawake wazazi na utapiamlo” alisema Rais Kikwete.

Alisema kwa kuangalia takwimu hizo katika jamii na ukuaji wa uchumi ni dhahiri kwamba taifa letu ili kufikia malengo yake kuna mambo mengi yanatakiwa kufanyiwa kazi na kuamini kwamba wataalamu hao katika mada zao mbalimbali watakazojadiliana watatoka na kitu cha maana kuisaidia serikali kupata mwelekeo sahihi wa kufikia taifa lenye kipato cha kati ifikapo mwaka 2025.

Dira ya maendeleo ya mwaka 2025 ambayo inayotaka kuifanya Tanzania kuwa nchi ya kipato cha kati yenye maisha bora, utawala bora na uchumi wenye ushindani miongoni mwa mambo machache yenye upeo wa juu yaliyomo katika dira hiyo ndiyo yanayotumika kujadili na hatimaye kuipa serikali majawabu ya mambo muhimu yanayotikisa safari ya kuelekea huko.

Ili kufika huko kwa mujibu wa Rais Kikwete viashiria kadhaa vitaonekana ikiwa ni pamoja na kushuka kwa mchango wa kilimo kwa pato la taifa na ajira, kukua kwa sekta ya kisasa ya viwanda na huduma kwa uchumi, kukua kwa miji na mabadiliko katika vizazi na vifo ambapo taifa linaondoka katika vifo na uzazi wa fujo na kuwa na vizazi vidogo na vifo kidogo kutokana na kukua kwa elimu na huduma za afya.

Alisema mpango wa muda mrefu umelenga ifikapo mwaka 2025 mchango wa kilimo kwa pato la taifa utapungua kutoka asilimia 27.8 kufikia 20.7, mchango wa viwanda kupanda kutoka 24.4 hadi 30.7 na mchango wa huduma utapanda kutoka asilimia 47.8 ya mwaka 2010 hadi 48.6.

“Ni matumaini yangu kwamba wastani wa idadi ya watu ikipungua kutokana na elimu na huduma safi za afya au ukuaji wa kasi wa pato la taifa kuliko ongezeko la watu na hivyo kipato kitaongezeka na umaskini utapungua”

Miaka 10 iliyopita mchango wa kilimo katika pato la taifa umekuwa mkubwa huku vizazi na vifo vikiwa ni vingi.

Mkutano huo ambao unajadili mabadiliko ya kiuchumi kwa ajili ya maendeleo ya jamii unatokana na ripoti ya mradi wa maendeleo ya jamii (THDR) iliyofadhiliwa na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP).

Naye Mratibu Mkazi wa mashirika ya Umoja wa Mataifa na mwakilishi wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) nchini , Alvaro Rodriguez akizungumza kwa niaba ya Umoja wa Mataifa katika mkutano huo amesema Umoja wa Mataifa utaendelea kuisaidia Tanzania kutengeneza ustawi kwa wananchi wake.

Alisema pamoja na kuwapongeza ESRF kwa kuandaa mkutano huo muhimu wa kuipatia serikali fikira za namna ya kuboresha hali za wananchi wake.

Alisema amefurahishwa kwa ESRF kusaidia kutafuta mustakabali wa maendeleo kwa minajili ya kuendeleza wananchi kwani maendeleo ya kweli ni yale yanayoboresha maisha ya wananchi.

Aidha alivitaja vigezo muhimu vya maendeleo ya jamii katika hali ya uchumi unaokua ambavyo ni kuhakikisha kwamba kuna usawa katika ukuaji wa uchumi na maisha ya wananchi, kuongeza uwezo wa kuhami maendeleo yaliyofikiwa dhidi ya haki zisizotabirika zinazovuruga ustawi,Kuhakikisha maendeleo endelevu ya wananchi na nchi na kuendelea kuwasaidia wanaume kwa wanawake kushiriki kikamilifu katika mchakato wa maendeleo iwe kiuchumi, kijamii na kisiasa na kugawana kwa usawa matunda ya maendeleo.

Amesema Mratibu huyo wa mashirika ya Umoja wa Mataifa nchini kwamba amefurahishwa na taarifa kwamba mkutano huo utajadili mada mbalimbali na kutolea ushauri kwa kuzingatia taarifa ya THDR.

Awali akimkaribisha Mwenyekiti wa Bodi ya ESRF Philemon Luhanjo, kumkaribisha rais Jakaya Kikwete Mkurugenzi Mtendaji wa ESRF Dk Hoseana Lunogelo alisema wakati taasisi hiyo inaadhimisha miaka 20 ya uwepo wake, katika mkutano wake wa 3 wa kitaifa wanatarajia wanazuoni kuchambua mada mbalimbali na kuandika kitu kitakachosaidia serikali katika kuhakikisha maendeleo ya kiuchumi yanakwenda sanjari na ustawi wa jamii kwa maana ya kuondokana na umaskini katika ngazi ya mtu mmoja mmoja.

Mada zinazochambuliwa zinatoka kwa wataalamu waliobobea kutoka Tanzania,Ethiopia, Uingereza, Norway na India.

Hakuna maoni :

Chapisha Maoni