WAZIRI MKUU Mizengo Pinda amesema
mchakato wa Bunge la Katiba unaoendelea hivi sasa ni halali na kwamba
mchakato huo ni wa kisheria.
Ametoa kauli hiyo leo mchana (Jumapili,
Septemba 21, 2014) wakati akizungumza na mamia ya waumini na viongozi
mbalimbali waliohudhuria ibada ya uzinduzi wa dayosisi mpya ya Ziwa
Tanganyika ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) na
kuwekwa wakfu Askofu Ambele Anyigulile Mwaipopo aliyeteuliwa kuongoza
dayosisi hiyo.
Dayosisi hiyo inakuwa ya 24 kwa kanisa hilo.
Waziri Mkuu alikuwa akitoa ufafanuzi wa
hoja ya Askofu Mwaipopo aliyetaka maoni ya Tume ya Mabadiliko ya
Katiba yaheshimiwe na Bunge Maalum la Katiba lisitishwe kama ambavyo
Jukwaa la Katiba limetaka na tamko la Jumuiya za Kikristo Tanzania
(CCT) limetamka.
Waziri Mkuu alisema: “Rasimu ya
Katiba iliyowasilishwa na Tume hiyo siyo Katiba bali mawazo
yaliyokusanywa ambayo yanapaswa kupitiwa na chombo kingine cha
kisheria ambacho ni Bunge Maalum la Katiba. Mchakato huu halali na
mchakato huo ni wa kisheria.”
Alisema muda ambao Tume hiyo ilipewa
haukuwa mrefu sana kwa hiyo isingekuwa rahisi kwao kuzingatia kila
eneo linalogusa maisha ya Watanzania. “Mfano suala la ardhi
halikuelezwa vizuri katika rasimu lakini kwa sasa limeelezwa vizuri
jinsi ardhi inavyoweza kumnufaisha Mtanzania kwenye kilimo, ufugaji,
uvuvi na rasilmali misitu,” alisema.
Alisema kinachowachanganya Watanzania
ni suala la Serikali mbili au tatu lakini katika makabrasha ya Tume
ambayo wajumbe wote walipewa, suala la Muungano halikupewa kipaumbele
na Watanzania wengi waliotoa maoni yao. “Kulikuwa na masuala
makubwa sita. Suala la ukiukwaji wa haki za binadamu ndilo lilikuwa
namba moja, suala lililopewa umuhimu wa pili lilikuwa ni la matatizo
ya huduma za jamii na hilo la muungano lilichangiwa na kundi dogo
sana,” alisema.
Alisema kwa mujibu wa takwimu za Tume
ya Jaji Warioba watu waliotaka Muungano wa Serikali tatu ni kati ya
asilimia 12 na 13. “Haiwezekani kwa takwimu zile za asilimia 12
hadi 13 za kutaka Serikali tatu, iamuliwe jumla kwamba ni kwa niaba
ya Watanzania wengi.”
Ili kukidhi shauku ya wengi, Waziri
Mkuu alisema yuko radhi ifanyike kura mahsusi ya kuwaomba Watanzania
waseme kama wanataka Muungano na tena uwe ni wa aina gani.
“Baba Askofu amesema tusitishe Bunge
la Katiba, hivi sababu hasa ya kusitisha ni nini? Je sote tunajua
hoja iliyowafanya wenzetu watoke nje na kususia ni ipi? Katika muda
wa kuchangia kulikuwa na dakika 40 za wengi, dakika 20 za wachache na
wakapewa dakika nyingine 30 za kuchangia. Muda ule ni mwingi mno kama
hujaweka mchango wako kwenye maandishi. Badala yake, sote
tulishuhudia kukashifiana, kejeli na kukashifiana.”
Aliwasihi Maaskofu, wachungaji na
viongozi wengine wa dini waliohudhuria uzinduzi huo waendelee kuumboe
mchakato huo ili uishe vizuri.
Katika hotuba yake, Waziri Mkuu
alimuomba Askofu huyo mpya apokee jukumu hilo kwa mikono miwili na
kumuahidi kuwa Serikali itasaidiana naye kuwaongoza Watanzania
walioko kwenye dayosisi yake. Dayosisi hiyo mpya inahusisha mikoa ya
Rukwa na Katavi eneo ambalo lina ukubwa wa kilometa za mraba 75,140.
Kati ya hizo km. za mraba 27,713 ni za mkoa wa Rukwa na km. za mraba
47,527 ni za mkoa wa Katavi.
Alisema katika dayosisi hiyo mpya kuna
changamoto nyingi kama vile za malezi ya vijana na watoto, tabia ya
watu kutopenda kufanya kazi hasa vijana, kukosekana kwa injili kwenye
maeneo wanayoishi wafugaji na suala la imani za ushirikina.
“Asilimia kubwa ya Watanzania ni
vijana na wao ndiyo Taifa la leo. Ukiangalia mavazi ya vijana wa kike
(vimini) na wa kiume (mlegezo) hutamani kuwaangalia mara ya pili.
Msingi mkubwa wa kuwabadilisha hawa wote ni malezi ya kiroho. Una
changamoto pia ya kufikisha neno la Mungu kwa wafugaji ambao ni wengi
eneo hili lakini hawana muda wa kuabudu na wengi wao hawalijui neno
la Mungu, wako bize na mifugo yao.”
“Lakini changamoto kubwa kuliko zote
ni ya kubadili mtazamo wa jamii kuhusu Mkoa wa Rukwa hasa kwenye
suala la ushirikina. Mtu hata kama hatoki huku bado ataweka bango
akisema Mganga machachari kutoka Sumbawanga. Baba Askofu naomba
tushirikiane kupiga sana vita imani hizi potofu kwa sababu
zinachangia mauaji ya wazee na walemavu wa ngozi,” alisisitiza
Waziri Mkuu.
Mapema, akitoa hotuba yake ya kwanza
mara baada ya kusimikwa rasmi, Askofu Mwaipopo aliiomba Serikali
isifumbie macho viashiria vyote vya upotevu wa amani kwani amani ni
tunda la upendo na wala haipatikani kwa ncha ya upanga.
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU
DAR ES SALAAM.
JUMAPILI, SEPTEMBA 21, 2014
Hakuna maoni :
Chapisha Maoni