Waziri wa Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi Zanzibar, Mhe. Hamad Rashid Mohamed (kushoto) akimkabaribisha Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo ya Tanzania (TADB), Bw. Francis Assenga (kulia) wakati walipomtembelea Ofisini kwake mjini Unguja.
Na Mwandishi wetu,
Waziri wa Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi Zanzibar, Mhe. Hamad Rashid Mohamed amesema sasa ni wakati muafaka kwa Benki ya Maendeleo ya Kilimo ya Tanzania (TADB) kuwekeza Visiwani Zanzibar ili kuchagiza juhudi za Serikali za kuwawezesha kiuchumi wakazi wa visiwa hivyo wanaojishughulisha na sekta za kilimo, uvuvi na uchakataji mazao.
Mhe. Hamad amesema Visiwa vya Zanzibar vina maeneo mengi ya uwekezaji yenye kuweza kuongeza tija na ongezeko la uchumi visiwani humo ikiwa kutakuwa na uwekezaji mkubwa katika maeneo hayo.
“Nawahakikishia, mkianza kuwekeza katika miradi kama ya mwani, uvuvi na karafuu Bebki itapata matokeo makubwa sana na mnaweza kuitumia Zanzibar kama mfano rejea katika utoaji wa mikopo yenye tija nchini,” alisihi.
Kwa mujibu wa Mhe. Waziri, Zanzibar ni miongoni mwa visiwa vyenye utajiri mkubwa ambavyo kukiwa na uwekezaji wa kimkakati vinaweza kutokea matokeo makubwa na yenye kuwanufaisha wananchi wengi.
Akizungumza na Mhe. Waziri, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa TADB, Bw. Francis Assenga amesema Serikali iliamua kuanzisha Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) ili kusaidia kukabiliana na mapungufu ya wakulima nchini kote ili kuhuisha upatikanaji wa mikopo katika sekta ya kilimo na kuchagiza mapinduzi katika kilimo nchini.
Bw. Assenga ameongeza kuwa Benki inatambua fursa za uwekezaji Visiwani Zanzibar na amemuahidi kuwa wamejipanga kuanza uwekezaji mkubwa wa wadau wa sekta za kilimo na uvuvi ambazo ni sekta za kipaumbele zinazopatiwa mikopo na TADB.
Ameongeza kuwa Benki yake imejipanga kuendeleza uongezaji wa thamani wa sekta hizo ili kuongeza tija sekta hizo ili kupambana na umaskini nchini.
TADB ni taasisi ya serikali ambayo ilianzishwa kwa ajili ya kutatua ufinyu mkubwa wa upatikanaji wa fedha mikopo kwa ajili ya maendeleo ya kilimo nchini ambao ulikuwa unachangiwa kwa kiasi kikubwa na mikopo mingi kutoka taasisi za fedha kuelekezwa zaidi kwenye upande wa biashara za bidhaa; riba kubwa kwenye mikopo ya kilimo; mikopo ya muda mfupi; masharti magumu ya kukopa bila kuzingatia hali halisi ya sekta ya kilimo na mazao ambayo inaathiriwa kwa kiasi kikubwa na mabadiliko ya hali ya hewa.
Hakuna maoni :
Chapisha Maoni