.

.

.

.

.

.

.

.
KARIBUNI TUHABARIKE, TUELIMISHANE, TUPEANE HABARI ZA KUKUFANYA UTABASAMU KIDOGO NA MATUKIO YALIYOFANYIWA UCHUNGUZI WA KINA TOKA KILA PEMBE CONTACTS: +255 787 377 722 Email: drweyunga@gmail.com PIA UNAWEZA KUNI FOLLOW KUPITIA INSTAGRAM YANGU @drweyunga | TANGAZA NASI ILI UWAFIKIE WATU WENGI ZAIDI.

Jumamosi, 3 Juni 2017

BALOZI SEIF ATAKA UFUMBUZI WA KUDUMU UPATIKANE BAINA YA MWEKEZAJI NA WANANCHI WA ENEO LA PWANI YA MTONI

Mkuu wa Mkoa Mjini Magharibi Mh. Ayoub Mohamed Mahmoud kati kati akimuonyesha Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi maeneo yalioathirika na mawimbi la Maji ya Bahari katika Pwani ya Mtoni.
Balozi Seif Ali Iddi akikagua baadhi ya maeneoyaliyoathirika na kasi ya maji ya Bahari na kusababisha mmong’onyoko wa ardhi ulioathiri baadhi ya Nyumba za Mtaa huo wa Asili.
 Sheha wa Shehia ya Mtoni Bwana Hassan Zaid Ali wa kwanza kutoka Kushoto akielezea athari za mmong’onyoko wa ardhi zinazolikumba eneo la Pwani ya Mtoni toke asili.
Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Tathmini ya Athari zaKimazingira Ndugu Ali Vuai Pandu akitoa ufafanuzi wa tathmini ya awali iliyofanywa na Wataalamu wa Kitengo chek katika eneo la Pwani ya Mtoni mbele ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi.
Mzee wa Mtaa wa Pwani ya Mtoni Bwana Yussu Amour Abdulla akimueleza Balozi Seif changamoto zinazowakumba Wananchi wa eneo hilo za kuongezeka kwa kina cha Maji ya Bahari na kuathiri makaazi yao.

                                                                                                    Picha na – OMPR – ZNZ.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi ameziagiza Taasisi zote zinazohusika na usimamizi wa Mazingira, Halmashauri ya Wilaya pamoja na Wananchi wa Mwambao wa Pwani ya Mtoni kukaa pamoja na Muwekezaji wa mradi wa Hoteli ya Kimataifa inayojengwa Mtoni Marine ili kulitafutia ufumbuzi wa kudumu tatizo la athari ya maji ya Bahari yanayolikumba eneo hilo.


Alisema hatua hiyo itatoa muelekeo mzuri wa pamoja utakaoepusha migogoro kwa kuzingatia maslahi ya pande zote mbili ile ya Muwekezaji pamoja na Wananchi wa Eneo la Pwani ya Mtoni.

Balozi Seif Ali Iddi alitoa agizo hilo alipofanya ziara fupi ya kukagua eneo la Pwani ya Mtoni na kusikiliza malalamiko yaWananchi wa sehemu hiyo kufuatia maji ya bahari kuvamia maeneo yao na kuleta athari kubwa ya kimazingira bila ya kujua hatma yao ya hapo baadae.

Alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itakuwa tayari kupokea ushauri wa pande hizo pamoja na kusubiri ripoti ya awali ya Kitaalamu inayofuatilia mwenendo mzima ya athari za kimazingira katika eneo hilo katika kipindi cha Miaka Kumi iliyopita.

Balozi Seif aliwataka ma kuwaomba Wananchi hao kuwa na subra wakati
Serikali yao ikiendelea kulitafutia ufumbuzi tatizo hilo linalohitaji umakini mkubwa hasa ikizingatiwa mabadiliko ya kimaumbile ya mazingira yanayojitokeza na kuathiri mambo mbali mbali Nchini.

Mapema akitoa ushauri wa athari zinazolikumba eneo hilo na mabadiliko
yake yanayojitokeza Mzee Yussuf Amour Abdulla alisema Mji wa Pwani ya
Mtoni upo tokea Karne ya 18 wakati eneo hilo lilikuwa njia ya Reli.

Mzee Yussuf alisema zipo nyumba zilizoathirika kwa kukatika na nyengine kubomoka kutokana na kasi ya maji ya Bahari katika kipindi hichi jambo ambalo limewatia wasi wasi wa hatma yao na vizazi vyao hapo baadae.

Alisema ipo mito miwili iliyokuwa akiingiza na kutoa maji ya habari
 wakati wa maji Makuu lakini kilichojitokeza wakati huu ni sehemu ndogo
iliyosalimika na maji ya bahari kutokana na uwepo wa miti ya Mikoko.

Mwakilishi huyo wa Wananchi wa Mtaa wa Pwani ya Mtoni aliishukuru na
kuipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Viongozi wake kwa umakini wake mkubwa inayoendelea kuuchukuwa wa kuwajali Wananchi wake inaowaongoza.

Alisema kitendo cha Viongozi hao kuanzia ngazi ya Juu, Kati, Mkoa hadi Wilaya kimethibitisha hali hiyo jambo ambalo kwao limekuwa likileta
faraja na kuwapa muelekeo wa maisha ya matumaini.

Akitoa ufafanuzi wa Kitaalamu Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Tathmini ya Athari za Kimazingira Ndugu Ali Vuai Pandu alisema uchunguzi wa awali
uliofanywa na Wataalamu kuhusu athari za Kimazingira wa eneo hilo
umeonyesha dalili zitazojichomoza za athari za Mazingira katika Pwani
ya Mtoni.

Nd. Ali alisema kipimo cha madhara ambayo yanajitokeza wakati wa uendelezaji wa mradi kwa mujibu wa Mikataba inayofungwa kinamuwajibika
muwekezaji kuondosha kasoro zinazojichomoza ambazo zina muelekeo wa
kuathiri jamii ya eneo husika.

Hata hivyo Kaimu Mkuu huyo wa Kitengo cha Tathmini ya Athari za Kimazingira alifafanua wazi kwamba Hali ya Hewa ya Kimaumbile nayo
imekuwa ikichangia madhara yanayojichomoza sehemu mbali mbali
kunakosababisha na mabadiliko ya Tabia Nchi.

Mapema Sheha wa Shehia ya Mtoni Bwana Hassan Zaid Ali alimueleza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif kwamba hali ya mmong’onyoko wa ardhi katika Pwani ya Mtoni umekuwepo tokea asili.

Bwana Hassan alisema mmong’onyoko huo ulikuwa akisababishwa na kasi ya
maji ya bahari kulingana na Bamvua la msimu wa mabadiliko ya upepo, lakini hivi sasa kasi ya Mmong’onyoko huo inaonekana kuongezeka zaidi
na kutia wasi wasi.

Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
3/6/2017.

Hakuna maoni :

Chapisha Maoni