“Tamaa yangu, na kwa kweli jitihada za Serikali ya Awamu ya Tano, zitakuwa katika ujenzi wa uchumi wa kipato cha kati ambapo sura na maisha ya Watanzania walio wengi yafanane fanane na nchi ya kipato cha kati. Njia moja ya kutufikisha huko ni uendelezaji wa viwanda.”
Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, Tarehe 20 Novemba 2015, BUNGENI, DODOMA.
UTANGULIZI
1.
Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja
kwamba Bunge lako Tukufu lipokee na kujadili Taarifa ya Hali ya Uchumi kwa
Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa 2017/18. Pamoja na hotuba hii
nawasilisha vitabu vya Taarifa ya Hali ya Uchumi kwa Mwaka 2016 na Mpango wa
Maendeleo wa Taifa 2017/18, ambapo taarifa hizi ndio msingi wa bajeti ya
Serikali kwa mwaka 2017/18 itakayowasilishwa Bungeni baadaye hivi leo.
3.
Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kutoa
pole kwako, Waheshimiwa Wabunge wote na wananchi kwa kuondokewa na wabunge
wenzetu, Mheshimiwa Hafidh Ally Tahir aliyekuwa Mbunge wa Dimani (CCM) na Mheshimiwa
Dkt. Elly Marko Macha, Mbunge wa Viti maalum (CHADEMA). Pia, nitumie fursa hii
kuwapa pole wabunge wote waliopoteza wapendwa wao na wananchi wote waliopatwa
na maafa mbalimbali katika mwaka huu, yakiwemo matukio ya kusikitisha ya
kuondokewa na watoto wetu 32, walimu wawili na dereva wa shule ya Lucky Vincent
katika ajali mkoani Arusha mwezi uliopita, wanafunzi watatu kule mkoani Geita, wanafunzi
wawili na mzazi mmoja mkoani Kagera kwa kuzama majini na Askari wetu nane na
wananchi wengine waliouawa kikatili katika matukio ya kupanga mkoani Pwani.
Tunamwomba Mwenyezi Mungu aziweke roho za marehemu mahali pema, peponi.
4.
Mheshimiwa Spika, kipekee kabisa, napenda
kumpongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania na wasaidizi wake wakuu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais
na Mheshimiwa Kassim M. Majaliwa (Mb), Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, kwa uongozi madhubuti kusimamia mabadiliko yanayoleta tija katika
utendaji Serikalini, kuharakisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii nakuendeleza misingi
ya utawala bora. Uongozi wao umejipambanua katika kupambana na rushwa, ufisadi,
ukwepaji kodi, uzembe na urasimu katika utumishi wa umma na ubadhirifu wa mali za
umma lakini pia msisitizo wa umuhimu wa kila mwananchi kufanya kazi. Juhudi hizi
zinapaswa kuungwa mkono kwa nguvu zote na viongozi na Wananchi wote.
5.
Mheshimiwa Spika, niruhusu pia
niwapongeze kwa dhati wabunge wapya walioingia Bungeni katika mkutano huu wa 7
wa Bunge la 11 ambao ni: Mheshimiwa Salma R. Kikwete, Mheshimiwa Dkt. Gertrude
Pangalile Rwakatare, wote wa CCM na Mheshimiwa Dkt. Catherine Ruge wa CHADEMA.
Tunawakaribisha kuungana na Waheshimiwa Wabunge wengine kutekeleza wajibu wa
msingi wa Bunge wa kuishauri na kuisimamia Serikali kwa hekima na weledi na
kuweka mbele maslahi ya Taifa kwa manufaa ya Watanzania. Nawapongeza pia
Waheshimiwa Wabunge kutoka vyama vyote waliochaguliwa na Bunge hili
kuiwakilisha nchi yetu katika Bunge la Afrika Mashariki. Matarajio yetu ni kuwa
watalinda na kusimamia na kutetea vema maslahi ya nchi yetu katika Bunge hilo
la Afrika Mashariki.
6.
Mheshimiwa Spika, naomba nitumie fursa
hii kuishukuru sana Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti, inayoongozwa na Mheshimiwa
Hawa Abdulrahman Ghasia, Mbunge wa Mtwara Vijijini; na Makamu wake, Mheshimiwa
Josephat Sinkamba Kandege, Mbunge wa Kalambo, kwa maelekezo na ushauri wa
kizalendo waliotupatia, ambao umesaidia kuboresha taarifa za mwenendo wa uchumi
wa Taifa kwa mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2017/18, ninazoziwasilisha.
7.
Mheshimiwa Spika, hotuba ninayoiwasilisha
imegawanyika katika maeneo makuu matano (5): eneo la kwanza ni utangulizi, la pili
ni taarifa ya mapitio ya Hali ya Uchumi kwa mwaka 2016 na robo ya kwanza ya
2017; eneo la tatu, ni Muhtasari wa Mapitio ya Utekelezaji wa Mpango wa
Maendeleo wa Taifa wa 2016/17; nne, ni Maeneo ya Kipaumbele ya Mpango wa Taifa
wa Maendeleo kwa mwaka 2017/18; na mwisho, ni Majumuisho.
MWENENDO WA HALI
YA UCHUMI 2016
Uchumi wa Dunia
8.
Mheshimiwa Spika, Kasi ya ukuaji wa
uchumi wa dunia kwa mwaka 2016, ilikuwa asilimia 3.1 ikilinganishwa na asilimia
3.2 mwaka 2015. Kupungua huku ni matokeo ya kupungua kwa ukuaji wa uchumi katika
nchi zilizoendelea, ambapo ukuaji wa uchumi kwa nchi zilizoendelea kilikuwa
asilimia 1.7 mwaka 2016 ikilinganishwa na asilimia 1.9 mwaka 2015, ukichangiwa na
kushuka kwa mahitaji ya bidhaa na huduma katika masoko mengi duniani na
kupungua kwa tija ya uzalishaji na kasi ya uwekezaji. Kasi ya ukuaji wa uchumi
kwa nchi zinazoendelea ilikuwa asilimia 4.1 sawa na ilivyokuwa mwaka 2015.
Ukuaji huu kwa nchi zinazoendelea ulichangiwa zaidi na kupungua kwa ukuaji wa
uchumi kwa nchi za China na Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara kufuatia kuporomoka
kwa bei za bidhaa hasa bidhaa ghafi katika soko la dunia, kupungua kwa
uwekezaji wa moja kwa moja wa sekta binafsi na kushuka kwa mahitaji ya bidhaa zinazozalishwa
katika masoko mengi duniani.
9.
Mheshimiwa Spika, mfumuko wa bei duniani
uliongezeka kufikia wastani wa asilimia 2.9 mwaka 2016 ikilinganishwa na
asilimia 2.8 mwaka 2015. Kwa kiasi kikubwa mfumuko wa bei uliongezeka kutokana
na kulegezwa kwa sera za bajeti na fedha kwa baadhi ya nchi na ukame uliochangiwa
na mabadiliko ya hali ya hewa (yanayojulikana kama La Nina). Mfumuko wa bei kwa nchi zilizoendelea uliongezeka kufikia
asilimia 0.8 kwa mwaka 2016 ikilinganishwa na asilimia 0.3 mwaka 2015, ambapo
kwa nchi zinazoendelea za Asia, uliongezeka hadi asilimia 3.1 kutoka asilimia
2.7 mwaka 2015. Kwa nchi za Afrika, Kusini mwa Jangwa la Sahara, ulifikia
asilimia 11.4 ikilinganishwa na asilimia 7.0 mwaka 2015.
Uchumi wa Afrika na Kikanda
10. Mheshimiwa Spika, kwa upande wa nchi za Afrika, Kusini mwa Jangwa la Sahara, wastani wa kasi
ya ukuaji wa uchumi ilipungua kutoka asilimia 3.4 mwaka 2015 hadi asilimia 1.4
mwaka 2016. Hii ni kutokana na kupungua kwa upatikanaji wa mikopo kutoka kwenye
masoko ya kimataifa uliosababisha miradi iliyopangwa katika kipindi hicho kushindwa
kukamilika, kuendelea kwa migogoro ya kisiasa kwa baadhi ya nchi (Burundi, Libya, Chad,
Sudan Kusini na DRC), na kuporomoka kwa bei za baadhi ya mazao ghafi, hususan, dhahabu
na mafuta ya petroli.
11. Mheshimiwa Spika, kasi ya ukuaji wa uchumi katika Jumuiya ya Afrika Mashariki ilishuka
kutoka wastani wa asilimia 6.5 mwaka 2015 hadi asilimia 5.3 mwaka 2016
ijapokuwa Jumuiya hii iliendelea kuongoza kwa ukuaji miongoni mwa Jumuiya
mbalimbali za Afrika. Kasi ndogo ya ukuaji wa uchumi katika Jumuiya hii ilichangiwa
na sababu mbalimbali ikiwemo kushuka kwa bei za bidhaa na kudorora kwa uchumi
wa dunia. Maoteo ya mwenendo wa uchumi katika ukanda huu yanaonesha utakua kwa wastani
wa asilimia 5.7 mwaka 2017 na asilimia 6.0 mwaka 2018. Matarajio haya
yanazingatia hatua zinazochukuliwa na nchi za ukanda huu katika kuboresha
mazingira ya uwekezaji na uendeshaji biashara kama vile kuwa na maeneo tengefu
ya ujenzi wa viwanda (industrial parks), hususan, vya nguo, bidhaa za ngozi,
kilimo, madawa na vifaa tiba.
12. Mheshimiwa Spika, Mfumuko wa bei katika nchi za Afrika Mashariki kwa mwaka 2016 uliendelea
kuwa wa kiwango cha tarakimu moja, ambapo Rwanda ilikuwa na asilimia 7.1,
Uganda asilimia 5.4, Tanzania asilimia 5.2, Kenya asilimia 6.3 na Burundi
asilimia 5.6. Aidha, kufikia Machi 2017, mfumuko wa bei kwa nchi hizi ulipanda,
ambapo kwa Burundi ulifikia asilimia 21.10, Rwanda asilimia 13.0; Kenya
asilimia 10.28; Uganda asilimia 6.4 na Tanzania asilimia 6.4. Hali hii
ilichangiwa na ukame katika maeneo mengi ya ukanda huu kutokana na kuchelewa
kwa msimu wa mvua.
13. Mheshimiwa Spika, kwa nchi za Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika, yaani SADC, kasi ya
ukuaji wa uchumi ilishuka kutoka wastani wa asilimia 1.9 mwaka 2015 hadi asilimia
1.1 mwaka 2016. Kasi ndogo ya ukuaji wa uchumi katika Jumuiya hii ilichangiwa
na uhaba wa nishati ya umeme pamoja na ukame uliochangiwa na mabadiliko ya hali
ya hewa ya La Nina. Licha ya kasi
ndogo ya ukuaji, Jumuiya hii iliendelea kuwa ya tatu kwa ukuaji miongoni mwa
Jumuiya za barani Afrika na unatarajiwa kukua kwa wastani wa asilimia 1.4 mwaka
2017. Mfumuko wa bei ulifikia asilimia 10.5 mwaka 2016 ikilinganishwa na asilimia
5.7 mwaka 2015, ukichangiwa na ukame na kuyumba kwa utekelezaji wa sera za mapato
na matumizi kwa baadhi ya nchi wanachama. Matarajio ni kuwa kwa mwaka 2017 mfumuko
wa bei utapungua hadi kufikia asilimia 8.7 kutokana na kushuka kwa gharama za
bidhaa, kuimarika kwa upatikanaji wa nishati ya umeme, na uthabiti wa bei ya
mafuta; na kuimarika kwa hali ya hewa.
Uchumi wa Taifa
Ukuaji wa Uchumi na Pato la Taifa
14. Mheshimiwa Spika, Pato la Taifa lilikua kwa wastani wa asilimia 7.0 kwa mwaka 2016, kama
ilivyokuwa mwaka 2015. Kiwango hiki hata hivyo ni chini ya maoteo ya kufikia
asilimia 7.2 kutokana na ukuaji wa baadhi ya shughuli kushindwa kufikia maoteo
ya viwango vya ukuaji. Baadhi ya shughuli za kiuchumi ambazo zilishindwa
kufikia maoteo ya viwango vya ukuaji ni pamoja na: sekta ya kilimo iliyokua kwa
asilimia 2.1 ikilinganishwa na maoteo ya asilimia 2.9; biashara na matengenezo
asilimia 6.7 dhidi ya asilimia 7.8; huduma za malazi na chakula asilimia 3.7
kinyume na maoteo ya asilimia 8.0; na huduma za utawala asilimia 2.1
ikilinganishwa na maoteo ya asilimia 6.3. Aidha, zipo shughuli za kiuchumi
zilizokua na hata kuzidi maoteo. Shughuli za uchumi zilizokuwa na viwango
vikubwa vya ukuaji ni pamoja na: habari na mawasiliano asilimia 13.0 dhidi ya
maoteo ya asilimia 12.1; usafirishaji na uhifadhi mizigo asilimia 11.8 dhidi ya
maoteo ya asilimia 8.0; uchimbaji madini na mawe asilimia 11.5 dhidi ya maoteo
ya asilimia 9.2; na uzalishaji viwandani asilimia 7.8 ikilinganishwa na maoteo
ya asilimia 6.7.
Mchango wa Kisekta katika Pato la Taifa
15. Mheshimiwa Spika, mchango wa shughuli za kilimo (mazao, ufugaji, misitu na uvuvi) katika
Pato la Taifa ulikuwa asilimia 29.1 mwaka 2016 ikilinganishwa na asilimia 29.0
mwaka 2015. Shughuli za viwanda na ujenzi zilichangia asilimia 25.2 ya Pato la
Taifa mwaka 2016 ikilinganishwa na asilimia 24.3 mwaka 2015, ambapo mchango wa
sekta za huduma (ikijumuisha biashara na matengenezo, usafirishaji na uhifadhi
mizigo, malazi, habari na mawasiliano, fedha na bima, upangishaji majumba,
elimu na afya) ulikuwa asilimia 39.1 mwaka 2016 ikilinganishwa na asilimia 40.0
mwaka 2015. Kuongezeka kwa mchango wa shughuli za viwanda, ni dalili kuwa azma
ya Serikali ya kujenga uchumi wa viwanda imeanza kuleta matokeo chanya, ambapo
tija na uzalishaji viwandani unaimarika. Pamoja na mambo mengine, hii inatokana
na kuimarika kwa upatikanaji wa miundombinu, hususan, nishati na usafiri.
Wastani wa Pato la Kila Mtu
16. Mheshimiwa Spika, Pato la Taifa kwa mwaka 2016 lilifikia Shilingi milioni 103,744,606 (kwa
bei za mwaka husika). Kiasi hiki cha Pato kikigawiwa kwa idadi ya watu
wanaokadiriwa kuwepo Tanzania Bara, ya watu 48,676,698, inafanya wastani wa
Pato la kila mtu kufikia Shilingi 2,131,299 ikilinganishwa na wastani wa Shilingi
1,918,897 mwaka 2015, sawa na ongezeko la asilimia 11.1. Hata hivyo, katika
thamani ya Dola za Marekani, wastani wa Pato la kila mtu liliongezeka kidogo kutoka
Dola 967.5 mwaka 2015 hadi Dola 979.1 mwaka 2016, ikimaanisha kuwa bado kuna
hatua ili kuingia katika kundi la uchumi wa kati. Kiwango cha chini cha uchumi
wa kati ni kufikia Dola 1,043. Hivyo basi, kasi ya ongezeko la Pato la
mwananchi katika thamani ya Dola haina budi kuongezeka. Hii itawezekana kwa
kutanzua changamoto zilizopo hususan, uzalishaji na tija katika sekta
zinazoajiri wananchi wengi hasa kilimo cha mazao, ufugaji na uvuvi.
Mwenendo wa Bei
17. Mheshimiwa Spika, Kwa miaka minne mfululizo, wastani wa mfumuko wa bei nchini umeendelea
kupungua, ukibaki katika kiwango cha tarakimu moja. Kwa mwaka 2016, mfumuko wa
bei ulifikia wastani wa asilimia 5.2 ikilinganishwa na asilimia 5.6 mwaka 2015.
Kupungua kwa wastani wa mfumuko wa bei nchini kulichangiwa kwa kiasi kikubwa
na: mwenendo wa kushuka wa bei za mafuta ya petroli katika soko la dunia na nchini;
kuimarika kwa upatikanaji wa vyakula nchini na hivyo wastani wa bei; na kuwepo
kwa sera madhubuti za usimamizi wa bajeti na fedha. Mfumuko wa bei uliongezeka
kidogo, ambapo ulifikia asilimia 6.4 mwezi Aprili 2017 lakini ukiwa ndani ya
maoteo ya wastani wa tarakimu moja (asilimia 5 – 8) kwa mwaka 2017. Hali ya kuongezeka
kwa mfumuko wa bei nchini ilichangiwa na hofu iliyotokana na kuchelewa kwa
msimu wa mvua katika maeneo mengi nchini na hivyo kuwepo kwa taharuki ya
kutokea upungufu wa chakula. Hata hivyo, maeneo mengi yamepata mvua ya kutosha
na hivyo bei ya chakula nchini
inatarajiwa kuimarika.
18. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2016 viwango vya riba za amana na mikopo vilipungua
ikilinganishwa na mwaka uliotangulia. Riba za amana za muda maalum zilipungua
kutoka wastani wa asilimia 9.30 hadi asilimia 8.78. Viwango vya riba za amana
za mwaka mmoja vilipungua kutoka wastani wa asilimia 11.16 mwaka 2015 hadi
asilimia 11.03 mwaka 2016. Vile vile, viwango vya riba za mikopo ya hadi mwaka
mmoja vilipungua kutoka wastani wa asilimia 14.22 kufikia asilimia 12.87 mwaka
2016. Mwenendo huu ulichangiwa na kuongezeka kwa ushindani wa kibenki. Kufuatia
hali hiyo, tofauti kati ya riba za amana na mikopo ya mwaka mmoja ilipungua
kufikia asilimia 1.83 mwaka 2016 ikilinganishwa na asilimia 3.06 mwaka 2015.
Hata hivyo, riba ya mikopo baina ya benki iliongezeka kufikia wastani wa
asilimia 13.49 mwezi Desemba 2016 kutoka asilimia 7.29 kwa muda kama huo mwaka
2015. Riba kwa dhamana za Serikali ilipungua kutoka asilimia 18.25 mwezi
Desemba 2015 kufikia wastani wa asilimia 15.12 mwezi Desemba 2016.
19. Mheshimiwa Spika, kufikia Machi 2017, riba za amana za muda maalum ziliongezeka kidogo kuwa
asilimia 10.89; na riba za amana za mwaka mmoja kufikia asilimia 12.03. Wakati
huo huo, riba za mikopo ya hadi mwaka mmoja ziliongezeka kufikia asilimia 18.07.
Ongezeko hili la riba za mikopo katika kipindi cha robo ya kwanza ya mwaka 2017
kunatokana na mabenki kuchukua tahadhari dhidi ya kuongezeka kwa makadirio ya
mikopo chechefu na kupunguza maoteo ya faida. Kuongezeka kwa riba za amana
kulichangiwa na kuongezeka kwa ushindani wa kibenki katika kuvutia amana. Kwa
upande mwingine, riba za mikopo baina ya benki zilipungua kufikia wastani wa
asilimia 8.16 na kwa dhamana za Serikali asilimia 14.52.
Amana katika Benki za Biashara
20. Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2016, amana katika benki za biashara ziliongezeka kwa asilimia
2.3 kufikia shilingi bilioni 19,729.5 kutoka shilingi bilioni 19,293.7 mwaka
2015. Kati ya amana hizo, sekta binafsi ilichangia asilimia 97.1 ikilinganishwa
na asilimia 95.6 mwaka 2015. Aidha, uwiano wa amana za fedha za kigeni katika
amana zote ulipungua kufikia asilimia 31.6 mwaka 2016 kutoka asilimia 32.8
mwaka 2015. Katika kipindi cha Januari hadi Machi 2017, amana katika benki za
biashara ziliongezeka kufikia shilingi bilioni 19,853.40, ambapo sekta binafsi ilichangia asilimia 96.4.
Mwenendo wa Mikopo kwa Sekta Binafsi
21. Mheshimiwa Spika, mikopo ya mabenki kwa sekta binafsi kwa mwaka 2016 iliongezeka kwa
asilimia 7.2 kufikia Shilingi bilioni 16,608.9 ikilinganishwa na Shilingi bilioni
15,492.7 mwaka 2015. Ukuaji huu ulikuwa chini ya kiwango cha mwaka 2015 cha
asilimia 24.8. Kiasi cha mikopo kilichotolewa kwa sekta binafsi mwaka 2016 kilifikia
asilimia 16.2 ya Pato la Taifa ikilinganishwa na asilimia 17.1 mwaka 2015. Kiwango
cha mikopo kilichotolewa kwa shughuli za uzalishaji; kilimo, uchukuzi na
mawasiliano, viwanda, huduma za kifedha, umeme, majengo na ujenzi, kilipungua mwaka
2016 ikilinganishwa na mwaka 2015. Wakati huo huo, mikopo ya shughuli za madini
na uchimbaji mawe, biashara, utalii, hoteli na migahawa na shughuli binafsi
iliimarika, japo kwa kasi ndogo. Mikopo iliyoelekezwa katika shughuli za
biashara, ilikuwa asilimia 21 ya mikopo yote na shughuli binafsi asilimia 18.6.
Mwenendo huu ulichangiwa, kwa kiasi kikubwa, na kupungua kwa ukwasi katika
mabenki kutokana na tahadhari zilizochukuliwa na mabenki kufuatia kuongezeka
kwa makisio ya viwango vya mikopo chechefu na kupungua kwa maoteo ya faida.
22. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Januari hadi Machi 2017, mikopo ya benki za biashara kwa
sekta binafsi iliendelea kuimarika, ikiongezeka kwa shilingi bilioni 77.4
kufikia shilingi bilioni 16,686.30. Hizi ni ishara njema za kuanza kuimarika
kwa uchumi na shughuli za sekta binafsi hususan, za uzalishaji viwandani, majengo
na mahoteli na mighahawa.
Ukuzaji Rasilimali
23. Mheshimiwa Spika, Tanzania ni mojawapo wa nchi chache za Afrika zilizojipambanua kwa kuwa na
utulivu wa uchumi jumla kwa muda mrefu sasa. Hii ikiwa ni pamoja na kuwa na
kasi kubwa ya ukuaji wa uchumi, mfumuko wa bei wa wastani na mwenendo wa
thamani ya shilingi umekuwa thabiti. Hali hii imekuwa kishawishi kikubwa cha mitaji
kutoka nje kuja nchini. Kwa mwaka 2016, ukuzaji rasilimali, kwa bei za miaka
husika, uliongezeka kwa asilimia 3.4 kutoka shilingi milioni 24,717,206 mwaka
2015 hadi Shilingi milioni 25,558,140. Hata hivyo, uwiano wa ukuzaji rasilimali
na Pato la Taifa, kwa bei za miaka husika, ulipungua kufikia asilimia 24.6
mwaka 2016 ikilinganishwa na asilimia 27.2 mwaka 2015. Kiwango cha ukuzaji
rasilimali kwa bei za mwaka 2007, kilipungua kwa asilimia 4.3 kutoka Shilingi milioni
13,733,585 mwaka 2015 kufikia Shilingi milioni 13,140,451 mwaka 2016.
Sekta ya Nje
24. Mheshimiwa Spika, Mwaka 2016, mwenendo wa biashara ya bidhaa na huduma kati ya Tanzania na
nchi mbalimbali uliendelea vizuri. Thamani ya mauzo ya bidhaa na huduma nje
iliongezeka kwa asilimia 4.1 kufikia dola za Marekani milioni 9,285.6 mwaka
2016 ikilinganishwa na Dola milioni 8,918.1 mwaka 2015. Aidha, uagizaji wa
bidhaa na huduma nje ilipungua kwa asilimia 14.0 kwa mwaka 2016 kutoka Dola milioni
12,528.2 mwaka 2015 kufikia dola za Marekani milioni 10,772.3. Mwenendo huo
ulitokana na kupungua kwa thamani ya bidhaa nyingi zilizoagizwa kutoka nje
isipokuwa kwa malighafi za viwandani zilizoongezeka ikichangiwa pia na kupungua
kwa gharama za usafirishaji, huduma zitolewazo na Serikali, na huduma nyingine za kibiashara.
25. Mheshimiwa Spika, Biashara kati ya Tanzania na nchi mbalimbali duniani ziliendelea kuimarika
na masoko kubadilika, ambapo kwa mwaka 2016 sehemu kubwa ya mauzo yote nje ya
nchi yalikwenda katika nchi za Uswisi (asilimia 16.2), India (asilimia 12.4),
Afrika ya kusini (asilimia 12.2), China (asilimia 6.2), Jamhuri ya Kidemokrasia
ya Kongo (asilimia 5.6) na Kenya (asilimia 5.5). Hii inaonesha kuwa kumekuwa na
mabadiliko kutoka masoko asilia, kama vile, Uingereza, Ujerumani na Canada. Bidhaa
zilizouzwa kwa wingi nchini Uswisi na India ni pamoja na dhahabu, mbegu za
mafuta, vito vya thamani na mbogamboga. Bidhaa zilizouzwa Kenya zilikuwa chai,
mahindi, vifaa vya ushonaji, mbogamboga na nafaka. Vile vile, bidhaa zilizouzwa
Afrika ya Kusini zilikuwa dhahabu, madini ya shaba na chai. Pamoja na maendeleo
haya, mauzo mengi nje ya nchi yaliendelea kuwa ya mazao ghafi yasiyoongezwa
thamani na hivyo kupata thamani ndogo.
26. Mheshimiwa Spika, kwa upande wa bidhaa zilizoagizwa kutoka nje, kiasi kikubwa kilitoka
katika nchi za China, India, Ufalme wa nchi za Kiarabu, Afrika ya Kusini,
Japani na Kenya, nchi ambazo kwa pamoja zilichangia asilimia 60.6 ya bidhaa
zote zilizoagizwa. Bidhaa zilizoagizwa kutoka China ni pamoja na mitambo na bidhaa
za marumaru, kwa Ufalme wa nchi za Kiarabu ni mafuta ya petroli na sukari na
kwa upande wa Japani na Afrika ya Kusini ni magari na bidhaa za chuma, kuonesha
kuwa uzalishaji nchini bado unategemea vipuri, malighafi na mitambo kutoka nje.
27. Mheshimiwa Spika, kufuatia mwenendo wa biashara kwa mwaka 2016, urari wa biashara ya bidhaa
na huduma ulikuwa na nakisi ya Dola za Marekani milioni 1,489.5, ikipungua kwa
asilimia 58.6 kutoka nakisi ya Dola za Marekani milioni 3,594.7 mwaka 2015. Hali
hii kwa kiasi kikubwa, ilichangiwa na kuongezeka kwa mapato ya mauzo ya bidhaa
na huduma nje ya nchi na kupungua kwa uagizaji wa bidhaa kutoka nje ya nchi. Hivyo,
urari wa malipo yote, kwa mwaka 2016, ukijumuisha urari wa biashara ya bidhaa
na huduma, mapato ya vitega uchumi, uhamisho wa mali, malipo ya kawaida,
uhamisho wa mitaji na malipo ya fedha katika uwekezaji, ulikuwa na ziada ya
dola za Marekani milioni 305.5
ikilinganishwa na nakisi ya dola za Marekani
milioni 199.1 mwaka 2015. Katika kipindi cha Januari hadi Machi mwaka
2017, thamani ya mauzo ya bidhaa na huduma nje ilifikia Dola za Marekani
milioni 2,224.8, ikichangiwa, kwa kiasi kikubwa, na mauzo ya bidhaa asilia na
zisizo asilia hasa huduma za utalii, dhahabu, bidhaa za mboga mboga na matunda.
Aidha, katika kipindi hicho, uagizaji wa bidhaa na huduma kutoka nje ulikuwa Dola
za Marekani milioni 2,203.6 na hivyo kuendelea kuwa na ziada katika urari wa
akaunti ya biashara ya bidhaa na huduma.
Akiba ya Fedha za Kigeni na Thamani ya Shilingi
28. Mheshimiwa Spika, hadi kufikia mwezi Desemba 2016, akiba ya fedha za kigeni ilifikia Dola za
Marekani milioni 4,325.6 ikilinganishwa na Dola milioni 4,093.7 Desemba 2015.
Kiasi hicho kilikuwa kinaweza kulipia gharama za kununua bidhaa na huduma kutoka
nje kwa miezi 4.2. Kufikia Machi 2017, akiba ya fedha za kigeni ilifikia Dola
za Kimarekani milioni 4,482.6, kiasi kinachotosheleza uagizaji wa bidhaa na
huduma kutoka nje kwa miezi 4.3. Kuongezeka kwa akiba ya fedha za kigeni
kumesaidia kurejesha utengamavu wa thamani ya shilingi. Katika kipindi cha mwaka
2016, mwenendo wa thamani ya shilingi ya
Tanzania dhidi ya dola ya Marekani ulikuwa wa kuridhisha ukipungua kwa asilimia
8.8 tu ambapo dola moja ya Marekani ilinunuliwa kwa wastani wa Shilingi 2,177.07
ikilinganishwa na shilingi 1,991.4 mwaka 2015.. Hadi kufikia Machi 2017, dola moja
ya Marekani ilinunuliwa kwa wastani wa shilingi 2,223.9 kutoka Shilingi 2,172.6
ilivyokuwa ikinunuliwa mwishoni mwa mwaka 2016.
Mabadiliko ya Maisha ya Watu
29. Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2012, Tanzania ina wastani
wa ongezeko la watu la asilimia 2.7 kwa mwaka, ambapo kufikia mwaka 2016
ilikadiriwa kuwa na watu 48,676,698. Kwa makadirio haya, Tanzania inakuwa ni nchi
ya tano kwa idadi ya watu Barani Afrika, ikitanguliwa na nchi nne (4) ambazo ni
Nigeria, Ethiopia, Misri na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo. Idadi kubwa ya
watu na kasi ya ongezeko imekuwa ni changamoto kubwa katika harakati za
kupunguza umaskini na kuimarisha utoaji wa huduma. Kwa kuzingatia hali hii,
Serikali imeendelea kuongeza na kuboresha upatikanaji wa elimu msingi hususan kwa
wasichana. Kwa upande mwingine, idadi kubwa ya watu ni fursa pia kwa maana ya
soko la bidhaa na huduma, ikiwa itaendana na maendeleo ya stadi, teknolojia,
ujasiriamali na pato la kila mwananchi.
30. Mheshimiwa Spika, licha ya hatua hizi, bado kumekuwa na changamoto nyingine kufuatia kasi
kubwa ya uhamiaji mijini, ambapo kwa sasa, takribani asilimia 30 ya watu nchini
wanaishi mijini. Kasi hii ya mabadiliko ya idadi ya watu na uhamiaji mijini inadunisha
kasi ya kuboresha upatikanaji wa nyumba
na makazi yaliyopangwa na pia utoaji wa
huduma zinazoendana na idadi ya wakazi wa mijini. Katika kukabiliana na
changamoto hizi, Serikali imeendelea kuimarisha upimaji wa maeneo ya makazi,
ujenzi wa nyumba za gharama nafuu na kuchukuwa hatua zinazolenga kuinua tija na
faida katika shughuli za kilimo. Hatua hizo ni pamoja na kuimarisha upatikanaji
wa huduma za ugani, pembejeo, zana za kilimo, masoko, miundombinu ya
umwagiliaji, na kuondoa utitiri wa kodi katika shughuli za kilimo. Hatua pia
zimeendelea kuchukuliwa kwa lengo la kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji na
uendeshaji wa shughuli za viwanda na biashara hasa vijijini. Lengo ni kupanua
fursa za ajira mbadala kwa wakazi wa vijijini, ikiwa ndiyo njia ya kuaminika
zaidi katika kudhibiti kasi ya watu kuhamia mijini. Huduma za mafunzo ya ufundi
stadi zimezidi kuimarishwa ili wale wanaohamia mijini waweze kuajirika na
kujiajiri kwa urahisi.
31. Mheshimiwa Spika, kwa upande wa ustawi wa jamii,
maisha ya watu yameendelea kuboreka kama inavyothibitishwa na taarifa ya Umoja
wa Mataifa ya Maendeleo ya Watu kwa mwaka 2016, ambapo kwa kigezo cha fahirisi
ya maendeleo ya watu (HDI) ustawi wa watanzania umeendelea kuimarika kutoka
alama 0.521 mwaka 2014 hadi alama 0.531 mwaka 2015. Kigezo hiki huzingatia
viashiria kadhaa vya maendeleo na ustawi, hususan, muda wa kuishi baada ya
kuzaliwa, elimu, na wastani wa kipato cha mwananchi. Kwa kutumia kigezo hiki
Tanzania ni nchi ya pili kwa ustawi wa maisha ya wananchi katika Ukanda wa
Afrika Mashariki baada ya Kenya iliyofikia alama 0.555 katika kipindi hiki.
32. Mheshimiwa Spika, mafanikio ya Tanzania ni matokeo ya jitihada zinazochukuliwa na Serikali
katika kuboresha upatikanaji wa huduma za jamii kama vile elimu, afya, maji
safi na salama, na umeme katika maeneo ya vijijini na mijini.
Mfano, idadi ya wananchi waliofikiwa na huduma ya umeme hadi Machi 2017
ilifikia asilimia 67.5 ikilinganishwa na asilimia 40 iliyokuwa imefikiwa
Aprili, 2016. Kwa maeneo ya mijini, idadi ya wananchi waliopata umeme ilifikia
asilimia 97.3 Machi 2017 ikilinganishwa na asilimia 63.4 mwaka 2014/15, na
upande wa maeneo ya vijijini ilifikia asilimia 49.5 Machi 2017 ikilinganishwa
na asilimia 21.0 mwaka 2014/15. Kwa upande wa upatikanaji wa maji, idadi
iliongezeka kutoka watu 21,900,000 Juni 2016 hadi 22,951,371 Machi 2017.
Kumekuwa na mafanikio pia kwa upande wa elimu, ambapo uandikishaji wa wanafunzi
wa darasa la kwanza uliongezeka kutoka milioni 1.5 mwaka 2014 hadi milioni 2.1
mwaka 2016. Vile vile, idadi ya wananchi wanaonufaika na huduma ya Mfuko wa
Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) imeongezeka kutoka 3,377,023 mwaka 2015/16 hadi
3,880,088 Machi 2017. Wanufaika wa Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF) wameongezeka
kutoka 8,717,130 mwaka 2015/16 hadi kufikia wanufaika 9,573,906 Machi 2017.
33. Mheshimiwa Spika, pamoja na kupunguza umasikini wa mahitaji ya msingi, ni dhamira ya
Serikali kuhakikisha kuwa idadi ya Watanzania wanaokosa mlo kwa siku au kuishi
kwa mlo mmoja inapungua kutoka kiwango cha asilimia 9.7 kwa sasa kufikia
asilimia 5.7 na 4.4 ifikapo mwaka 2020 na 2025, kwa mtiririko huo. Hatua
zinazochukuliwa kufikia lengo hili ni pamoja na kuimarisha uzalishaji na hivyo upatikanaji
wa chakula katika kaya; kuongeza fursa za ajira mijini na vijijini; kuendelea
na mpango wa kusaidia kaya masikini; na kuwezesha upatikanaji wa mikopo nafuu
kwa wajasiriamali kupitia mifuko ya maendeleo ya vijana, wanawake na wajasiriamali
wadogo.
34. Mheshimiwa Spika, licha ya mafanikio yaliyofikiwa, kiwango cha umaskini kwa maeneo ya
vijijini bado ni kikubwa ikilinganishwa na maeneo ya mijini. Umaskini vijijini
umepungua kutoka asilimia 39.4 mwaka 2007 hadi asilimia 33.3 mwaka 2012 ikimaanisha
kuwa japo vijijini umaskini unapungua lakini bado ni chini ya wastani wa
kitaifa. Mantiki yake ni kuwa kasi kubwa ya ukuaji wa uchumi haijaligusa kundi
kubwa la wananchi wa vijijini, ambao wengi wao hutegemea shughuli za kilimo,
ufugaji na uvuvi. Sekta hizi, ambazo ndizo msingi wa ustawi wa maisha ya watu
wa vijijini, zimekuwa na tija na kasi ndogo ya ukuaji kwa kipindi chote.
Shabaha ya Serikali ni kupunguza wastani wa umaskini vijijini kutoka kiwango
cha sasa cha asilimia 33.3 hadi kufikia asilimia 19.7 na 15 mwaka 2020 na mwaka
2025, kwa mtiririko huo.
35. Mheshimiwa Spika, kipimo cha mgawanyo wa kipato miongoni mwa wananchi (Gini coefficient)
kwa upande wa Tanzania Bara kinaonesha kuwa tofauti ya kipato imepungua kutoka
0.37 mwaka 2006/7 hadi 0.34 mwaka 2011/12. Hata hivyo, tofauti ya kipato kati
ya jiji la Dar es Salaam na maeneo ya miji mingine na ile ya maeneo ya vijijini
ni kubwa zaidi. Hali hii imechangiwa na tofauti ya upatikanaji wa huduma,
miundombinu, fursa za ajira, athari za mazingira na mabadiliko ya tabia nchi
katika shughuli msingi za jamii husika.
36. Mheshimiwa Spika, Kwa mujibu wa Utafiti wa Afya ya Uzazi na Mtoto na Viashiria vya Malaria
Tanzania 2015/16, vifo vya watoto wachanga chini ya mwaka mmoja vimepungua
kutoka 51 kwa vizazi hai 1,000 mwaka 2010 hadi 43 kwa vizazi hai 1,000 mwaka
2015/16, vifo vya watoto chini ya miaka mitano vimepungua kutoka 81 kwa vizazi
hai 1,000 mwaka 2010 hadi vifo 67 kwa vizazi hai 1,000 mwaka 2015/16. Kushuka
kwa viashiria hivi kunatokana na kuimarika kwa upatikanaji wa huduma za msingi
za kijamii ikiwemo afya ya uzazi na mama na mtoto nchini.
37. Mheshimiwa Spika, maelezo ya kina kuhusu hali ya uchumi yapo katika kitabu cha Hali ya
Uchumi kwa mwaka 2016.
UTEKELEZAJI WA MPANGO WA MAENDELEO WA TAIFA WA
MWAKA 2016/17
Utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo 2016/17
38. Mheshimiwa Spika, mwaka 2016/17 ulikuwa mwaka wa kwanza wa utekelezaji wa Mpango wa Pili wa
Maendeleo wa Miaka Mitano. Mpango huu utatekelezwa hadi 2020/21, ambapo msukumo
ni kuchochea mageuzi ya uchumi kupitia ujenzi wa uchumi wa viwanda na
kufungamanisha maendeleo ya uchumi na maendeleo ya watu. Kwa kuzingatia hili,
Mpango wa Maendeleo wa mwaka 2016/17 ulijielekeza katika maeneo makuu manne ya
kipaumbele, ikiwa ni:-
(i) Kukuza uchumi na ujenzi wa msingi wa uchumi wa viwanda;
(ii) Kufungamanisha uchumi na maendeleo ya watu;
(iii)
Kujenga mazingira
wezeshi kwa uendeshaji biashara na uwekezaji; na
(iv)
Kuimarisha usimamizi wa
utekelezaji wa Mpango.
39. Mheshimiwa Spika, mapitio ya utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo wa 2016/17 yamefafanuliwa kwa
kina katika hotuba za mipango na bajeti za Mawaziri wa sekta husika. Kwa maana
hiyo nitajikita kuelezea hatua zilizofikiwa katika utekelezaji wa baadhi tu ya
miradi ya maendeleo kwa mwaka 2016/17.
Miradi Iliyopewa Msukumo wa Kipekee:
40.
Mheshimiwa Spika, Hii ni miongoni mwa miradi ya kimkakati iliyobainishwa kwa utekelezaji
katika Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano, 2016/17 – 2020/21. Utekelezaji
wa miradi hiyo ni kama ifuatavyo:
(i)
Ujenzi wa Reli ya Kati: kusainiwa kwa mkataba
wa kusanifu na kujenga awamu ya kwanza ya mradi kutoka Dar es Salaam – Morogoro
(Km 205) ambapo mkandarasi ameanza maandalizi ya ujenzi ikiwemo ujenzi wa
kambi, ofisi pamoja na kiwanda cha kukarabati mataruma. Mkandarasi amelipwa Shilingi
bilioni 300 malipo ya awali (advance payment) na Mheshimiwa Rais alizindua kazi
ya ujenzi tarehe 12 Aprili 2017. Taratibu zinazoendelea ni kupata fedha na
kuendelea na ujenzi sehemu za reli zilizobakia. Kwa sehemu ya Morogoro hadi
Makutupora (Km 336), Serikali inaendelea na mazungumzo na Mkandarasi
aliyepatikana; na kwa sehemu za Makutupora hadi Tabora (Km 294), Tabora hadi
Isaka (Km 133) na Isaka hadi Mwanza (Km 249), Serikali ipo kwenye mazungumzo na
baadhi ya mabenki ambayo yameonesha nia ya kutoa mkopo nafuu wa benki kwa ajili
ya ujenzi.
(ii)
Kuboresha Shirika la Ndege Tanzania: Ndege mbili (2) zenye uwezo wa kubeba abiria 76 kila moja zilinunuliwa na
zilianza kutoa huduma tangu Oktoba 2016. Vile vile, maandalizi ya ununuzi wa
ndege nyingine 4 yamekamilika na mikataba imesainiwa, ambapo malipo ya awali ya
kiasi cha Dola za Marekani milioni 56.89 tayari yamefanyika. Kati ya ndege
hizo, moja inategemewa kuwasili Julai 2017; mbili zinategemewa kuwasili Juni
2018, na ya mwisho, ambayo itakuwa ya masafa marefu yenye uwezo wa kubeba
abiria 262 inategemewa kuwasili Julai 2018.
(iii) Makaa ya Mawe Mchuchuma na Chuma Liganga: maandalizi yote ya ujenzi wa miradi hii yamekamilika,
ikiwa ni pamoja na kutenga fedha kwa ajili ya malipo ya fidia kwa wananchi
watakaopisha mradi. Vile vile, kampuni ya Sichuan
Hongda (Group) Corporation Ltd, ambayo ndio mbia katika miradi hii,
wametenga jumla ya Dola za Kimarekani milioni 300 kwa ajili ya kulipia sehemu
ya mtaji (equity) wao katika miradi.
Mfumo uliokubalika na pande zote mbili ni mwekezaji kujenga mtambo wa kufua
umeme, kumiliki na kuuendesha (Build Own and Operate, BOO). Mauziano ya umeme
kwa TANESCO hayatajumuisha gharama za uwekezaji.
(iv) Mradi wa Bomba la Mafuta kutoka Hoima Uganda – Bandari ya Tanga
Hatua iliyofikiwa ni pamoja na:
kusainiwa kwa mkataba wa makubaliano
ya awali; kutolewa kwa vivutio vya kodi; kusainiwa kwa Inter- Govermental Agreement; kufanyika kwa tathmini ya njia ya
bomba; kufanyika kwa tathmini ya
mahitaji ya njia ya bomba; kufanyika tathmini ya masuala ya kijamii na
mazingira; kufanyika kwa upembuzi yakinifu kwa ajili ya ujenzi wa gati ya kupokelea
mafuta – Chongoleani katika bandari ya Tanga; na kutangazwa kwa zabuni za
kuwapata wataalam elekezi kwa ajili ya uchunguzi wa udongo.
(v)
Ununuzi na Ukarabati wa Meli kwenye Maziwa Makuu: Hatua iliyofikiwa ni kuendelea na taratibu za
ununuzi kwa ajili ya ujenzi wa meli mpya kwa ajili ya usafirishaji wa abiria na
mizigo katika ziwa Victoria na ukarabati mkubwa wa Mv. Victoria na Mv. Butiama.
Kwa upande wa Mv. Liemba katika ziwa Tanganyika, mjenzi amepatikana ambaye ni
M/S LEDA SHIPYARD. Ujenzi wa meli mbili za mizigo ziwa Nyasa umekamilika.
(vi)
Uanzishwaji wa Shamba la Miwa na Kiwanda cha Sukari Mkulazi: Shilingi Billioni 2 tayari zimewekezwa katika mradi huu. Kazi zilizofanyika
ni: kupima ubora wa udongo; vitalu vya mbegu za miwa vimeandaliwa; na taratibu
za kupata huduma ya wataalam wa kufanya upembuzi yakinifu, uchunguzi wa mbegu
za miwa, tathmini ya athari za mazingira na ujenzi wa barabara za kuingia
katika eneo la mradi zinaendelea.
(vii) Ujenzi wa Mitambo ya Kusindika Gesi Kimiminika: Hatua iliyofikiwa ni pamoja na: kupatikana kwa eneo la mradi Likong’o
mkoani Lindi; kuundwa kwa timu ya majadiliano na kuandaliwa kwa hadidu za
rejea, kupitia nyaraka muhimu zinazohusu mradi (sera, sheria, mikataba, kanuni
na mikakati ya Serikali); na kuanza kwa majadiliano na kampuni zinazoshiriki
katika mradi juu ya masuala yatakayozingatiwa katika kuandaa mkataba kati ya
kampuni husika na Serikali (Host Government Agreement – HGA).
(viii)
Uendelezaji wa Maeneo Maalum ya Kiuchumi
a. Kituo cha Biashara cha Kurasini: kiasi cha fidia kilicholipwa kwa ajili ya kupata eneo la mradi ni Shilingi
bilioni 101.04 na wananchi 1,019 tayari wamelipwa fidia. Eneo hili kwa sasa lipo
chini ya umiliki wa Serikali kwa asilimia 100 na hivyo maandalizi ya mpango
mahsusi wa uwekezaji katika eneo hilo yanaendelea.
b. Eneo Maalum la Uwekezaji la Bagamoyo: Shilingi bilioni 26.66 zimetumika
kulipa fidia kwa wananchi 1,155 kati ya 2,273 wanaopaswa kupisha mradi
kwenye eneo la hekta 2,339.6.
c. Eneo Maalum la Uwekezaji la Mtwara: Tayari eneo la hekta 10 kati ya hekta 110 za eneo lililotengwa kwa ajili
ya Mtwara SEZ limetangazwa kwa ajili ya matumizi ya bandari huru (Freeport
Zone) na maandalizi ya kuweka miundombinu, hususan barabara, kwa eneo hilo
yanaendelea.
Kujenga
Msingi wa Uchumi wa Viwanda
41. Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza azma
ya kujenga uchumi wa viwanda, mwelekeo umeanza kuwa vizuri. Miradi ya viwanda mbalimbali imeanzishwa kutokana na mchango wa
sekta binafsi katika mikoa mbalimbali nchini, kwa mfano kwa mkoa wa Pwani una
jumla ya miradi mipya ya viwanda 82. Aidha, baadhi ya miradi mikubwa ya viwanda
iliyozinduliwa na kuwekwa mawe ya msingi kwa mkoa wa Pwani pekee ni pamoja na:-
viwanda viwili vya Tywford Tiles (Chalinze) na Goodwill Ceramic (Mkuranga) vya
kutengeza marumaru (tiles); kiwanda cha nondo cha Kiluwa Steel Industries Ltd
(Mlandizi Pwani) ambacho kimeanza uzalishaji; kiwanda cha Global Packaging (Mailimoja Pwani) ambacho kinafanya kazi; kiwanda
cha kutengeneza juisi ya matunda cha Bakhresa Food
Product Ltd (Mkuranga) ambacho kimezinduliwa na kinafanya kazi; kiwanda cha
Elyven Agric Co. Ltd (Bagamoyo); kiwanda cha Juisi cha Sayona Fruits Ltd (Mboga
Pwani); na kiwanda cha KEDS Tanzania Co. Ltd (Kibaha Pwani).
42. Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa na mchango mkubwa kuwezesha sekta binafsi kuwekeza
katika viwanda hivi, ikiwa ni pamoja na kusaidia upatikanaji wa ardhi, kuweka
miundombinu inayohitajika, na kutoa vibali vya ujenzi na pia vivutio.
Halmashauri na Serikali za Mitaa katika maeneo haya zimekuwa na msaada na
ushirikiano mkubwa kwa wawekezaji ikiwemo kutoa maeneo ya viwanda ili
kuhamasisha uwekezaji. Mathalan, Maswa wameanzisha kiwanda cha kuzalisha Chaki
cha Maswa Youth Enterprises Ltd kwa utaratibu huo. Nitumie fursa hii kuwapongeza kwa dhati viongozi wa mikoa,
wilaya, halmashauri na Serikali za Mitaa walioitikia kwa dhati wito wa Serikali
kujielekeza katika kuvutia na kuwezesha uwekezaji. Niwatake pia viongozi wa
Halmashauri zote nchini kuiga mfano wa wenzao wanaofanya jitihada zote katika
kuhakikisha kuwa Halmashauri zinaandaa mazingira mazuri na maeneo ya uwekezaji kwa
ajili ya sekta binafsi.
43. Mheshimiwa Spika, Serikali pia kupitia mashirika yake mbalimbali imeanza kuwekeza katika
ujenzi wa viwanda, mwitiko wa pekee na wa kupongezwa ni wa Mifuko ya Hifadhi ya
Jamii, ambapo PPF na NSSF wanashirikiana kuwekeza katika kilimo cha miwa na
uzalishaji wa sukari katika eneo la Mkulazi na Mbigiri (Morogoro); na LAPF
wanajenga machinjio ya kisasa ya nyama (kwa Makunganya – Morogoro). Shirika la
Taifa la Maendeleo (NDC) linashirikiana na sekta binafsi kwa ajili ya uwekezaji
katika eneo la viwanda la TAMCO – Kibaha kwa uendelezaji wa viwanda vya nguo na
uunganishaji wa magari na matrekta, ambapo kiwanda cha kuunganisha matrekta
kimefikia hatua ya kuanza majaribio. Hatua nyingine zinazoendelea chini ya NDC
ni pamoja na jitihada za kufufua Kiwanda cha General Tyre (Arusha); hatua za
awali za uwekezaji katika mradi wa uchenjuaji wa Magadi Soda (Bonde la
Engaruka). NDC pia kwa ubia na kampuni ya TCIMRL ya China imewekeza katika
miradi ya Mchuchuma na Liganga.
Ujenzi wa Miundombinu na Mazingira Wezeshi
44. Mheshimiwa Spika, ujenzi wa uchumi wa viwanda unahitaji miundombinu ya uhakika. Hivyo,
Serikali imeendelea na utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kuimarisha na
kuboresha miundombinu na huduma za uchumi wa viwanda. Miongoni mwa miradi hii
ni: ujenzi wa mtambo wa kufua umeme wa Kinyerezi II (MW 240); upanuzi wa mtambo
wa kufua umeme wa Kinyerezi I (MW 185); ujenzi wa njia ya umeme ya msongo wa kV
400 Iringa – Singida - Shinyanga (km 670), kV 220 Makambako – Songea (km 250),
na North West Grid kV 400 (Mbeya –
Sumbawanga – Mpanda - Kigoma – Nyakanazi km 1,148); usambazaji umeme Vijijini na Makao Mkuu ya Wilaya (REA
Turnkey Phase III), ambapo wateja 146,831 sawa na asilimia 58.7 ya lengo
wameunganishwa; na ukarabati wa njia ya reli ya kati. Kwa upande wa barabara
hatua iliyofikiwa ni kukamilika kwa ujenzi wa barabara za Masasi – Songea –
Mbambabay, sehemu ya Namtumbo – Tunduru (km 193), na Tunduru – Mangaka –
Mtambaswala (km 202.5); barabara ya Dodoma – Babati (km 261); Bagamoyo – Msata
na daraja la Ruvu chini; na kukamilika kwa Daraja la Kilombero katika barabara
ya Ifakara – Mahenge. Ujenzi wa barabara ya Kidahwe – Kasulu – Kibondo –
Nyakanazi unaendelea na umefikia asilimia 16.4; na ujenzi wa barabara za juu za
TAZARA na Interchange ya Ubungo
umeanza.
Kufungamanisha Ukuaji wa Uchumi na Maendeleo ya Watu
45. Mheshimiwa Spika, Kwa upande wa kufungamanisha ukuaji wa uchumi na
maendeleo ya watu Serikali inaendelea kutekeleza sera ya elimumsingi bila
malipo; uboreshaji wa miundombinu na huduma za kujifunzia na kufundishia;
kukamilika kwa ujenzi wa mabweni katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam;
kutoa mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu; kukamilika kwa ujenzi wa Hospitali ya Taaluma na Tiba ya Chuo
Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili, Kampasi ya Mloganzila; na kukamilika kwa ukarabati wa vyuo vya ualimu kumi. Katika kuimarisha ujuzi na stadi za kazi, Serikali
imekamilisha matayarisho ya Sera ya Taifa ya Ajira ya mwaka 2017, Miongozo ya
Mafunzo Kazini kwa vitendo kwa wanafunzi (Apprenticeship Framework) na mafunzo
kwa vitendo kwa wahitimu (Internship Framework). Vile vile, Serikali imeingia
mikataba na viwanda vya TOOKU Garment na Mazava Fabrics kwa ajili ya kutoa
mafunzo ya stadi za ubunifu na ushonaji wa nguo viwandani. Maeneo mengine yaliyozingatiwa ni pamoja na
kupanua miundombinu ya upatikanaji wa maji safi na salama mijini na vijijini;
huduma za afya na upimaji wa maeneo ya makazi.
46. Mheshimiwa Spika, maeneo mengine yaliyoendelea kutekelezwa ni yale yaliyotoa fursa za ajira
na ushiriki wa wananchi wengi katika shughuli za uchumi wa viwanda, ikiwa ni
pamoja na: kuandaliwa kwa program ya muda mrefu na mfupi ya upimaji na
umilikishaji wa ardhi hususan kwa matumizi ya kilimo; kukamilika kwa ukarabati
wa maghala 106 katika Halmashauri za Wilaya za Iringa, Mufindi, Mbeya, Songea,
Kalambo, Mbozi, Momba na Njombe; na kuingizwa nchini kwa tani 231,140 za
mbolea.
47. Mheshimiwa Spika, katika kuhamishia Shughuli za
Serikali Kuu Dodoma: awamu ya kwanza imekamilika ambapo majengo ya ofisi za wizara katika
kipindi cha mpito na nyumba za makazi kwa baadhi ya viongozi zimepatikana. TBA
na Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma wanaendelea na kukamilisha ukarabati wa
nyumba za makazi na ofisi. Vile vile, Serikali kwa kupitia Halmashauri ya
Manispaa ya Dodoma inaendelea na upimaji wa viwanja vya makazi na ofisi, ambapo
watumishi wa Umma wameandaliwa mkakati maalum utakaosaidia upatikanaji wa
viwanja kwa ajili ya makazi. Aidha, Shirika la Nyumba la Taifa linaendelea na
ujenzi wa nyumba mpya 300 za makazi na zinazotarajiwa kukamilika Septemba,
2017. Kwa upande mwingine, Serikali inaendelea na mazungumzo na kampuni binafsi
kutoka Switzerland, China na Zimbabwe na pia ya ndani ambayo yameonesha nia ya
kushiriki katika ujenzi wa miundombinu ya maji kwa mji mpya wa Dodoma. Taasisi
za Serikali kama vile TBA, TANESCO, SUMATRA, TEMESA, TANROADS, TTCL na Halmashauri
ya Manispaa ya Dodoma zimekamilisha maandalizi ya awali ya kuboresha
miundombinu muhimu inayohitajika kuwezesha uendeshaji wa Serikali bila vikwazo
katika kipindi hiki.
Utekelezaji wa Bajeti ya Maendeleo
48. Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2016/17 Serikali ilipanga kutumia Shilingi bilioni 11,820.503 kwa
ajili ya bajeti ya maendeleo, ambapo, Shilingi bilioni 8,702.697 zilikuwa za
ndani na bilioni 3,117.805 za nje. Hadi Aprili 2017, fedha zilizokuwa
zimetolewa ni Shilingi bilioni 4,516.7, sawa na asilimia 38 ya bajeti ya
maendeleo, ikijumuisha fedha zilizotolewa kwa Halmashauri. Fedha za maendeleo
zilizotolewa zinajumuisha Shilingi bilioni 3,608.9 fedha za ndani na Shilingi bilioni
907.8 fedha za nje. Kwa ujumla kiasi cha fedha kilichotolewa ni chini ya maoteo
ya mtiririko wa fedha kwa wakati husika. hii ilichangiwa na sababu mbalimbali,
ikiwa ni pamoja na kuchelewa kupatikana kwa misaada na mikopo ya kibiashara
kufuatia majadiliano na Washirika wa Maendeleo na mabenki kuchukua muda mrefu,
kupanda kwa riba ya mikopo ya kibiashara katika soko la fedha kimataifa hivyo
Serikali kufikia maamuzi ya kuahirisha kuchukua mikopo husika. Hata hivyo,
miradi ambayo ina vyanzo vya fedha mahsusi kama vile Wakala wa Nishati Vijijini
(REA), Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA), Mfuko wa Barabara, Bodi ya Mikopo ya
Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB), Mfuko wa Maji na Mfuko wa Reli ilipatiwa
fedha zote zilizokusanywa katika kipindi husika.
49. Mheshimiwa Spika, Mikakati mbalimbali imewekwa kuhakikisha fedha zilizopangwa kwa ajili ya
matumizi ya miradi ya maendeleo zinapatikana kwa kiasi cha kuridhisha. Miongoni
mwa mikakati hiyo ni pamoja na kuendelea na majadiliano baina ya Serikali na
Washirika wa Maendeleo ili kuhakikisha fedha za misaada na mikopo nafuu
zinapatikana kama zilivyoahidiwa; kuimarisha makusanyo ya ndani ya Serikali; na
kuendelea kuboresha mazingira ya uendeshaji biashara ili kuvutia uwekezaji wa
sekta binafsi nchini. Aidha, Serikali ipo katika hatua za mwisho za majadiliano
na benki ya Credit Suisse ili kupata mkopo wa Dola za Marekani Milioni 500 kwa
ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo.
Changamoto za Utekelezaji wa Mpango na Bajeti ya 2016/17
50. Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa Mpango na Bajeti ya
mwaka 2016/17 umekabiliwa na changamoto kadhaa ikiwa ni pamoja na mwenendo wa upatikanaji wa fedha, upatikanaji wa maeneo ya
uwekezaji na matayarisho hafifu ya miradi ambapo kwa baadhi ilionekana bayana
kuwa ama ipitiwe upya au majadiliano yaanze upya ili kulinda maslahi ya Taifa.
(i) Mwenendo wa Upatikanaji
wa Fedha: Kwa upande wa upatikanaji wa fedha kutoka makusanyo ya
mapato ya ndani, haya yamekuwa yakiongezeka na yamekuwa yakipatikana kwa
wakati. Kumekuwepo na kuchelewa kupatikana kwa mikopo yenye masharti nafuu na
ya kibiashara kutoka nje; na Majadiliano kuchukua muda mrefu hivyo kuchelewa
kupatikana kwa fedha za kuelekeza baadhi ya miradi ya maendeleo.
Kumekuwa na kuchelewa
kwa ukamilishaji wa taratibu za kufikia maafikiano na wakopeshaji, hivyo,
mikopo kuchelewa kupatikana. Katika mwaka 2016/17, kwa makusudi kabisa,
ilionekana ipo haja ya kusitisha mchakato wa kukopa baada ya riba za mabenki
duniani kupanda sana kufikia wastani wa asilimia 9 kutoka asilimia 6.
Zipo hatua mbalimbali zilizochukuliwa kukabiliana na changamoto hii. Pamoja
na kuzidi kuimarisha makusanyo ya ndani ya Serikali, msisitizo ni kuhakikisha kuwa fedha zinazopatikana
zinaelekezwa kwenye miradi yenye tija; kuendelea kuboresha mazingira ya
uendeshaji biashara ili kuvutia uwekezaji wa sekta binafsi nchini, ikiwa ni
pamoja na wawekezaji wadogo hususan upatikanaji wa mikopo nafuu na maeneo ya
uwekezaji na pia kuhuisha sheria, kanuni, taratibu na kupunguza ada, kodi na tozo za uwekezaji na
uendeshaji biashara. Aidha, Serikali inaendelea na majadiliano na baadhi ya
taasisi za fedha na mabenki ili kupata mkopo kwa ajili ya utekelezaji wa miradi
ya maendeleo.
(ii) Upatikanaji wa Maeneo
ya Uwekezaji: Baadhi ya miradi imekuwa na
utekelezaji hafifu kutokana na kuwepo migogoro ya ardhi na kutokamilika kwa
hatua za kulipa fidia. Uhakiki umeonesha kuwepo kwa udanganyifu katika gharama
na watu wanaostahili kulipwa fidia katika maeneo mengine. Hali hii ililazimisha
madai kupitiwa upya na hivyo kuchelewa
kuanza kwa utekelezaji. Hatua zilizochukuliwa na Serikali ni kuongeza kasi ya
kupata Maeneo Maalum ya Uwekezaji (EPZ na SEZ) na maeneo ya viwanda kwa ngazi
zote za mikoa. Halmashauri zote zimeagizwa na tayari baadhi zimetenga maeneo ya
viwanda na biashara ndogo ndogo. Vile vile, mashirika ya umma yenye ardhi kama
vile NDC yametumia maeneo hayo kuingia ubia na wawekezaji binafsi.
(iii) Mapungufu katika
Maandalizi ya Miradi: Serikali katika hatua
za kuimarisha maandalizi ya miradi, ambapo imeandaa na kuweka utaratibu wa
maofisa kutumia kikamilifu Mwongozo wa Usimamizi wa Uwekezaji wa Umma. Pamoja
na kuandaa Mwongozo huo, Serikali imechukua hatua ya kutoa mafunzo kwa wataalam
422 wanaohusika na uratibu wa miradi ya maendeleo kwa Mikoa na Halmashauri zote
pamoja na Wizara, Taasisi, Idara Zinazojitegemea na Wakala wa Serikali.
51. Mheshimiwa Spika, maelezo ya kina kuhusu Utekelezaji
wa Miradi ya Maendeleo yapo katika kitabu cha Mpango (Sura ya Tatu).
MPANGO WA MAENDELEO WA MWAKA 2017/18
Mazingira Yanayoongoza Mpango
52. Mheshimiwa Spika, Mpango wa Maendeleo wa Taifa 2017/18 ni wa pili katika utekelezaji wa
Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano (2016/17 – 2020/21). Msukumo wake
ni kufanikisha utekelezaji wa malengo ya Mpango wa Miaka mitano hasa kwa miradi
ambayo utekelezaji wake unaendelea tokea 2016/17.
53. Mheshimiwa Spika, utayarishaji wa Mpango wa Maendeleo wa Taifa 2017/18 umezingatia yafuatayo
kama mwongozo: Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025; Mpango wa Pili wa Maendeleo wa
Taifa wa Miaka Mitano (2016/17 - 2020/21); sera na mikakati mbalimbali ya kisekta,
kikanda (EAC na SADC) na Umoja wa Afrika; Agenda ya 2030 ya Malengo ya
Maendeleo Endelevu; Agenda ya 2063 ya Maendeleo ya Afrika; na Ilani ya CCM ya
Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015. Vile vile, umezingatia mwenendo wa uchumi wa Taifa,
kikanda na kidunia kwa mwaka 2016 na maoteo kwa mwaka 2017. Umezingatia pia
hali halisi ya utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2016/17 na
changamoto za utekelezaji zilizojitokeza.
Ushirikishwaji wa Jamii katika Maandalizi ya Mpango
54. Mheshimiwa Spika, mchakato wa maandalizi ya Mpango huu umezingatia dhana ya ushirikishi
mpana wa wadau ikiwa ni pamoja na Wizara, Idara Zinazojitegemea, Wakala wa
Serikali, Taasisi za Serikali, Taasisi za Utafiti na Elimu ya Juu, Sekta
Binafsi na Washirika wa Maendeleo. Pia uliweza kupata maoni ya Waheshimiwa
Wabunge katika mkutano wa Tano wa Bunge la 11 kuhusu Mapendekezo ya Serikali
kwa Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2017/18. Katika mkutano tajwa, waheshimiwa
wabunge walitoa maoni na mchango mkubwa uliotuwezesha kuandaa Mpango huu.
Miongoni mwa maoni mahsusi ya Waheshimiwa Wabunge ni kuwa: Ujenzi wa Reli ya
Kati kwa kiwango cha standard gauge
upewe kipaumbele; kuboresha mazingira ya uwekezaji na kufanya biashara;
utekelezaji wa mkakati wa kujenga zahanati katika kila kijiji na vituo vya afya
kila kata; kuimarisha upatikanaji wa madawa na vifaa tiba; kuendeleza maeneo ya
viwanda vidogo, na maeneo mahsusi ya EPZ/SEZ; kutoa kipaumbele kwa utekelezaji
wa miradi ya makaa ya mawe - Mchuchuma na chuma - Liganga; kuboresha elimu ya
juu na kuongeza wigo wa utoaji wa mikopo kwa wanafunzi; kuboresha miundombinu
ya barabara; na programu ya kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.
55. Mheshimiwa Spika, maoni na ushauri wa wadau wengine ambao umezingatiwa katika maandalizi ya
Mpango huu ni pamoja na: Kuimarisha ufuatiliaji na tathmini ya utekelezaji wa
Mpango; upatikanaji wa mikopo ya muda mrefu na nafuu; uimarishwaji wa
miundombinu msingi ya bandari na nishati ya umeme; na kuboresha utoaji wa
huduma msingi za ustawi wa jamii hususan elimu, afya, maji, uboreshaji wa
mipango miji, nyumba na makazi, na utunzaji wa mazingira.
Shabaha na Malengo ya Uchumi Jumla kwa mwaka 2017/18
56. Mheshimiwa Spika, Shabaha na malengo ya uchumi jumla katika kipindi cha mwaka 2017/18 ni kama
ifuatavyo:-
(i)
Kuongeza kasi ya ukuaji
wa Pato Halisi la Taifa kufikia asilimia 7.1 mwaka 2017 ikilinganishwa na
asilimia 7.0 mwaka 2016;
(ii)
Kuendelea kudhibiti
kasi ya mfumuko wa bei na kuhakikisha unabaki kwenye wigo wa tarakimu moja;
(iii) Kuongeza ukusanyaji wa mapato ya ndani (ikijumuisha ya Serikali kuu na Mamlaka
za Serikali za Mitaa) kufikia asilimia 16.5 ya Pato la Taifa;
(iv) Mapato ya kodi kufikia asilimia 14.2 ya Pato la Taifa mwaka 2017/18;
(v)
Matumizi ya Serikali
kufikia asilimia 24.9 ya Pato la Taifa;
(vi) Kuwa na nakisi ya bajeti (ikijumuisha misaada) ya asilimia 3.8 ya Pato la
Taifa;
(vii) Kuwa na akiba ya fedha za kigeni kwa kiwango kinachokidhi mahitaji ya
uagizaji wa bidhaa na huduma kutoka nje kwa kipindi kisichopungua miezi minne
(4); na
(viii) Kuhakikisha utulivu wa thamani ya Shilingi ya Tanzania.
Maeneo ya Kipaumbele 2017/18
57.
Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia shabaha
na malengo haya, miradi iliyobainishwa kuwa ya kipaumbele kwa Mpango wa
Maendeleo wa Mwaka 2017/18 ni ile inayotarajiwa kutoa matokeo makubwa kuendana
na malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025 na Mpango wenyewe. Mingi ya
miradi hii utekelezaji wake ulianza mwaka 2016/17, hivyo inaendelea. Hii ni
pamoja na miradi ya: ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha Standard Gauge; Kuhuisha Shirika la
Ndege Tanzania, hususan kukamilisha malipo ya ununuzi wa ndege 4; miradi ya Chuma
cha Liganga na Makaa ya Mawe ya Mchuchuma; Uanzishwaji/Uendelezaji wa Kanda
Maalum za Kiuchumi; Mtambo wa Kuchakata
Gesi Asilia - Lindi; na Shamba la Kilimo na Uzalishaji Sukari Mkulazi. Malengo ya utekelezaji
kwa maeneo haya kwa mwaka 2017/18 yameainishwa katika kitabu cha Mpango wa
Maendeleo kwa Mwaka 2017/18 (Sura ya nne).
58. Mheshimiwa Spika, miradi mingine ya kipaumbele itakuwa
katika maeneo yafuatayo:
(a) Ujenzi wa Msingi wa
Uchumi wa Viwanda: ikihusisha miradi ya:- Uendelezaji
wa Eneo la Viwanda TAMCO - Kibaha; Tathmini ya matumizi ya eneo la Kiwanda cha
General Tyre – Arusha; Mradi wa Magadi Soda – Bonde la Engaruka, Arusha;
kuimarisha Mfuko wa Taifa wa Maendeleo ya Wajasiriamali (NEDF); uendelezaji wa
maeneo ya viwanda vidogo katika mikoa ya Morogoro, Dar es Salaam, Mbeya,
Mwanza, Kigoma na Mtwara; ujenzi wa ofisi za SIDO katika mikoa mipya. Maeneo
mengine ni pamoja na kuendeleza viwanda vya ngozi, kupanua mnyororo wa thamani
wa pamba hadi nguo na uzalishaji wa madawa na vifaa tiba nchini. Kwa lengo
hili, Serikali itaendelea kuhamasisha uwekezaji binafsi hususan katika viwanda
vinavyotumia malighafi zinazopatikana kwa wingi nchini ikiwa ni pamoja na viwanda
vya kusindika nyama, maziwa, maji, misitu, chokaa, mawe urembo, gypsum na mazao ya vyakula na matunda.
Serikali itaendelea kuziimarisha taasisi zake ili kuwekeza katika viwanda kwa
njia ya PPP.
(b) Kufungamanisha Ukuaji
wa Uchumi na Maendeleo ya Watu: Miradi katika eneo
hili ni ile inayolenga kuimarisha upatikanaji wa fursa za: Elimu na Mafunzo ya
Ufundi: Kugharamia
Elimumsingi bila malipo; Kupanua ruzuku na mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya
juu; Ununuzi wa vifaa kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum; ukarabati na upanuzi
wa Maktaba ya Mkoa – Dodoma; na ujenzi wa Vyuo vitano vya VETA katika Mikoa ya
Geita, Simiyu, Njombe, Rukwa na Kagera. Kwa upande wa Afya na Maendeleo ya Jamii ni: hatua zitaendelezwa za kuboresha
Hospitali za Rufaa na mikoa; kuhakikisha upatikanaji wa vifaa vya kisasa;
kuimarisha upatikanaji wa dawa, vifaa, vifaa tiba na vitendanishi katika
hospitali, vituo vya afya na zahanati; kuongeza udhibiti wa magonjwa ya
kuambikiza; na kudhibiti maambukizi mapya ya virusi vya UKIMWI, hususan kwa
vijana. Miradi
ya Maji: ukarabati na upanuzi wa huduma za maji Vijijini; kuboresha huduma
za maji katika Jiji la Dar es Salaam; mradi wa kutoa maji Ziwa Victoria kwenda
Kahama, Nzega, Igunga, Tabora hadi Sikonge; ujenzi, ukarabati na upanuzi wa
huduma za maji mijini na vijijini; na kutoa maji mto Ruvuma kwenda Manispaa ya
Mtwara-Mikindani; kujenga na kuimarisha hifadhi ya vyanzo vya maji na misitu,
upandaji miti, uvunaji wa maji, kuhimiza matumizi ya teknolojia jadidifu na
hifadhi ya mazingira. Hatua nyingine ni pamoja na kupanua upatikanaji wa maji
safi, utunzaji wa mazingira,
na kuimarisha uhimilivu dhidi ya mabadiliko ya tabia nchi.
(c) Mazingira Wezeshi kwa
Uendeshaji Biashara: katika eneo hili, Serikali itaendelea na azma yake ya
kupanua miundombinu ya huduma za kiuchumi kufikia azma yake ya kuboresha
mazingira ya biashara ikihusisha miradi inayoendelea ya ukarabati wa
miundombinu ya reli; miradi ya barabara na madaraja katika barabara za Kidahwe
– Kasulu – Kibondo – Nyakanazi, Manyoni – Tabora – Uvinza, Tabora – Koga –
Mpanda; Ujenzi wa barabara za juu za TAZARA na Ubungo Interchange; ujenzi wa Daraja la Selander na miundombinu ya mabasi yaendayo haraka (awamu ya II, III na IV)
jijini Dar es Salaam. Aidha, miradi ya bandari ikijumuisha bandari za Dar es
Salaam, Mtwara, Tanga, Bagamoyo, bandari kavu ya Ruvu na bandari za Maziwa Makuu
(Victoria, Tanganyika na Nyasa). Kwa upande wa usafiri wa anga, Serikali
itaendelea na ujenzi wa jengo la abiria
(terminal III) katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere; upanuzi
wa uwanja wa ndege wa Kigoma, Tabora na Mwanza; ujenzi na ukarabati wa viwanja
vya ndege vya Geita, Sumbawanga, Shinyanga, Mtwara, Musoma, Iringa na Songea;
na ukarabati wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa Kilimanjaro.
(d) Kuimarisha Utekelezaji
wa Mpango na Miradi: Serikali itaendelea
kuchukua hatua ya kuimarisha mitaji ya benki za ndani za maendeleo (TIB na
TADB) na kuanza utaratibu wa kuzitumia kama vyombo vyake vya ukusanyaji wa
mikopo ya muda mrefu na ya gharama nafuu kwa wawekezaji. Aidha, eneo hili litajumuisha
miradi ya kuendeleza na kusimamia matumizi ya ardhi; kuimarisha
mipango miji; maendeleo ya nyumba na makazi; kuweka
mfumo utakaowezesha nchi kufaidika na ushirikiano wa kikanda na kimataifa; kuimarisha utawala bora na
utawala wa sheria.
Serikali itaendelea kuweka mazingira wezeshi ili kuchochea ushiriki na maendeleo
ya sekta binafsi, hususan, sekta binafsi ya ndani, katika utekelezaji wa Mpango
na ujenzi wa viwanda. Serikali itaendelea kuboresha kanuni, taratibu na mifumo
ya taasisi ya usimamizi wa biashara na uwekezaji nchini. Kwa kuzingatia hili,
Serikali itaendelea kuchukua hatua mbalimbali, ikiwa ni pamoja na:
(i) Kufanya mapitio ya sera, sheria na taratibu
zinazochochea ushiriki wa sekta binafsi, ama kuwekeza moja kwa moja au kwa ubia
na sekta ya umma;
(ii) Kutenga maeneo ya uwekezaji ili kupunguzia sekta
binafsi usumbufu hususan upatikanaji wa ardhi ikiwa ni pamoja na kutenga maeneo
mahsusi ya uwekezaji (EPZ, SEZ na kuanzisha land
bank chini ya TIC), na kuyawekea maeneo hayo miundombinu msingi, na
kuikodisha kwa wawekezaji kwa gharama nafuu;
(iii) Kujenga miundombinu wezeshi (barabara, umeme,
maji na reli) na kuifikisha katika maeneo ya shughuli za wawekezaji;
(iv) Kusimamia utekelezaji wa sheria na taratibu na
kuhakikisha kuwepo kwa amani na usalama;
(v) Kuimarisha mifuko maalum ya kuchochea ushiriki wa
sekta binafsi, kwa mfano SAGCOT Catalytic
Fund na PPP Facilitation Fund;
(vi) Kuboresha huduma kwa wawekezaji, ikiwa ni pamoja
na kuimarisha “one stop centre” chini ya TIC, bandari ya Dar es Salaam na vituo
vya utoaji huduma ya pamoja mipakani (one stop border post); na
(vii) Kuweka utaratibu utakaoboresha upatikanaji wa
mikopo ya muda mrefu kwa gharama nafuu ikiwa ni pamoja na kuimarisha mitaji ya
benki maalum za maendeleo (TADB) na (TIB).
(e) Kuhamishia Makao Makuu
ya Shughuli za Serikali Kuu Dodoma: katika mwaka 2017/18 Serikali itaendelea na utekelezaji wa
azma ya kuhamishia shughuli za Serikali makao makuu Dodoma. Katika utekelezaji
wa azma hii, Wizara zimeelekezwa kutenga fedha za kugharamia stahili za
watumishi kwa kutumia ukomo wa bajeti uliotengwa kwenye mafungu yao. Ofisi ya
Waziri Mkuu inaendelea kuratibu upatikanaji wa maeneo ya kujenga ofisi na
nyumba za viongozi wa Serikali kwa kuzingatia mahitaji na maboresho ya mpango
wa ardhi katika mji wa Dodoma.
59. Mheshimiwa Spika, kwa kuitikia wito wa Serikali wa kujenga uchumi wa viwanda, mifuko ya
hifadhi ya jamii imeonesha nia ya kuwekeza katika miradi ya viwanda katika
maeneo mbalimbali nchini. Baadhi ya miradi ambayo inatarajiwa kutekelezwa na
mifuko hii katika mwaka 2017/18 ni pamoja na ufufuaji wa: kiwanda cha sukari
katika Gereza la Mbigiri Dakawa Morogoro; kiwanda cha kutengeneza viatu katika
Gereza la Karanga Moshi; kiwanda cha nguo cha urafiki; Dar Es Salaam; kiwanda
cha Morogoro Canvas Mill; kiwanda cha chai cha Mponde kilichopo Lushoto Mkoani
Tanga; kiwanda cha Kilimajaro Machine Tools, Kilimanjaro (KMTC) na kiwanda cha
Kubangua Korosho cha Tandahimba na Newala. Vile vile, mifuko hii inatarajia
kuanzisha viwanda vipya katika maeneo mbalimbali, vikiwemo: kiwanda cha dawa;
kiwanda cha kuzalisha bidhaa za hospitali na gesi ya oksijeni; kiwanda cha
kusindika zabibu, Chinangali Dodoma; viwanda vya kusindika nafaka na ukamuaji
wa mafuta; na kiwanda cha kuzalishaji wanga kutokana na zao la muhogo na viazi
vitamu huko Lindi.
60. Mheshimiwa Spika, maelezo ya kina kuhusu Miradi ya
Kipaumbele yapo katika kitabu cha Mpango (Sura ya Nne).
61. Mheshimiwa Spika, vipo vihatarishi
mbalimbali ambavyo vinaweza kuathiri utekelezaji wa miradi ya maendeleo.
Vihatarishi hivyo vinaweza kuwa vya ndani au vya nje. Kihatarishi kikuu cha
ndani ni ufinyu wa rasilimali fedha na uwepo wa tofauti za mpangilio wa
vipaumbele, mpango-kazi na mtiririko wa upatikanaji fedha baina ya taasisi za
utekelezaji. Vihatarishi vya nje ni pamoja na: mitikisiko ya kiuchumi kikanda
na kimataifa; majanga asilia na athari za mabadiliko ya tabianchi; na
mabadiliko ya kiteknolojia.
62. Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kushirikiana na wadau katika
kutekeleza Mpango huu, imebainisha na kuweka tahadhari kwa kuchukua hatua
zifuatazo:- kuandaa bajeti yenye mwelekeo wa kupunguza utegemezi wa kibajeti kwa
kuwianisha vyanzo vya mapato na mkakati
wa kuyakusanya na kuwianisha matumizi na upatikanaji wa mapato ya Serikali; kuboresha
mazingira ya biashara kwa lengo la kuimarisha sekta binafsi kuchangia utekelezaji
wa baadhi ya miradi; na kuendelea kutoa elimu kwa umma kuhusu Mpango na namna
bora ya utekelezaji ili kuongeza ushiriki wa jamii na sekta binafsi.
Ugharamiaji wa Mpango 2017/18
Sekta ya Umma
63.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2017/18, Shilingi bilioni
11,999.6 zimetengwa kwa ajili ya kugharamia utekelezaji wa miradi ya maendeleo
ambapo Shilingi bilioni 8,969.8 ni fedha za ndani na Shilingi bilioni 3,029.8 ni fedha za nje. Hivyo, fedha zilizotengwa katika bajeti ya
maendeleo zimeongezeka kutoka Shilingi bilioni 11,820.5 mwaka 2016/17 hadi Shilingi
bilioni 11,999.6 kwa mwaka 2017/18, ikiwa ni sawa na asilimia 38 ya bajeti
yote. Kiasi hiki ni kikubwa kwa asilimia 1.2 ya makadirio ya kutenga Shilingi bilioni
11.80 kila mwaka kutoka mapato ya Serikali kama ilivyojidhihirisha katika
mapitio ya utekelezaji kwa mwaka 2016/17. Serikali itahakikisha kuwa kiasi cha
fedha kilichopangwa kwa matumizi ya maendeleo kinapatikana na kugawiwa kwa
ajili ya kugharamia miradi ya maendeleo iliyokusudiwa na kwa wakati. Hivyo,
pamoja na juhudi za kupanua na kukusanya mapato katika vyanzo vya kawaida vya
Serikali, msisitizo umewekwa katika kubaini na kukusanya kutoka vyanzo vipya. Mfumo
wa ukusanyaji katika baadhi ya maeneo utafanyiwa mabadiliko ili kuongeza
ufanisi.
Mashirika na Taasisi za Umma
64.
Mheshimiwa Spika, katika historia ya nchi yetu na pia nchi nyingi zinazoendelea, Mashirika
ya Umma yamekuwa na mchango mkubwa katika kuchangia maendeleo ya nchi husika.
Kwa kutambua hili, Serikali imeelekeza mashirika na taasisi zake za umma za
kibiashara kuchangia katika kugharamia
utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo nchini. Taasisi hizi zinaweza
kutekeleza hili kupitia mapato na/au kwa kukopa kwa ridhaa ya Serikali kutokana
na dhamana ya mali zao ili kugharamia utekelezaji wa miradi itakayobainishwa
kuwa ya kipaumbele.
Sekta Binafsi
65. Mheshimiwa Spika, kama ilivyojidhihirisha mwaka 2016/17, sekta binafsi, ya ndani na nje,
imepokea kwa hamasa wito wa Serikali wa kuchochea uwekezaji hasa katika maeneo
mengine zaidi ya kilimo na madini. Serikali kupitia Baraza la Taifa la Biashara
itaendelea kusimamia utekelezaji wa maazimio yenye lengo la kuimarisha
mazingira wezeshi ya uwekezaji na uendeshaji biashara nchini. Katika kuvutia
uwekezaji kwa njia ya ubia kati ya sekta ya umma na sekta binafsi, Serikali
itaendelea kuimarisha Mfuko wa fedha wa miradi ya ubia (PPP Facilitation Fund)
kwa lengo la kugharamia uandaaji wa upembuzi yakinifu kwa miradi inayotarajiwa
kutekelezwa kwa njia ya ubia kati ya Serikali na sekta binafsi. Matokeo tarajiwa
ni ongezeko la uwekezaji wa sekta binafsi katika miradi ya kipaumbele kwa njia
ya ubia. Serikali pia imeamua, kwa makusudi kuondoa mlolongo wa kodi kwa sekta
ya kilimo na biashara ndogo ndogo kwa ajili ya kuinua uwekezaji katika sekta
hizi. Vile vile, imechukua hatua za kuhakikisha upatikanaji wa maeneo ya
viwanda na biashara ndogo kwa urahisi. Msukumo pia umewekwa kuboresha
upatikanaji wa mikopo ya gharama nafuu na ya muda mrefu kwa wawekezaji, ikiwa
ni pamoja na kuimarisha benki za maendeleo nchini.
66.
Mheshimiwa Spika, maelezo ya kina kuhusu Ugharamiaji wa Mpango yapo katika
kitabu cha Mpango (Sura ya Tano).
Ufuatiliaji, Tathmini na Utoaji wa Taarifa
68.
Mheshimiwa Spika, Serikali katika kuimarisha eneo hili imeamua
kuweka mfumo wa mafunzo na malezi yatakayoharakisha kuimarisha utaalam wa
kupanga, kutayarisha, kusimamia, kufuatilia na kutathmini utekelezaji wa
miradi. Ninatumia fursa hii kuwaelekeza Maafisa Masuhuli kutenga fedha za
ufuatiliaji na tathmini kama sehemu ya gharama za utekelezaji wa miradi husika.
69.
Mheshimiwa Spika, hatua pia zimechukuliwa kwa lengo la kuhuisha
nyenzo za ufuatiliaji na tathmni. Hii ni pamoja na kuandaa na kutoa mafunzo juu
ya matumizi ya Mwongozo wa Usimamizi wa Uwekezaji wa Umma. Kwa mwaka 2017/18,
mafunzo yatatolewa kwa maofisa wa ufuatiliaji na tathmini kuwawezesha kujua
hatua za msingi katika kuandaa, kuratibu na kutathmini miradi ya maendeleo. Serikali
kupitia Tume ya Mipango itaandaa mfumo wa kuhifadhi taarifa za miradi ya
maendeleo kwa ajili ya kuimarisha upatikanaji wa taarifa za ufuatiliaji na
tathmini.
70.
Mheshimiwa Spika, kwa lengo la kuimarisha vigezo vya kufuatilia na
kutathmini utekelezaji wa miradi, Serikali kupitia Tume ya Mipango itaratibu
zoezi hilo kupitia Mkakati wa Utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa
Miaka Mitano. Hatua hii itasaidia kuboresha upatikanaji wa taarifa za
ufuatiliaji na tathmni ya miradi husika kwa kuzingatia vigezo vya utekelezaji
vilivyokusudiwa kwa kipindi husika.
71. Mheshimiwa Spika, maelezo ya kina kuhusu Ufuatiliaji, Tathmini na Utoaji Taarifa yapo katika
kitabu cha Mpango (Sura ya Sita).
MAJUMUISHO NA HITIMISHO
Majumuisho
72. Mheshimiwa Spika, tangu Serikali ilipotangaza dhamira ya kujenga uchumi wa viwanda kumekuwa
na mwitiko wa uwekezaji, wa umma na binafsi, unaotia matumaini makubwa.
Jitihada hizi hazina budi kuungwa mkono, hususan, kwa kuweka kusudio la
kuendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji na uendeshaji biashara nchini.
Hivyo, hatua za mapitio ya sera, sheria, kanuni na mfumo taasisi wa usimamizi
zitaendelea kuimarishwa ili kuhakikisha kuwa tunakuwa na mfumo unaoakisi
kusudio hili kwa vitendo. Aidha, hasa kutokana na ukweli kuwa sehemu kubwa ya
viwanda vitakavyoanzishwa vitatumia malighafi zinazopatikana kwa wingi hapa
nchini, hatua za makusudi zitaendelea kuchukuliwa kwa lengo la kuongeza
uzalishaji, tija na ubora wa malighafi zinazozalishwa nchini ili kukidhi
mahitaji ya soko linalozidi kukua na kubadilika.
73. Mheshimiwa Spika, kuna kasi kubwa ya mabadiliko ya mfumo wa maisha na matarajio ya jamii,
hasa kundi kubwa la vijana. Matarajio haya ya vijana yanaweza kufikiwa tu ikiwa
wataweza kuajiriwa au kuwa na shughuli za kujiajiri wenyewe. Kwa mantiki hii ni
wajibu wa msingi kabisa wa Serikali kuzidi kupanua fursa za uwekezaji.
Uwekezaji unaweza kuwa ama wa Serikali moja kwa moja, ubia kati yake na sekta
binafsi au wa sekta binafsi moja kwa moja. Kwa kutambua hili, Serikali
inahitaji sana ushirikiano na mshikamano kati yake na sekta binafsi.
Ushirikiano na mshikamano huu unapaswa kuwa mpana na wa kina katika nyanja zote,
kuanzia kuibua, kupanga, kutekeleza na kufuatilia na kutathmini hatua za
utekelezaji. Katika kutekeleza hilo, msukumo umewekwa katika kuimarisha ushirikiano
na sekta binafsi kwa kuandaa mikutano na mashauriano ya mara kwa mara ikiwa
pamoja na ya Baraza la Biashara Tanzania (TNBC) itakayojadili na kutoa
mapendekezo ya namna ya kuondoa changamoto zilizopo.
74. Mheshimiwa Spika, Serikali ya Awamu ya Tano ilitangaza toka mwanzo kabisa azma yake ya
kujitanabaisha kuwa ya ukweli na uwajibikaji hasa katika kusimamia matumizi ya
rasilimali zinazopatikana kwa manufaa ya Taifa na kila mwananchi. Kutokana na
hili, Serikali inaendelea kujielekeza katika kuimarisha makusanyo ya mapato ya
ndani kwa kufanyia mapitio ya mifumo na muundo wa usimamizi wa makusanyo ya kodi,
malimbikizo ya kodi, kupanua wigo wa kodi kwa kusajili walipa kodi wapya,
pamoja na utekelezaji wa mikakati ya kuongeza makusanyo ya kodi. Msukumo pia
umewekwa katika kuongeza matumizi ya teknolojia ya kielektroniki ili kupunguza
athari za mapungufu ya kibinadamu katika kukusanya, kutunza na kuhifadhi fedha
na kumbukumbu. Hatua hizi zote ndizo zitawezesha ustawi wa uchumi na
utekelezaji bora wa Mpango wa Maendeleo.
75. Mheshimiwa Spika, mafanikio yaliyopatikana katika uchumi na utekelezaji wa Mpango yamechangiwa
na wadau mbalimbali wa ndani na nje ya nchi wakiwemo nchi marafiki, washirika
wa maendeleo, sekta binafsi na wananchi kwa ujumla. Kwa niaba ya Serikali,
ninawashukuru wadau hao kwa michango yao.
76. Mheshimiwa Spika, kabla ya kumaliza hotuba yangu napenda kumshukuru Naibu Waziri wa Wizara ya
Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Ashatu K. Kijaji (Mb), Mawaziri na Makatibu Wakuu wa
Wizara zote, Wakuu wa Idara za Serikali na Taasisi zinazojitegemea kwa
ushirikiano wao wakati wote wa maandalizi ya kutayarisha Taarifa ya Hali ya
Uchumi 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa 2017/18. Kipekee napenda
kuwashukuru watendaji wote wa Wizara ya Fedha na Mipango wakiongozwa na Katibu
Mkuu Bw. Doto James kwa kusimamia vizuri kazi za kila siku za Wizara. Aidha,
niwatambue Bw. Maduka Kessy, Kaimu Katibu Mtendaji, viongozi na watumishi wote
wa Tume ya Mipango kwa kufanikisha maandalizi ya hotuba hii.
Hitimisho
77. Mheshimiwa Spika, napenda kuwashukuru Waheshimiwa
Wabunge na wananchi wote kwa kunisikiliza. Aidha, hotuba hii na vitabu vya Hali
ya uchumi 2016, na Mpango wa Maendeleo wa Taifa 2017/18 vinapatikana katika
tovuti ya Wizara ya Fedha na Mipango www.mof.go.tz na www.mipango.go.tz.
78. Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo
naomba sasa Waheshimiwa Wabunge wapokee, kujadili na kupitisha Taarifa ya Hali
ya Uchumi 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa 2017/18.
79. Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.
Hakuna maoni :
Chapisha Maoni