.

.

.

.

.

.

.

.
KARIBUNI TUHABARIKE, TUELIMISHANE, TUPEANE HABARI ZA KUKUFANYA UTABASAMU KIDOGO NA MATUKIO YALIYOFANYIWA UCHUNGUZI WA KINA TOKA KILA PEMBE CONTACTS: +255 787 377 722 Email: drweyunga@gmail.com PIA UNAWEZA KUNI FOLLOW KUPITIA INSTAGRAM YANGU @drweyunga | TANGAZA NASI ILI UWAFIKIE WATU WENGI ZAIDI.

Alhamisi, 19 Oktoba 2017

NAIBU WAZIRI AMTAKA MKANDARASI WA SHINYANGA AIRPORT KUANZA KAZI HARAKA

Naibu Waziri wa Ujenzi. Uchukuzi na Mawasiliano, (Sekta ya Ujenzi), Mhe. Elius Kwandikwa (katikati) akizungumza na Meneja wa Tanroads Shinyanga, Bw. Bartholomew Ndirimbi (kushoto) na Meneja wa Kiwanja cha Ndege cha Shinyanga, Bw. Julius Msollow (kulia)
                                   Muonekano wa jengo la kiwanja cha ndege cha Shinyanga.
Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Mhe. Elius Kwandikwa, akizungumza na wananchi wa Mwigumbi mkoani Shinyanga, alipofanya ziara ya kukagua barabara ya Mwigumbi – Maswa (KM 50.3), inayounganisha mkoa wa Shinyanga na Simiyu.
Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Mhe. Elius Kwandikwa, akifafanua jambo kwa Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga, Bi. Josephine Matiro (Watatu kushoto), alipofika mkoani humo kukagua maendeleo ya kiwanja cha ndege cha Shinyanga kilichopo eneo la Ibadakuli.

                                                                                                  Na Mwandishi Wetu

NAIBU Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (sekta ya Ujenzi), Mhe. Elius Kwandikwa, amemtaka Mkandarasi wa kampuni ya ujenzi ya China ya CHICO aliyepewa zabuni ya ujenzi wa Kiwanja cha ndege cha Shinyanga kuanza ujenzi huo haraka.

Akizungumza mara baada ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa kiwanja hicho katika eneo la Ibadakuli leo, mkoani Shinyanga, Mhe. Kwandikwa, amesema kuwa haoni sababu ya mkandarasi huyo kuchelewa kuleta vifaa vyake katika eneo la mradi hadi sasa wakati tayari mkataba wa kuanza kazi hiyo umeshasainiwa.

"Mkandarasi hana sababu ya kuchelewa kuanza kazi wakati fedha zipo na zimeshatengwa kwa ajili ya mradi huu na mkataba umeshasainiwa, sasa namwagiza kuleta vifaa vyake na kuanza kazi mara moja", amesema Mhe. Kwandikwa.

Aidha, Mhe. Kwandikwa amemtaka Meneja wa kiwanja hicho, Bw. Julius Msollow kuhakikisha anakuwa bega kwa bega na kutoa ushirikiano kwa kumsimamia mkandarasi huyo, ili kuhakikisha kiwanja hicho kinakamilika mapema na kwa viwango vinavyotakiwa.

"Naamini tukimsimamia vizuri mkandarasi huyu tutapata kiwanja kizuri na imara hapa Shinyanga na tutafungua fursa mbalimbali za kiuchumi katika mkoa huu", amesisitiza Mhe. Kwandikwa.

Kwa upande wake, Meneja wa kiwanja cha ndege cha Shinyanga, Bw. Msollow, amemhakikishia na kuahidi kuwa atatoa ushirikiano kwa mkandarasi huyo atakapowasili eneo la mradi.

Bw. Msollow amesema kuwa mradi huo utahusisha ujenzi wa barabara ya kuruka na kutua ndege, jengo la abiria, maeneo ya maegesho ya ndege na mnara wa kuongozea ndege.

Amesema barabara ya kutua na kupaa kwa ndege inarefushwa kwa urefu wa Kilometa mbili na itakuwa kwa kiwango cha lami, ikigharimu zaidi ya shilingi Bilioni 49.

Wakati huohuo, Naibu Waziri Kwandikwa, amekagua maendeleo ya ujenzi wa barabara ya Mwigumbi - Maswa (KM 50.3), mkoani Simiyu na kumsisitiza mkandarasi anayejenga barabara hiyo kuikamilisha kwa wakati na kwa viwango.

Amesisitiza kuwa kukamilika kwa barabara hiyo ambayo ni kiungo kwa wananchi wa Maswa, Bariadi, Lamadi na Mwanza, kutarahisisha huduma za usafirishaji wa abiria na mizigo katika maeneo hayo.

Naye, Meneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS), mkoani Simiyu, Mhandisi Albert Kent, amesema kuwa mradi upo katika hatua nzuri na unatarajiwa kukamilika ndani ya miaka miwili kutoka sasa.

Naibu Waziri Kwandikwa amefanya ziara ya kikazi katika mkoa wa Shinyanga na Simiyu ambapo amekagua miradi mbalimbali inayotekelezwa na Wizara yake.

Hakuna maoni :

Chapisha Maoni