Mkutano wa siku mbili wa Sekta ya uziduaji (Madini, Mafuta na Gesi) 2017 umeanza hii leo Mjini Dodoma, ukishirikisha wadau mbalimbali ikiwemo asasi za kiraia, serikali pamoja na wanasheria kutoka ndani na nje ya nchi.
Mkutano huo unaoandaliwa na muunganiko wa asasi za kiraia nchini ambazo zinaangazia utawala bora katika sekta ya uziduaji HakiRasilimali, umelenga kujadili sera, sheria na mifumo ya uendeshaji katika sekta hiyo kwa manufaa ya jamii na taifa kwa ujumla.
Akifungua mkutano huo, Padri Steven Munga alisema sekta ya uziduaji ni chachu ya maendeleo nchini hivyo inapaswa kuangaziwa vyema na hatimaye kuleta matokeo chanya kwa taifa.
Mwenyekiti wa Bodi ya HakiRasilimali, Donald Kasongi alisema mchango wa asasi za kiraia katika sekta ya uziduaji ni mkubwa hivyo asasi hizo zinapaswa kushiriki na kushirikishwa ipasavyo katika kuboresha sekta hiyo.
Mstahiki Meya wa Manispaa ya Dodoma, Profesa Davis Mwamfupe alisema mkutano huo ni ishara kwamba suala la kuboresha sekta ya uziduaji si la Rais John Magufuli pekee bali pia asasi za kiraia kwani zina nafasi kubwa ya kuhakikisha rasilimali zilizopo nchini zinabaki kuwa utajiri na siyo laana kwa taifa.
Washiriki wa mkutano huo wametaka mazungumzo zaidi katika kuboresha sekta ya uziduaji nchini ili kuhakikisha inatoa matokeo chanya kwa taifa badala ya kutumia manufaa ya idadi kubwa ya wabunge bungeni kupitisha mikataba mibovu ambayo imeligharimu taifa.
Hakuna maoni :
Chapisha Maoni