.

.

.

.

.

.

.

.
KARIBUNI TUHABARIKE, TUELIMISHANE, TUPEANE HABARI ZA KUKUFANYA UTABASAMU KIDOGO NA MATUKIO YALIYOFANYIWA UCHUNGUZI WA KINA TOKA KILA PEMBE CONTACTS: +255 787 377 722 Email: drweyunga@gmail.com PIA UNAWEZA KUNI FOLLOW KUPITIA INSTAGRAM YANGU @drweyunga | TANGAZA NASI ILI UWAFIKIE WATU WENGI ZAIDI.

Jumapili, 12 Novemba 2017

MWANAFUNZI MWENYE MIMBA JELA NA WAZAZI MPAKA WAMTAJE ALIYESABABISHA MIMBA - RC WANGABO

Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo akiwatahadharisha wanafunzi juu ya kosa la kupata mimba wakiwa shuleni wakati alipotembelea shule hiyo ya Sekondari Kirando Wilayani Nkasi.
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo akivishwa Scarf ya Kumkaribisha katika Shule ya Sekondari Kirando wilayani Nkasi na Kijana wa Scout Juma Rajabu mwanafunzi wa Shule hiyo. 

Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo amewaagiza wakuu wa wilaya na wakuu wa shule Mkoani humo kumkamata na kuwaweka ndani wazazi na mwanafunzi yeyote wa kike atakayebainika kuwa na mimba hadi hapo watakapomtaja aliyesababisha mimba hiyo.

Amesema kuwa kumekuwa na tabia ya kumalizana kienyeji huko majumbani na matokea yake watuhumiwa hawafikishwi sehemu husika ili waweze uwajibishwa na hatimae kupunguza kasi hiyo ya mimba kwa wananfunzi.

“Mwalimu Mkuu unapogundua tu kwamba mwananfunzi ana mimba mweke pembeni ita wazazi wake, washirikishe polisi wawachukue wawekwe ndani kwa muda wa masaa 48, hadi hapo watakapomtaja muhusika wa mimba hiyo, ukifanya hivyo mara kadhaa mabadiliko yatatokea,” Amesisitiza

Ametoa agizo hilo baada ya kusomewa taarifa ya shule ya sekondari Kirando, Wilayani Nkasi wakati alipotembelea kukagua ujenzi wa maabara wa shule hiyo pamoja na na kuongea na wanafunzi, taarifa iliyobainisha kupatikana kwa mimba saba kwa kipindi cha Januari hadi oktoba mwaka huu na kesi zote zipo polisi.

Halikadhalika alitahadharisha kuwa shule yeyote atakayoitembelea katika ziara yake hiyo ya kujitambulisha katika Halmashauri nne za mkoa huo, ihakikishe inabainisha hatua zilizochukuliwa kwa watuhumiwa na zilipofikia na si kueleza tu idadi ya kesi na kuwepo kwa kesi hizo polisi.

Kwa upande wake mwalimu Mkuu wa Shule ya Sekondari Kirando Erneo Mgina amesema kuwa kati ya wanafunzi saba waliopata ujauzito wanafunzi watatu ni wa “A – Level” na wanne ni wa “O – Level” na kueleza kuwa wengi wao hupata mimba wakati wa likizo na huwabaini pale tu wanaporudi shule na kuwapima.

Marufuku kuuza mbolea tofauti na bei elekezi

Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo ameagiza kukamatwa kwa wafanyabiashara wote wanaouza wanaouza pembejeo kwa zaidi ya bei elekezi iliyotolewa rasmi na serikali kwani kufanya hivyo ni kukiuka utaratibu uliowekwa na serikali kwaajili ya kuwanufaisha wakulima.

Amesema kuwa kumekuwa na baadhi ya maduka katika Manispaa ya Sumbawanga wanauza mbolea kwa bei isiyo halali na hivyo tayari ameshaagiza vyombo vya dola viwashughulikie watu hao haraka iwezekanavyo.

“Ni marufuku kwa wauzaji wa pembejeo kuuza mbolea kwa bei ambayo ni nje ya bei elekezi, msako mkali utafanyika kwa halmashauri zote kuhakikisha kuwa bei elekezi ndio inayotumika na kuwabaini wale wote wanaouza kinyume na bei hii elekezi,” Alisisitiza.

Ameongeza kuwa bei hizo zinatofautiana kati ya Halmashauri na Halmashauri na kwa Manispaa ya Sumbawanga bei elekezi kwa mbolea ya kupandia (DAP) ni shilingi 55,427 na ya kukuzia (Urea) ni 42,848. Halmashauri ya Nkasi mbolea ya kupandia (DAP) ni shilingi 55,961 na ya kukuzia (Urea) ni 43382. 

Halmashauri ya Kalambo mbolea ya kupandia (DAP) ni shilingi 57,022 na ya kukuzia (Urea) ni 44,443 na Sumbawanga Vijijini mbolea ya kupandia (DAP) ni shilingi 56,808 na ya kukuzia (Urea) ni 44229.

Atoa wito kwa wafanyabiashara nchini kununua mahindi Rukwa.

Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo ametoa wito kwa wafanyabiashara wote nchini ambao wanahitaji mahindi kufika haraka katika mkoa wa Rukwa kununua zao hilo kwani kumekuwa na ziada ambayo wananchi wanahitaji kuuza lakini soko hakuna.

Amesema kuwa katika wilaya ya Nkasi pekee kuna zaidi ya tani 23,000 za chakula ambacho ni ziada ya wilaya na imekosa wanunuzi na kumuagiza katibu tawala wa Mkoa kuhakikisha anafanya mawasiliano na mikoa mingine ambayo ina upungufu wa chakula ili kuja kununua ziada hiyo ambayo wananchi wamekuwa wakilalamika kukosa soko.

Pia, amemuagiza katibu tawala wa Mkoa kuhakikisha kuwa kunakuwa na mratibu wa mahindi katika kila wilaya ili kuwasaidia wafanyabiashara wa mahindi kutoka nje ya mkoa kupata urahisi wa kununua mahindi na kuwaepusha na utapeli.

“Tani zaidi ya 23,000 ipo kwenye wilaya moja tu, hii ni fursa kwa wafanyabiashara waliopo kwenye mikoa ambayo ina upungufu wa chakula kuja kununua mahindi na kuyapeleka huko wankoyahitaji, hivyo nakuagiza katibu tawala kuhakikisha kuwa unafanya mawasiliano na mikoa na ambayo ina upungufu pamoja na wafanyabishara wenye kuhitaji ili tuweze kuwasaidia wananchi wetu lakini kuwe na mratibu wa kuweza kusimamia hili ili wafanyabiashara hao wasipate tabu,”

Ameyasema hayo baada ya kusomewa taarifa ya wilaya ya Nkasi iliyobainisha uwepo wa ziada ya tani 23,000 za mahindi kwaajili ya kuuza ambapo wakulima wa wilaya hiyo na kwengineko Mkoani humo wamekuwa wakilalamikia soko la zao hilo.

Kwa upande wake Kaimu Katibu Tawala wa wilaya ya Nkasi Mwanaisha Luhaga alipokuwa akisoma taarifa hiyo alisema kuwa changamoto kubwa inayowakabili hivi sasa ni upatikanaji wa mbolea kwa wananchi ambapo mpaka sasa wilaya imepokea tani 20 tu kati ya 850.

Hakuna maoni :

Chapisha Maoni