.

.

.

.

.

.

.

.
KARIBUNI TUHABARIKE, TUELIMISHANE, TUPEANE HABARI ZA KUKUFANYA UTABASAMU KIDOGO NA MATUKIO YALIYOFANYIWA UCHUNGUZI WA KINA TOKA KILA PEMBE CONTACTS: +255 787 377 722 Email: drweyunga@gmail.com PIA UNAWEZA KUNI FOLLOW KUPITIA INSTAGRAM YANGU @drweyunga | TANGAZA NASI ILI UWAFIKIE WATU WENGI ZAIDI.

Alhamisi, 17 Desemba 2015

DK. SHEIN AKUTANA NA UJUMBE WA KAMPUNI YA CNOOC KUTOKA CHINA

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein akisalimiana na Makamo Rais wa Kampuni ya Kimataifa ya CNOOC kutoka Nchini China Cui Hanyun wakati alipofika ikulu mjini Zanzibar leo na ujumbe aliofuatana nao.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) akizungumza Ujumbe wa Kampuni ya China National Offshore Oil Company ltd (CNOOC) ulifoka Ikulu Mjini Zanzibar kuonana na Rais ukiongozwa na Balozi wa China nchini Tanzania Xie Yunliang (wa pili kulia) na Makamo Rais wa Kampuni ya Kimataifa ya (CNOOC) Cui Hanyun (katikati) wengine ni viongozi wa juu wa kampuni hiyo,[Picha na Ikulu.]
 
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa azma ya Kampuni ya China National Offshore Oil Company (CNOOC) ya kutaka kuanzisha ushirikiano katika sekta ya mafuta na gesi hapa nchini itasaidia katika kutekeleza lengo la Zanzibar la kuinua uchumi wake.

Dk. Shein aliyasema hayo leo huko Ikulu mjini Zanzibar wakati alipokuwa na mazungumzo na Ujumbe wa Kampuni ya China National Offshore Oil (CNOOC) uliofuatana na Balozi mdogo anayefanyia kazi zake hapa Zanzibar Mhe. Xie Yunliang.

Katika mazungumzo hayo, Dk. Shein alisema kuwa China ina historia kubwa katika harakati zake za kuiunga mkono Zanzibar tokea mwaka 1964 na kuanzia hapo hadi hii leo iko bega kwa bega na Zanzibar hivyo azma ya Kampuni ya CNOOC kutoa ushirikiano wake kwa Zanzibar katika kuendeleza juhudi za Serikali katika kuinua sekta ya nishati itasaidia kukuza uchumi na maendeleo ya Zanzibar.

“Uhusiano wa Zanzibar na China ni wa kihistoria na ulianza muda mrefu hivyo, kujitokeza kwa Kampuni ya CNOOC kutoka nchini humo kutazidisha ushirikiano kama ilivyo kwa sekta nyenginezo hatua ambayo itasaidia lengo na madhumuni ya Zanzibar katika kuimarisha uchumi wake”, alisema Dk. Shein.

Aidha, Dk. Shein alisisitiza kuwa jambo muhimu katika ushirikiano huo ni kupata utaalamu na uzoefu kutoka kwa Kampuni hiyo ikiwa ni pamoja na kutoa nafasi za masomo zinazohusiana na sekta hiyo kwa wazalendo hatua ambayo itasidia kufikia lengo lililokusudiwa.

Dk. Shein alisema kuwa Zanzibar imeweza kupata ushirikiano mkubwa kutoka nchi hiyo ikiwa ni pamoja na kuungwa mkono katika sekta zake za maendeleo hivyo azma ya China katika kuiunga mkono Zanzibar kwenye eneo hilo jipya itasaidia kwa kiasi kikubwa kuinua uchumi na maendeleo ya Zanzibar.

Alisema kuwa Zanzibar ina mengi ya kujifunza kutoka kwa ndugu zao wa China hivyo, kwa upande wa sekta ya mafuta na gesi Zanzibar itapata mafanikio makubwa na kuweza kupiga hatua kibiashara na kitaalamu.

Dk. Shein alisema kuwa juhudi za makusudi zimechukuliwa na Serikali zote mbili ile ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuhakikisha suala la mafuta na gesi linatekelezwa na kusimamiwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar hatua ambayo inatoa fursa kwa Zanzibar kushirikiana na Kampuni yoyote yenye sifa na uwezo kutoka nje.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alisema kuwa baada ya kufuatwa kwa taratibu husika za kiserikali katika kutekeleza azma hiyo, Zanzibar itakuwa na matumaini makubwa katika kupata mafanikio kwa kuendeleza ushirikiano huo kwa pande zote mbili.

Nae Makamu wa Rais wa Kampuni hiyo ya CNOOC Bwana Cui Hanyun alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa Zanzibar kwa kuendeleza uhusiano na ushirikino kati yake na China ambao umedumu kwa muda mrefu.

Bwana Hanyun alisema kuwa Kampuni ya CNOOC ni Kampuni kubwa na ya Kitaifa nchini China ambayo imeanza mwaka 1982 ambapo hivi sasa inafanya kazi sehemu mbali mbali duniani zikiwemo nchi za Amerika, Ulaya, Asia, Afrika na Australia.

Miongoni mwa nchi za Afrika ambazo kampuni hiyo inaendeleza shughuli zake ni Kenya, Nigeria, Uganda, Garbon na nchi nyenginezo za Bara la Afrika na kueleza hatua zinazoendelea katika uendelezaji wa sekta hiyo katika nchi hizo.

Bwana Hanyun alisema kuwa Kampuni hiyo imekuwa ikitoa ushirikiano kwa njia mbali mbali ikiwa ni pamoja na kutoa utaalamu juu ya sekta ya mafuta na gesi sambamba na ushauri elekezi.
 
Pamoja na hayo Kiongozi huyo wa Kampuni hiyo aliahidi kutoa ushirikiano wake mkubwa katika kuhakikisha Zanzibar inaimarika katika sekta ya mafuta na gesi na kuweza kupata manufaa ya kimaendeleo na kiuchumi.

Nae Balozi Mdogo anaefanyia kazi zake hapa Zanzibar Mhe. Xie Yunliang alimuhakikishia Dk. Shein kuwa China itaendeleza uhusiano na ushirikiano wake na Zanzibar katika kuimarisha sekta mbali mbali za maendeleo ikiwa ni pamoja na kuendelea kuipa nafasi za masomo nchini humo. Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Hakuna maoni :

Chapisha Maoni