Jumatatu, 8 Februari 2016
WAIMBAJI WA NYIMBO ZA INJILI WATUNUKIWA TUZO ZA HESHIMA KUTOKA CHUO KIKUU AFRICAN GRADUATE UNIVERSITY CHA JIJINI DAR ES SALAAM
Na Dotto Mwaibale
Chuo Kikuu cha African Graduate University kimewatunuku tuzo za heshima za stashahada ya uzamili katika ngazi mbalimbali waimbaji wa nyimbo za injili nchini kutokana na mchango wao katika jamii.
Akizungumza wakati wa kukabidhi tuzo hizo kwa waimbaji hao katika mahafali ya pili ya chuo hicho yaliyofanyika Dar es Salaam juzi Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Askofu Profesa Stephano Nzowa alisema ni jambo jema kuwakumbuka watu mbalimbali waliolifanyia taifa mambo mazuri.
Chuo chetu kimeona ni vema kikawapa tuzo za heshima watu mbalimbali wakiwemo wanamuziki wa nyimbo za injili kwani kupitia uimbaji wao wameweza kutoa mafunzo kwa watu na wengine kuacha kutenda dhambi na kuamua kuokoka" alisema Profesa Nzowa.
Baadhi ya waimbaji wa nyimbo za injili waliotunukiwa tuzo hizo ni Rais wa Shirikisho la Muziki Tanzania, Ado Novemba ambaye alitunukiwa tuzo ya heshima ya udaktari, Stella Joel ambaye ametunukiwa Tuzo ya Heshima ya Shahada ya Uzamili ya Mahusiano na Upendo Mbila aliyetunukiwa Tuzo ya Heshima ya Shahada ya Uzamili ya Uongozi wa Umma.
Akizungumza baada ya kupata tuzo hiyo Stella Joel alisema anamshukuru mungu kwa kumuwezesha kupata tuzo hiyo na kuwa imemtia nguvu kuendelea kufanya kazi ya mungu kupitia uimbaji.
Kwa upande wake Upendo Mbila alitoa shukurani zake kwa chuo hicho kwa kutambua mchango wa waimbaji wa nyimbo za injili kwa kuwapa tuzo hizo ambazo ni muhimu kwao.
(Imeandaliwa na mtandao wa www.habari za jamii.com-simu namba 0712-727062)
Jisajili kwenye:
Chapisha Maoni
(
Atom
)
Hakuna maoni :
Chapisha Maoni