Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo anaeshughulikia Kilimo na Maliasili Bibi Maryam Juma Abdullah (aliyesimama) akiwakaribisha ugeni kutoka Benki ya Maendeleo ya Kilimo ya Tanzania (TADB).
Na Mwandishi wetu,
Benki ya Maendeleo ya Kilimo ya Tanzania (TADB) imeanza kuchangamkia fursa za uwekezaji katika sekta ya kilimo na mifugo visiwani Zanzibar kwa kuanza mchakato wa kutoa mikopo kwa wakulima na wakazi wa visiwa hivyo wanaojishughulisha katika uchakataji wa mazao ya kilimo visiwani humo.
Akizungumza wakati wa walipotembelea Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi, visiwani humo Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Benki hiyo, Bw. Francis Assenga alisema kuwa TADB ikiwa chombo cha Muungano ina wajibu kusaidia juhudi za Serikali katika kuinua ukuaji wa uchumi na kupunguza umaskini nchini Tanzania hasa katika kuchagiza mapinduzi na maendeleo katika Sekta ya Kilimo, ambayo inaajiri zaidi ya asilimia 75 ya watu wenye uwezo wa kufanya kazi nchini na pia kutoa kiasi cha zaidi ya asilimia 65 cha mali ghafi kwa ajili ya viwanda vya nchi.
“Uanzishwaji wa TADB unatokana na Serikali kutambua umuhimu wa uwekezaji wenye tija kwenye maeneo yote ya sekta ya Kilimo na kuleta mapinduzi ya dhati ya Kilimo ili kuwezesha upatikanaji wa mikopo na mitaji ya riba nafuu ikiwa ni pamoja na kuhamasisha mabenki na taasisi zingine za fedha nchini kutoa mikopo zaidi kwenye sekta ya Kilimo,” amesema.
Bw. Assenga amesema Zanzibar ina utajiri mkubwa kwenye uzalishaji wa viungo ‘spices’ ambayo ni mojawapo wa minyororo ya thamani ya mwanzo inayopatiwa mikopo kwa ajili ya uongezaji wa thamani mazao mbalimbali na Benki ya Kilimo.
Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo anaeshughulikia Kilimo na Maliasili Bibi Maryam Juma Abdullah ameishukuru Benki hiyo kwa kuiangalia Zanzibar kuwa sehemu ya kimkakati na kutaka kuanza mikopo visiwani humo.
Hakuna maoni :
Chapisha Maoni