.

.

.

.

.

.

.

.
KARIBUNI TUHABARIKE, TUELIMISHANE, TUPEANE HABARI ZA KUKUFANYA UTABASAMU KIDOGO NA MATUKIO YALIYOFANYIWA UCHUNGUZI WA KINA TOKA KILA PEMBE CONTACTS: +255 787 377 722 Email: drweyunga@gmail.com PIA UNAWEZA KUNI FOLLOW KUPITIA INSTAGRAM YANGU @drweyunga | TANGAZA NASI ILI UWAFIKIE WATU WENGI ZAIDI.

Jumanne, 20 Februari 2018

VIJIJI VYOTE KUPATIWA MAJI SAFI NA SALAMA-MAJALIWA

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewahakikishia wananchi wa wilaya ya Misungwi kuwa vijiji vyote vitapatiwa huduma ya maji safi kupitia miradi inayotekelezwa katika wilaya hiyo ukiwemo wa Mbarika-Misasi utakaogharimu sh. bilioni 12.4.

Alitoa kauli hiyo jana (Jumatatu, Februari 19, 2018) wakati akizungumza na wananchi mara baada ya kuweka jiwe la ujenzi wa mradi huo akiwa katika siku ya tano ya ziara yake ya kikazi mkoani Mwanza. Mradi huo unatarajiwa kuhudumia vijiji 12.

Vijiji hivyo ni Igenge, Lutalutale, Bugisha, Ngaya, Ikula, Sumbugu, Matale, Kasololo, Isuka, Nduha, Manawa na Misasi ambapo jumla ya wakazi 47,011 wanatarajiwa kunufaika na mradi huo.

Alisema Serikali ya Awamu ya Tano ina mikakati mizuri inayolenga kumaliza tatizo la upatikanaji wa maji safi na salama katika maeneo mbalimbali nchini vikiwemo vijiji vya wilaya ya Misungwi ili kuwawezesha wananchi hasa wanawake kushiriki katika shughuli za maendeleo kuliko kutafuta maji.

Waziri Mkuu alisema Serikali kupitia Kampeni ya Rais Dkt. John Magufuli ya kumtua mama ndoo, itahakikisha wananchi katika maeneo yote nchini wanapata huduma ya maji safi na salama katika umbali usiozidi mita 400 kutoka kwenye makazi yao.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Wilaya ya Misungwi, Bw. Eliud Mwaiteleke alisema mradi huo umegawanyika katika miradi midogo minne ambayo ni Igenge, Mbarika-Ngaya, Ngaya-Matale na Matale-Manawa-Misasi.

Alisema shughulli zilizokamilika ni pamoja na ujenzi wa vituo 48 vya kuchotea maji, matanki mapya manne na moja limekarabatiwa pamoja na mtandao wa mabomba wenye urefu wa kilomita 73,087.

Awali, Waziri Mkuu aliweka jiwe la msingi la ujenzi wa shule ya Sekondari ya Kata ya Gulumungu katika kijiji cha Nyamayinza, ambapo aliwapongeza wakazi wa kata hiyo kwa uamuzi wa kujenga shule, ambayo itawawezesha watoto wao kupata elimu.

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
JUMANNE, FEBRUARI 20, 2018.

Hakuna maoni :

Chapisha Maoni