.

.

.

.

.

.

.

.
KARIBUNI TUHABARIKE, TUELIMISHANE, TUPEANE HABARI ZA KUKUFANYA UTABASAMU KIDOGO NA MATUKIO YALIYOFANYIWA UCHUNGUZI WA KINA TOKA KILA PEMBE CONTACTS: +255 787 377 722 Email: drweyunga@gmail.com PIA UNAWEZA KUNI FOLLOW KUPITIA INSTAGRAM YANGU @drweyunga | TANGAZA NASI ILI UWAFIKIE WATU WENGI ZAIDI.

Jumatano, 6 Mei 2015

WANANCHI NA TAASISI WATAKIWA KUCHUKUA TAHADHARI WANAPOTAKA KUPIMA MAENEO YAO YA ARDHI KUEPUKA KUTAPELIWA

Mkurugenzi Msaidizi wa Upimaji na Ramani vijijini wa Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Bw. Huruma Lugalla (kushoto) akitoa maelekezo kwa wataalam wa Upimaji na Ramani wa wizara hiyo wakati wa uhakiki wa moja ya ramani ya eneo linalopaswa kuwa la makazi ya watu na taasisi nje kidogo ya mji wa Chalinze, Bagamoyo mkoani Pwani iliyopimwa na Kampuni ya Intergrated Property Consultancy and Services (IPCS) ya Morogoro na kubainika kuwa chini ya kiwango.
Wataalam wa Upimaji na Ramani wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi wakifanya uhakiki wa moja ya ramani ya eneo linalopaswa kuwa la makazi ya watu na taasisi nje kidogo ya mji wa Chalinze, Bagamoyo mkoani Pwani lililopimwa chini ya kiwango. Katikati (aliyesimama) ni Bw. Bernard Malugu, Mkurugenzi wa Kampuni ya Intergrated Property Consultancy and Services (IPCS) ya Morogoro iliyoifanya kazi hiyo chini ya kiwango.
 
                                                                                    Na. Aron Msigwa –MAELEZO
 
Dar es salaam. Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imeto tahadhari kwa Taasisi na wananchi wanaotaka kupimiwa maeneo yao ya ardhi kuhakikisha kuwa wanafuata sheria, kanuni na taratibu zinazosimamia masuala ya upimaji wa ardhi ili kuepuka kupata hasara na kuingia kwenye migogoro ya ardhi isiyo ya lazima kutokana na kutumia watu au makampuni yasiyosajiliwa kishera.

Hatua hiyo imekuja kufuatia baadhi ya makampuni yanayojishughulisha na upimaji wa Ardhi na ramani kugundulika kufanya kazi za wateja wao chini ya viwango kufuatia ramani zilizowasilishwa na makampuni hayo wizarani hapo kwa ajili ya kuidhinishwa kukosa sifa pindi zinapofanyiwa uhakiki na wataalam wa wizara hiyo.

Mkurugenzi Msaidizi wa Upimaji na Ramani vijijini wa wizara hiyo Bw. Huruma Lugalla akizungumza mara baada ya timu ya wataalam wa wizara hiyo kufanya uhakiki wa moja ya ramani ya eneo linalopaswa kuwa la makazi ya watu na taasisi nje kidogo ya mji wa Chalinze, Bagamoyo mkoani Pwani ambalo upimaji wake umekiuka kanuni na taratibu amesema Serikali haitayafumbia macho makampuni yote yanayochukua fedha za wananchi na Taasisi na kisha kufanya upimaji usiokidhi viwango vilivyowekwa na wizara hiyo kwa mujibu wa Sheria.

Amesema wizara hiyo itaendelea kuchukua hatua mbalimbali ikiwemo kuyafungia makampuni yote yanayobainika kufanya kazi chini ya kiwango, kukiuka kwa makusudi taratibu za upimaji wa ardhi na kufanya uzembe wa kushindwa kuweka mipaka na alama sahihi za maeneo wanayoyapima jambo linalochangia mivutano na migogoro pindi maeneo husika yanapogawiwa kwa wananchi.

“Nawaomba wananchi na Taasisi mbalimbali zinazotaka kupimiwa maeneo yao kwa kutumia makampuni kuwa makini na kuchukua tahadhari ili kuepuka hasara ya kulipa gharama za upimaji mara mbili, msichukue watu wa kati au kampuni zisizosajiliwa kisheria ambazo haziko kwenye orodha ya Katibu wa Baraza la Taifa la Wapima Ardhi” Amesisitiza. 
 
Bw. Lugalla ameeleza kuwa Kampuni ya Intergrated Property Consultancy and Services (IPCS) kutoka Morogoro iliyohusika na zoezi la upimaji na ramani katika eneo hilo haikufuata sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa kwa mujibu wa sheria kufuatia ramani iliyowasilishwa na Mkurugenzi wake Bw. Bernard Malugu wizarani hapo kushindwa kukidhi vigezo vya ubora unaotakiwa mara baada ya kuhakikiwa na wataalam wa Upimaji na ramani wa Wizara.

Amesema wataalam wa upimaji na ramani wa Wizara hiyo mara baada ya kufanya uhakiki wa eneo hilo wamebaini ukosefu wa alama (bikoni) za baadhi viwanja, kukosekana kwa pini za kugawa viwanja na tofauti umbali wa eneo la kiwanja kimoja hadi kingine iliyokuwepo kwenye ramani ambayo haikuendana na uhalisia wa eneo husika wakati wa zoezi la uhakiki.

Aidha, amebainisha kuwa ramani ya eneo hilo ilisainiwa kimakosa na Mkurugenzi wa Kampuni hiyo kufuatia kampuni yake ambayo imesajiliwa kisheria dhamana kuamua kumtafuta mtu wa kati wa kuifanya kazi hiyo badala yake na kisha Mkurugenzi wake Bw. Bernard Malugu kuidhinisha ramani hiyo kwa kuisaini huku ili ipelekwe wizarani kupatiwa kibali huku akijua wazi kanuni na taratibu zinazosimamia sekta hiyo hazimruhusu kutoa kazi kwa mtu au kampuni nyingine.

“Ili kuepusha migogoro ya ardhi inayoweza kutokea katika eneo lile taratibu zitafuatwa ili kampuni hiyo iifanye kazi ile upya kwa gharama zake na kisha kuwaita wataalam wa wizara kufanya uhakiki upya ili kujiridhisha kabla ya kutoa kibali cha viwanja hivi, Sisi kama wizara hatutakubali kuendelea kulaumiwa na wananchi kwa uzembe unaofanywa na makampuni haya” Amesisitiza.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Kampuni ya IPCS iliyopewa kazi ya kupima eneo hilo akitoa utetezi kwa kampuni yake mara baada ya kufanyika kwa uhakiki huo alikiri kuwa kampuni yake imefanya makosa na kukiuka sheria, miiko na maadili yanayosimamia shughuli za upimaji na ramani nchini. Amesema yeye kama Mkurugenzi wa kampuni hiyo alisaini ramani ya eneo hilo Machi 19, 2015 kimakosa hivyo kampuni yake imeonyesha uzembe na udhaifu wa usimamizi ikiwemo yeye mwenyewe kutomfahamu mtu wa kati aliyeifanya kazi hiyo.

Aidha, amesema kampuni yake iko tayari kuyabeba mapungufu yote yaliyojitokeza na kukubali kurudia kazi ya kupima na kuweka mipaka iliyokosekana endapo itaruhusiwa na wizara hiyo kufanya hivyo.

Hakuna maoni :

Chapisha Maoni