Ligi Kuu ya Vodacom inatarajiwa
kuendelea mwishoni mwa wiki kwa viwanja sita kutimua vumbi, michezo
mitatu ikifanyika siku ya jumamosi na michezo mingine mitatu
kufanyika siku ya jumapili.
Katika Uwanja wa Jamhuri mjini
Morogoro, wenyeji timu ya Polisi Morogoro watawakaribisha maafande wa
Ruvu Shooting kutoka Mlandizi, Coastal Union watakua wenyeji wa
Kagera Sugar kwenye dimba la Mkwakwani, huku JKT Ruvu
wakiwakaribisha Azam FC katika uwanja wa Azam Complex Chamazi.
Jumapili Mgambo JKT watakua wenyeji
wa timu ya Ndanda FC kwenye Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga, huku
Mtibwa Sugar wakiwa wenyeji wa wagonga nyundo timu ya Mbeya City
katika Uwanja wa Manungu Turiani.
Katika Uwanja wa Taifa jijini Dar es
salaam watani wa jadi Simba SC watakuwa wenyeji wa Young Africans,
mchezo unaotarajiwa kuanzakutimua vumbi majira ya saa 10 kamili jioni
kwa saa za Afrika Mashariki.
KUZIONA SIMBA, YANGA SH.7,000
Shirikisho la Mpira wa Miguu nchini
(TFF) limetangaza viingilio vya mchezo wa siku ya jumapili kati ya
Simba SC na Young African utakaofanyika kwenye dimba la Uwanja wa
Taifa kuanzia majira ya saa 10 kamili za jioni.
Mchezo huo utachezeshwa na mwamuzi
Martin Saanya kutoka Morogoro, akisaidiwa na Soud Lila (DSM) mshika
kibendera wa kwanza, Florentina Zabron (Dodoma) mshika kibendera wa
pili, Mwamuzi wa akiba Israel Mjuni (DSM), na kamisaa wa mchezo ni
Ame Santimeya (DSM).
Viingilio vya mchezo huo, VIP A sh.
40,000, VIP B sh. 30,000, VIP C sh. 20,000, Rangi ya Machungwa
(Orange) sh. 10,000, huku Rangi ya Bluu na Kijani ikiwa ni sh. 7,000.
Tiketi zitaanza kuuzwa keso
(jumamosi) saa 2 kamili asubuhi katika vituo vya, Karume (Ofisi za
TFF), Mgahawa wa Steers (Posta Mpya), Oilcom (Buguruni), BigBon
(Kariakoo), Olicom (Ubungo), Dar Live (Mbagala), Uwanja wa Uhuru,
Kivukoni (Ferry) na Makumbusho (kituo cha mabasi).
Magari yenye vibali maalum ndiyo
yatakayoruhusiwa kuingia ndani ya uwanja siku ya jumapili kwa kupitia
barabara ya Mandela na Uwanja wa Uhuru, barabara ya Chang'ombe
itafungwa kuanzia saa 12 kamili asubuhi.
TFF inawaomba, wapenzi, washabiki na
wadau wa mchezo kununua tiketi katika vituo vilivyotajwa ili kuepuka
kuuziwa tiketi bandia, ili kuimarisha ulinzi na usalama wa mchezo,
mashabiki wenye mabegi, silaha, vilevi na chupa za maji
hawataruhusiwa kuingia navyo uwanjani.
Aidha katika mchezo huo TFF itatoa
ujumbe maalum kupitia kwa wachezaji kuhamasisha juhudi za Taifa za
kuzuia mauaji dhidi ya watu wenye ulemavu wa ngozi (Albino).
TAIFA STARS KUIVAA MALAWI
Timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa
Stars) itashuka dimbani jumapili Machi 29 mwaka huu, kucheza mchezo
wa kirafiki na timu ya Taifa ya Malawi (The Flames) katika Uwanja wa
CCM Kirumba jijini Mwanza.
Mchezo huo wa kirafiki ambao upo
katika kalenda ya FIFA kwa timu za Taifa (Machi 23-31) na utatarajiwa
kuanza majira ya saa 10 na nusu jioni kwa saa za Afrika Mashariki.
NKONGO KUCHEZESHA ZESCO Vs AS KALOUM
Mwamuzi wa kimataifa wa Tanzania
mwenye beji ya FIFA, Israel Mjuni Nkongo amechaguliwa kuchezesha
mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika (CL) kati ya wenyeji Zesco FC ya
Zambia dhidi ya AS Kaloum ya Guinea.
Katika mchezo huo wa kwanza wa
mzunguko wa pili, Nkongo atasaidiwa na washika kibendera John
Kanyenye na Josephat Bulali na mwamuzi wa akiba Waziri Sheha wote
kutoka Tanzania, huku Kamisaa wa mchezo akiwa Mayixole Elvin Shishana
kutoka nchini Afrika Kusini
Mchezo huo unatarajiwa kufanyika
kati ya tarehe 13,14,15 Machi mwaka huu nchini Zambia.
IMETOLEWA NA SHIRIKISHO LA MPIRA WA
MIGUU TANZANIA (TFF)
Hakuna maoni :
Chapisha Maoni