Hakimu mkazi wa mahakama ya Mkoa wa
Dodoma Rebecca Mbilu amemtaka mwenyekiti wa jumuiya ya wafanyabishara
nchini, Johnson Minja kuwaambia wafanya biashara nchini waache
kufunga maduka yao wakati wa kesi yake kwani ni sharti mojawapo la
dhamana yake.
Hakimu Mbilu ameyasema hayo leo
wakati wa kesi inayomkabili mwenyekiti huyo kufuatia wafanyabiashara
nchini kufunga maduka yao kwa ajili ya kuja mkoani Dodoma kusikiliza
kesi inayomkabili mwenyekiti huyo.
Wakati wa kusikiliza kesi hiyo
ambayo imepangwa kutajwa tena Machi 26 mwaka huu, Mbilu amemwambia
Minja awaambie wafanyabiashara kufungua maduka yao wakati kesi hiyo
ikiwa inaendelea mahakamani.
“Moja ya sharti la dhamana yako ni
kuhakikisha kuwa unaendeleza amani wakati wote wa kesi yako ikiwa ni
pamoja na kuwaambia wafanyabiashara waendelee kufungua maduka yao ili
wananchi waendelee kupata huduma, kwanini umewaambia wafanya biashara
wafunge maduka yao?” alihoji hakimu Mbilu.
Hata hivyo Minja amejibu kwa kifupi
kuwa hana taarifa zozote za wafanyabiashara nchini kufunga maduka.
Naye wakili wa Mshtakiwa huyo,
Godfrey wasonga amesema mahakamani hapo kuwa wafanyabiashara walikuja
kusikiliza kesi hiyo siyo kwamba wamefunga maduka yao bali walikuwa
wamekuja mkoani Dodoma kwa ajili ya matembezi yao wakati maduka yao
yakiendelea kutoa huduma.
Lakini katika hali isiyokuwa ya
kawaida wafanyabiashara hao wamemhakikishia hakimu huyo kuwa
wamefunga maduka yao nchi nzima kwa ajili ya kuja kusikiliza kesi
inayomkabili mwenyekiti wao kwani kesi hiyo siyo ya kwake peke yake
bali ni ya wafanyabishara wote Tanzania.
“Unasikia Minja kama
wafanyabishara wataendelea kufunga maduka yao wakati wa kesi yako na
kusababisha wananchi kukosa huduma nitakufutia dhamana na utakwenda
kulala Isanga,” alisema Hakimu Mbilu.
Awali mwendesha mashtaka wa
serikali, Godfrey Wambali ameiomba mahakama kuahirisha kesi hiyo hadi
MAchi 26 kwa kuwa uchunguzi wa kesi hiyo bado haujakamilika.
Mwenyekiti huyo anakabiliwa na
mashtaka mawili ya kuwachochea wafanyabiashara mkoani Dodoma kutenda
kosa na kuwakataza wafanyabiashara nchini wasitumie mashine za
kieletroniki za kukusanya kodi za efds ambavyo vyote ni makosa ya
jinai.
Mwisho.
Hakuna maoni :
Chapisha Maoni