Naibu Waziri wa Nishati na Madini (Madini), Charles Kitwanga
(kulia) akimsikiliza kwa makini Meneja Mradi Mkazi wa Kampuni ya Yakobsen
Elektro ya Norway inayojenga mtambo wa Kinyerezi I Markkli Repo ( wa pili
kutoka kushoto) mara baada ya kuwasili katika eneo la mtambo huo ili aweze
kuwaongoza wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwenye
ziara katika mitambo hiyo.
Meneja Miradi ya Kinyerezi Mhandisi Simon Jilima (kulia)
akielezea maendeleo ya ujezi wa mtambo wa Kinyerezi I mbele ya Naibu Waziri wa
Nishati na Madini (Madini), Charles Kitwanga (wa tano kutoka kulia), Kamati ya
Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini na wataalamu kutoka Wizara ya Nishati na
Madini.
Mbunge wa Lulindi- Masasi, Jerome Bwanausi (katikati)
akisisitiza jambo katika ziara hiyo. Kushoto ni Naibu Waziri wa Nishati na
Madini (Madini), Charles Kitwanga na kulia ni Meneja Miradi ya Kinyerezi
Mhandisi Simon Jilima.
Mkurugenzi wa Shirika la Umeme Nchini (Tanesco) Mhandisi
Felchesmi Mramba akielezea mikakati ya shirika la Tanesco kuboresha huduma za
umeme nchini kote.
Meneja Miradi ya Kinyerezi Mhandisi Simon Jilima amesema
kuwa mtambo wa Kinyerezi 1 unaojengwa na kampuni ya Yakobsen Elektro ya Norway
unatarajia kukamilika mapema Juni mwaka huu.
Mhandisi Jilima aliyasema hayo mbele ya Kamati ya Kudumu ya
Bunge ya Nishati na Madini iliyofanya ziara katika mtambo huo ili kujionea
maendeleo ya ujenzi wake. Kamati hiyo imeanza ziara ya kutembelea miradi ya
umeme iliyopo katika mikoa ya Dar es Salaam, Dodoma, Singida, Arusha na
Kilimanjaro pamoja na kuzungumza na wadau wa madini aina ya tanzanite katika
mkoa wa Manyara.
Mhandisi Jilima alisema kwa sasa mradi huo umekamilika kwa
asilimia 80 na kufafanua kazi inayofanyika kwa sasa ni kumalizia utandazaji wa
nyaya, ufungaji wa mabomba ya maji na gesi pamoja na ujenzi wa barabara za
ndani.
Alisema kuwa ofisi kwa ajili ya watumishi pamoja na karakana
kwa ajili ya kuhifadhia mitambo imekamilika.
Akielezea gharama za mradi huo Mhandisi Jilima alisema mpaka
sasa serikali imelipa kiasi cha Dola za Marekani milioni 167.2 na kuongeza kuwa
kiasi cha Dola za Marekani milioni 15 kinatarajiwa kumaliziwa kabla ya
kukamilika kwa mradi.
Akielezea changamoto katika utekelezaji wa mradi huo,
Mhandisi Jilima alieleza kuwa awali changamoto kubwa ilikuwa ni ukamilishwaji
wa mradi wa bomba la gesi ili waweze kutumia gesi hiyo katika kuzalisha umeme
lakini kutokana na kasi ya mradi huo kuwa ya kuridhisha wana imani kuwa gesi
itaanza kuzalishwa mapema kabla ya kukamilika kwa mtambo wa Kinyerezi 1
“ Ndugu wajumbe, awali tulikuwa na wasiwasi wa kupatikana kwa
gesi kwa ajili ya kuzalisha umeme kupitia mradi wa Kinyerezi 1 kutokana na
mradi wa bomba la gesi kuwa na changamoto nyingi, lakini baada ya kuona mradi
wa bomba la gesi uko katika hatua nzuri yaani zaidi ya asilimia 90, tunaamini
kuwa mara mtambo utapokamilika, gesi itakuwa imekwishaanza kuzalishwa na hapo
ndipo tutaanza kuzalisha umeme mara moja,” alieleza Mhandisi Jilima
Akielezea fidia kwa wakazi waliopisha ujenzi wa mradi huo,
Mhandisi Jilima alieleza kuwa mradi wa Kinyerezi I ulikwishafanya tahmini
pamoja na kulipa fidia kwa wakazi waliopisha ujenzi wa mtambo huo tangu mwaka
juzi.
Wakati huohuo wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Nishati na
Madini walipongeza hatua iliyofikiwa ya ujenzi wa mtambo huo na kuitaka
serikali kukamilisha malipo ya kiasi kilichobaki cha Dola za Marekani milioni
15 ili mradi huo uweze kukamilika kwa wakati.
Hakuna maoni :
Chapisha Maoni