.

.

.

.

.

.

.

.
KARIBUNI TUHABARIKE, TUELIMISHANE, TUPEANE HABARI ZA KUKUFANYA UTABASAMU KIDOGO NA MATUKIO YALIYOFANYIWA UCHUNGUZI WA KINA TOKA KILA PEMBE CONTACTS: +255 787 377 722 Email: drweyunga@gmail.com PIA UNAWEZA KUNI FOLLOW KUPITIA INSTAGRAM YANGU @drweyunga | TANGAZA NASI ILI UWAFIKIE WATU WENGI ZAIDI.

Alhamisi, 20 Agosti 2015

UMOJA WA MATAIFA WAANZA MAADHIMISHO YA MIAKA 70 KWA KUPANDA MIRTI HIFADHI YA MLIMA KILIMANJARO





Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mohamed Gharib Bilal amewaasa Watanzania hususan wakazi wa eneo la Hifadhi ya Mlima Kilimanjaro kufanya jitihada za makusudi kutunza maeneo yanayozunguka Mlima huo ili uendelee kuwa kivutio kikubwa cha utalii nchini kwa ajili ya maendeleo yao na kwa Taifa kwa ujumla.

 Hayo yamesemwa kwa niaba yake na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais-Mazingira, Mhe. Binilith Mahenge (Mb.) alipowasilisha hotuba wakati wa tukio la upandaji miti ambalo ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 70 ya Umoja wa Mataifa lililofanyika leo katika Hifadhi ya Mlima Kilimanjaro, Kijiji cha Marua, Mkoani Kilimanjaro.
 
 Mhe. Bilal alisema kuwa, Mlima Kilimanjaro ambao ni mrefu zaidi Afrika, unaosimama peke yake na wenye barafu kwa mwaka mzima pamoja na kwamba hali ya hewa ya Tanzania ni joto sana ni moja ya vivutio vikubwa vya utalii ambavyo vinachangia kwenye pato la taifa na hata kipato cha mwananchi mmoja mmoja kwa Kilimanjaro na maeneo yanayozunguka mkoa huo.
 
 “Nawaasa wazee wangu na wakazi wote wa Kilimanjaro kuwa na jitihada za makusudi kutunza maeneo yanayozunguka mlima huu na tusisubiri watu kutoka Dar es Salaam na maeneo mengine ya mbali kufanya kazi hiyo”, ilisisitiza sehemu ya hotuba ya Dkt. Bilal.
 
 Akizungumzia matukio kuelekea maadhimisho ya miaka 70 ya Umoja wa Mataifa ambayo yatafikia kilele tarehe 24 Oktoba mwaka huu, Mhe. Bilal alipongeza na kuwashukuru waandaji wa shughuli hiyo wakiongozwa na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Timu ya Umoja wa Mataifa hapa nchini na TANAPA kwa kuwekea msisitizo umuhimu wa kulinda na kutunza mazingira.
 
 Aliongeza kuwa japo hapo awali, Umoja wa Mataifa uliundwa kutokana na vita na mapigano yaliyojitokeza duniani miaka ya nyuma anafarijika kuona Umoja huo kwa sasa umebadilika na umekuwa ni chombo cha kupigania na kutetea haki za binadamu na utunzajia wa mazingira.
 
 “Nichukue fursa hii kupongeza Kaulimbiu ya Maadhimisho ya miaka 70 ya Umoja wa Mataifa inayosema “Umoja wa Mataifa wenye Nguvu, Dunia Bora” na ile kaulimbiu yetu ya hapa nchini inayosema:”Dunia Moja Watu Bilioni Saba; Kutunza Mazingira ni Wajibu Wetu”. Hivyo ni wajibu wa kila mmoja wetu kutunza mazingira ili kuhakikisha watu hao bilioni saba hawaangamii,” alisema Mhe. Dkt. Bilal.
 
 Mhe. Dkt. Bilal aliongeza kusema kuwa, wakati umoja wa Mataifa ukiadhimisha miaka 70 mwaka huu, pia utakuwa na matukio mengine matatu makubwa ambayo ni kuhitimisha utekelezajii wa Malengo ya Milenia, Kupitishwa kwa agenda mpya ya Maendeleo Endelevu baada ya mwaka 2015 na kupitishwa kwa mkataba mpya wa Mambadiliko ya Tabianchi utakaorithi Itifaki ya sasa ya Kyoto.
 
 Awali akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Mhe. Leonidas Gama, Mkuu wa Wilaya ya Moshi Vijijini, Mhe. Novatus Makunga alisema kuwa Mkoa huo umejitahidi kuchukua hatua mbalimbali za kukabiliana na uharibifu wa mazingira ya Hifadhi ya Mlima Kilimanjaro ikiwemo kusitisha vibali vya uvunaji wa miti ya mbao na kuni; kuhimiza matumizi ya nishati mbabadala kwenye taasisi za shule, vyuo na magereza; kuhamasisha wananchi kupanda miti kwenye vyanzo vya maji pamoja na kuhifadhi misitu ya asili.”Tunapongeza Taasisi zote zilizoamua kuchagua Mkoa wetu kwa maadhimisho haya ya upandaji miti kwani yameongeza uelewa na ari kwa wananchi kuwa utunzaji mazingira ni jukumu la kila mmoja wetu”, alisema Mhe. Gama.
 
 Naye Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo ya Umoja wa Mataifa (UNDP) nchini, Bw. Alvaro Rodriguez alisema kuwa Umoja wa Mataifa unajivunia miaka 70 ya mafanikio katika kukabiliana na changmoto mbalimbali zinazoikabili duniani kama vita, uharibifu wa mazingira, ukiukwaji wa haki za binadamu na kwamba maadhimisho hayo ni fursa ya kutathmini mafanikio hayo na kuongeza juhudi zaidi katika kukabiliana na changamoto hizo ili kuzimaliza kabisa.
 
 Aliongeza kuwa Umoja huo utaendelea kushirikiana kwa karibu na Tanzania ili kuiwezesha kufikia malengo ya maendeleo na kutoa wito kwa Serikali kuridhia Malengo mapya ya maendeleo endelevu.
 
 Kwa upande wake Kiongozi wa Mabalozi wa Umoja wa Ulaya nchini, Mhe. Filberto Ceriani Sebregondi alisema kuwa Umoja huo utaendelea kusaidia miradi mbalimbali ya maendeleo nchini ikiwemo ile ya utunzaji misitu, maji na kilimo pamoja na kuimarisha wakala mbalimbali za taifa ili kweza kukabiliana na Mabadiliko ya tabianchi.
 
 Tukio hilo la upandaji miti ambalo ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 70 ya Umoja wa Mataifa ambayo yatafikia kilele tarehe 24 Oktoba, 2015, lilihudhuriwa na Watendaji kutoka Serikalini akiwemo Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Balozi Celestine Mushy, Mabalozi na Wawakilishi wa Mashirika ya Kimataifa na Wananchi.


Hakuna maoni :

Chapisha Maoni