.

.

.

.

.

.

.

.
KARIBUNI TUHABARIKE, TUELIMISHANE, TUPEANE HABARI ZA KUKUFANYA UTABASAMU KIDOGO NA MATUKIO YALIYOFANYIWA UCHUNGUZI WA KINA TOKA KILA PEMBE CONTACTS: +255 787 377 722 Email: drweyunga@gmail.com PIA UNAWEZA KUNI FOLLOW KUPITIA INSTAGRAM YANGU @drweyunga | TANGAZA NASI ILI UWAFIKIE WATU WENGI ZAIDI.

Ijumaa, 29 Januari 2016

TAARIFA YA THBUB KWA VYOMBO VYA HABARI

TUME ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB) imepokea taarifa ya tarehe 27 Januari, 2016 kutoka Bungeni kuhusu uamuzi wa Serikali kupunguza matangazo ya moja kwa moja (Live) ya vikao vya Bunge kupitia Televisheni ya Taifa (TBC). Tume inafanyia uchambuzi taarifa hizo ili kuona kama uamuzi huo hautaingilia haki ya wananchi kupata habari chini ya Ibara ya 18(d), ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977.

Aidha Tume imesikitishwa na vurugu zilizotokea Bungeni baada ya uamuzi huo kutolewa ambapo zilisababisha askari wa kutuliza ghasia (FFU) kuingia ndani ya ukumbi wa Bunge.

Ibara ya 63(2) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ya mwaka 1977 inatamka kuwa, “ ...Bunge... ndicho chombo kikuu cha Jamhuri ya Muungano ambacho kitakuwa na madaraka, kwa niaba ya Wananchi, kusimamia na kuishauri Serikali ya Jamhuri ya Muungano na vyombo vyake vyote katika utekelezaji wa majukumu yake kwa mujibu wa Katiba hii”.

Mantiki ya Ibara hii ni kwamba Bunge ni muhimili wa kitaifa unaowakilisha wananchi kuisimamia na kuishauri Serikali (executive) na vyombo vyake katika kutekeleza majukumu yake (executive) na si kinyume chake.

Tume inaamini kwamba vurugu siyo njia sahihi ya kupata muafaka wa mambo ambayo Waheshimiwa Wabunge hawakubaliani nayo.

Aidha, Tume inatamka kwamba kitendo cha askari wa kikosi cha FFU kuingia bungeni kuwatoa Wabunge waliokuwa wakifanya vurugu ni kitendo kilichodhalilisha Bunge kama muhimili muhimu wa Taifa na ni kitendo cha aibu kwa Taifa.

Mwisho, Tume inatoa rai kwa uongozi wa Bunge na Wabunge wote kuzingatia kanuni za Bunge katika kutekeleza shughuli za Bunge.

Bahame Tom Nyanduga
Mwenyekiti
TUME YA HAKI ZA BINADAMU NA UTAWALA BORA
Januari 29, 2016

Hakuna maoni :

Chapisha Maoni