Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
Balozi Seif Ali Iddi akizungumza na Waandishi wa Habari hawapo
pichani hapo uwanja wa ndege wa Pemba kabla ya kurejea Unguja baada
ya kumaliza ziara ya Siku Tatu Kisiwani Pemba. Kulia ya Balozi Seif
ni Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi Zanzibar Nd. Vuai Ali
Vuai na Kushoto ya Balozi Seif ni Spika wa Baraza la Wawakilishi
Zanzibar Mh. Panadu Ameir Kificho.
Balozi Seif akijibubaadhi ya maswali
ya Waandishi wa Habari alipokutana nao uwanja wa ndege wa Pemba
baada ya kukamilisha ziara yake ya siku Tatu Kisiwani humo. Kushoto
ya Balozi Seif ni Spika wa Baraza la Wawakilishi Mh. Pandu Ameir
Kificho, Mkuu wa Mkoa wa Kusini Pemba Mh. Mwanajuma Majid na Mjumbe
wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM Dr. Maua Daftari. Picha na –
OMPR – ZNZ.
Press Release:-
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
Balozi Seif Ali Iddi alisema kwa vile Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar
imeshatangaza Tarehe ya Kurejewa kwa Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar yeye
binafsi haoni umuhimu wa kurejewa kwa mazungumzo kati ya Katibu Mkuu
wa CUF Maalim Seif Sharif Hamad na Rais wa Zanzibar Dr. Ali Mohammed
Shein .
Alisema mazungumzo hayo kwa sasa
hayana tija yoyote kwa vile Wananchi katika kipindi hichi wameanza
kujiweka tayari wakijiandaa kupiga kura kufuatia Tume ya Uchaguzi ya
Zanzibar { ZEC } kufuta matokeo ya uchaguzi Tarehe 28 Oktoba mwaka
2015.
Akizungumza na Waandishi wa Habari
kwenye Uwanja wa ndege wa Pemba akijiandaa kurejea Kisiwani Unguja
baada ya kumaliza ziara yake ya siku Tatu Kisiwani Pemba kukagua
shughuli mbali mbali za Maendeleo akiwa Mtendaji Mkuu wa Serikali
Balozi Seif Ali Iddi alisema iwapo yapo malalamiko yoyote muhusika
wake ana wajibu wa kwenda Mahakamani kwa hivi sasa.
Balozi Seif alisema mazungumzo ya
pamoja kati ya Rais wa Zanzibar na Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi
{CUF } Maalim Seif Sharif Hamad kuhusu kufutwa kwa Uchaguzi Mkuu
yalifanyika kwa maombi ya Maalim Seif ambae yeye binafsi ndie
aliyeamua kujiondoka kwenye maendeleo ya vikao vya mazungumzo hayo.
Alisema kinacholikabili Taifa kwa
wakati huu ni suala la marejeo ya uchaguzi na kuwaomba watu walioamua
kutoshiriki uchaguzi huo wa marudio ni vyema wakabakia nyumbani ili
kutoa fursa kwa wenzao waliokubali kushiriki watumie haki yao ya
Kidemokrasia kuwachaguwa Viongozi wanaowataka.
Balozi Seif alifahamisha kwamba hata
yeye anaheshimu maamuzi ya Tume ya Uchaguzi ya Z anzibar ambayo
haiwezi kuingiliwa na chombo chochote licha ya kwamba Tayari alikuwa
ameshashinda na kupewa cheti kinachothibitisha kuwa Mwakilishi wa
Jimbo la Mahonda.
“ Tupo tuliokwishashinda kwenye
chaguzi zetu za Majimbo na kupewa vyeti vinavyothibisha ushindi huo
lakini baadhi yetu kwa nini tuendelee kushutumu maamuzi ya tume
ambayo kutokana na sababu za msingi ilizoeleza za kujitokeza kwa
dosari kadhaa kwenye zoezi zima ikalazimika kufuta matokeo na
uchaguzi wote ? ”. Aliuliza Balozi Seif.
Akizungumzia uvumi uliojitokeza wa
kuwepo kikundi cha Vijana wanaopiga watu katika badhi ya maeneo
maarufu Mazombi Balozi Seif alisema hana taarifa yoyote iliyomfikia
akiwa kama Kiongozi wa Juu wa Serikali kuhusu shutma hizo.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
alitoa agizo kwa vyombo vya Ulinzi kufanya uchunguzi dhidi ya shutuma
hizo na pale itakapobainika kuwepo kwa shutma hizo vifanye juhudi ya
kuwakamata wahusika hao na kuwafikisha mbele ya Doli ili sheria
ichukuwe mkondo wake.
Balozi Seif alieleza kwamba nia ya
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Ile ya Jamuhuri ya Mauungano wa
Tanzania ni kuiona nchi inaendelea kubakia katika hali ya amani na
utulivu wakati wote kabla na baada ya uchaguzi.
Aliwaasa na kuwaomba Wananchi wa
maeneo mbali mbali Kisiwani Pemba kuendelea kuishi kwa amani na
upendo na kushirikiana katika mambo yao bila ya kuendekeza zaidi
itikadi zao za Kisiasa ambazo tayari zimeshaonyesha muelekeo mbaya.
Alieleza kwamba matokeo ya sasa
yaliyojichomoza katika hujuma za moto sambamba na baadhi ya watu
kuanza kuashiria vitisho dhidi ya wananchi wenzao walioamua kushiriki
uchaguzi wa marejeo kwa kuwatilia X nyumba zao yanaonyesha safari ya
hatari katika maisha miongoni mwa jamii.
Hakuna maoni :
Chapisha Maoni