Na Lorietha Laurence-WHUSM
Waziri wa Habari ,Utamaduni,Sanaa na Michezo Mhe.Nape Mosses Nnauye amewataka waandishi wa habari kuwa wazalendo kwa kuandika habari za maendeleo ya bara la Afrika.
Hayo ameyasema leo jijini Dar es Salaam wakati wa ufunguzi wa mkutano wa China-Afrika Public Diplomacy Forum na kueleza kuwa uhusiano baina ya Afrika na China ni wa muda mrefu na umejikita katika kuboresha teknolojia ya mawasiliano na hivyo kukuza uchumi wake.
Aidha aliongeza kuwa ili bara la Afrika liweze kuelezea historia yake kwa mataifa mingine katika kujiletea maendeleo kuna haja ya kuvijengea uwezo vyombo vya habari katika kutoa habari nzuri zenye manufaa kwa jamii husika.
“Katika karne hii tuliyopo sasa kuna mabadiliko mengi ya teknolojia hivyo ni budi kuendelea kuimarisha ushirikiano ulipo baina ya China na Afrika ili kuleta maendeleo chanya kwa jamii zetu kupitia vyombo vya habari huku tukitunza na kueneza tamaduni zetu” alisema Mhe.Nape.
Waziri Nape alizidi kufafanua kuwa vyombo vya habari katika nchi za bara la Afrika vina uwezo mkubwa wa kukuza na kueneza utamaduni, kuhudumia jamii,kujenga umoja wa kitaifa na kulinda maslahi ya jamii duniani.
Naye Rais wa China Public Diplomacy Association Bw. Li Zhaoxing amesema kuwa anafurahishwa na uhusiano uonaozidi kuimarika baina ya nchi za Afrika na China na kuahidi kuboresha mawasiliano na mahusiano ili kufikia mafanikio makubwa yaliyokusudiwa.
Mkutano wa China-Afrika Public Diplomacy Forum umejikita katika kujadili mambo mbalimbali ikiwemo mahusiano baina ya mtu na mtu na Vyombo vya habari,afya,na tiba asilia.
Hakuna maoni :
Chapisha Maoni