.

.

.

.

.

.

.

.
KARIBUNI TUHABARIKE, TUELIMISHANE, TUPEANE HABARI ZA KUKUFANYA UTABASAMU KIDOGO NA MATUKIO YALIYOFANYIWA UCHUNGUZI WA KINA TOKA KILA PEMBE CONTACTS: +255 787 377 722 Email: drweyunga@gmail.com PIA UNAWEZA KUNI FOLLOW KUPITIA INSTAGRAM YANGU @drweyunga | TANGAZA NASI ILI UWAFIKIE WATU WENGI ZAIDI.

Ijumaa, 26 Mei 2017

CCM YAMPONGEZA JPM SAKATA LA MCHANGA WA MADINI, YALAANI VIKALI MAUAJI MKOANI PWANI

Katibu wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi CCM, Itikadi na Uenezi Ndg Humprey Polepole akizungumza na Waandishi wa Habari katika ukumbi wa Mikutano Ofisi ndogo ya CCM Lumumba Jijini Dar es salaam. 

Picha Zote na Mathias CanalNa Mathias Canal, Dar es salaam

Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt John Pombe Magufuli ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM Taifa kwa kutekeleza sera na kuisimamia ilani ya ushindi ya CCM ya mwaka 2015/2020 na kuwaomba watanzania wote kwa kauli moja pasina itikadi za vyama kumuunga mkono kwani atakuwa imara na madhubuti zaidi katika utendaji wake iwapo ataungwa mkono na watanzania wote.

Chama cha Mapinduzi (CCM) Kimetoa pongezi hizo kutokana na maamuzi yaliyofanywa na Rais Magufuli mara baada ya kupokea Ripoti ya kamati iliyokuwa inachunguza Hatma ya mchanga wa madini iliyoundwa na Rais Magufuli Machi 29 mwaka huu ikiwajumuisha Profesa Abdulkarim Hamisi Mruma (Mwenyekiti), Profesa Justiania Rwezaura Ikingula, Profesa Joseph Bushweshaiga, Dokta Yusuph Ngenya, Dokta Joseph Yoweza Phili, Dokta Ambrose Itika, Mohamed Zengo Makongoro na Hery Issa Gombela.

Kauli hiyo imetolewa na Katibu wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi CCM, Itikadi na Uenezi Ndg Humprey Polepole wakati akizungumza na Waandishi wa Habari katika ukumbi wa Mikutano Ofisi ndogo ya CCM Lumumba Jijini Dar es salaam.

Polepole alisema kuwa uamuzi wa kuundwa kwa kamati hiyo ulitokana na kukamatwa kwa makontena 277 ya mchanga huo katika bandari ya Dar es salaam Machi 23 Mwaka huu baada ya Rais kufanya ziara ya kushitukiza katika bandari hiyo na kukuta makontena 20 yakiwa mbioni kusafirishwa kinyume cha maelekezo yake ya Machi 2 ya kuzuia kusafirisha mchanga huo nje ya nchi.

Alisema kuwa huu sio wakati wa kulumbana na kutofautiana kisa itikadi za vyama bali ni wakati wa kusimama pamoja na kuikabili vita ya kiuchumi kwani kwa kuzingatia taarifa iliyosomwa na Profesa Mruma mbele ya Rais Magufuli imebainisha jinsi Taifa lilivyopata hasara ya mabilioni ya fedha kwa kuwa makontena yaliyozuiliwa bandarini yana thamani ya madini yaliyomo kwa kiwango cha wastani wa shilingi Bilioni 829.4 na kiwango cha juu ni Shilingi Trioni 1.4

"Tumeibiwa na kudhulumiwa sana mali zetu ambazo tumezirithi kutoka kwa babu zetu lakini awamu ya Tano ikiongozwa na Rais Magufuli imeamua kwa dhati kabisa kutilia mkazo Vita dhidi ya Rushwa, Uhujumu uchumi, Udhalimu wa kila namna, sambamba na wizi na ufisadi kwa maslahi mapana ya Taifa la Tanzania na Watanzania wote" Alisema Polepole

Akizungumzia Mauaji yanayotokea katika maeneo mbalimbali nchini hususani Mkoani Pwani katika Wilaya ya Kibiti, Rufiji na Mkuranga alisema kuwa kipindi hiki kigumu kwa kuwapoteza ndugu zetu vyama vya siasa vilipaswa kushikamana kwa pamoja pasina kujali itikadi zao badala yake vimeanza kutumia misiba hiyo kwa maslahi ya kiuongozi kuliko maslahi ya Taifa.
Polepole alisema kuwa vyombo vyote vya serikali vinavyoshughulikia ulinzi vinapaswa kutumia Rasilimali zao, Weledi na Utendaji wao, na kuweka umaalumu katika kuyakabili matukio ya mauaji na kuyakomesha kabisa.
 

"Hakuna dini yoyote Duniani inayoamini katika kutoa uhai wa mtu ambapo pia kuua mtu ni kinyume na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hivyo Tunataka amani ya wananchi wetu inarudi"
 
"Tunatambua kuwa wananchi wetu wanapita katika wakati mgumu kutokana na kukatishwa kinyama maisha ya Wananchi wenzao, Viongozi, Askari, Watendaji wa serikali, Wanachama wa CCM si kwa sababu ya mapenzi ya Mungu Bali kwa sababu yamekatishwa katika namna inayokiuka ubinadamu kwa kuuawa kikatili na watu wasio na Utu, Hisia na Imani ya Dini" Alisema Polepole
 
Polepole ametilia msisitizo wananchi kutoa taarifa kwa jeshi la Polisi kuhusu watu wanaofanya mauaji hayo kwani ushirikiano huo utasaidia kufichua uovu wa wadhalimu wanaokatisha maisha ya watanzania.
Katibu wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi CCM, Itikadi na Uenezi Ndg Humprey Polepole akisisitiza jambo wakati akizungumza na Waandishi wa Habari katika ukumbi wa Mikutano Ofisi ndogo ya CCM Lumumba Jijini Dar es salaam.

Waandishi wa habari wakimsikiliza Katibu wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi CCM, Itikadi na Uenezi Ndg Humprey Polepole wakati wa Mkutano wake na Waandishi wa Habari katika ukumbi wa Mikutano Ofisi ndogo ya CCM Lumumba Jijini Dar es salaam.
Katibu wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi CCM, Itikadi na Uenezi Ndg Humprey Polepole akizungumza na Waandishi wa Habari katika ukumbi wa Mikutano Ofisi ndogo ya CCM Lumumba Jijini Dar es salaam.

Hakuna maoni :

Chapisha Maoni