Mazungumzo ya kutafuta amani nchini
Sudani Kusini, hatimaye jana yamemalizika, baada ya pande zote mbili
zinazokinzana kukubali kusaini makubaliano zaidi ya 40 waliojiwekea
jijini Arusha.
Baadhi ya makubaliano hayo ni pamoja
na kufanyia marekebisho katiba ya chama, kupunguza madaraka ya raisi,
kuongeza idadi ya wajumbe katika kamati kuu ya chama, kukubali
kuwajibika wote kwa yote yaliotokea na kuwaomba msamaha wananchi wa
Sudani Kusini kwa kuwasababishia
machafuko na vita.
Mengine ni pamoja na haki ya kila
mwanachama kugombea uongozi, kuleta mabadiliko ya kidemokrasia katika
chama, utawala bora na uwazi katika chama na kutumia makubaliano ya
Arusha kuharakisha mazungumzo ya Adis Ababa.
Akisoma makubaliano hayo mara baada
ya kusaini pande hizo zinazokinzana, Katibu Mkuu wa Chama cha
Mapinduzi (CCM) Abdulraham Kinana, amewaomba kutimiza kwa dhati
maazimio waliojiwekea na kuyatekeleza kwa faida ya nchi yao.
Naye Rais wa Tanzania Jakaya
Kikwete, ameungana na wenzake kadhaa katika kushuhudia tukio la
kihistoria la utilianaji sahihi ya makubaliano ya amani na kusitisha
mapigano katika nchi mpya ya Sudan Kusini.
Amesema ni vema wahusika wa mapigano
hayo wakatimiza maazimio waliojiweka kwa utekelezaji na kuwapongeza
kwa uamuzi wa kukubali kusaini makubaliano hayo na kuwataka
wayatimize ili kurahisisha utendaji wao wa kazi.
Kikwete amesema kila kiongozi kabla
ya kufanya kitu ni lazima atafakari mara mbili jambo lolote analotaka
kufanya, kuwa lina faida kwa wananchi wa nchi hiyo au la.
Naye Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta,
amewapongeza sana kwa kukubali kusaini makubaliano hayo na
kuwakaribisha kwake pale watakapohitaji msaada wowote kwa ajili ya
kuharakisha maendeleo ya nchi hiyo.
Rais wa Uganda Yoweri Museveni, naye
ameungana na wenzake kuwapongeza kwa kufikia hatua hiyo na kusema
nchi hiyo ndugu wa karibu na Uganda na hivyo imekuwa furaha kuona
sasa wanakwenda kutulia bila mapigano.
Baada ya hatuba hizo za wosia kwa
wapinzani hao ndani ya chama kimoja, Rais Salva Kiir Mayardit na
Mpinzani wake, Riek Machar ambaye ndiye aliyekuwa makamu wa Rais
kabla ya mtafaruku, walionekana wenye furaha muda wote na kupongezana
kwa kupeana mikono mara kwa mara, huku
wakishangiliwa na wapambe wao
waliofurika ndani ya ukumbi wa Ngurudoto, Jijini Arusha.
Wakinzani hao wote kwa pamoja
wameahidi kutimiza kwa vitendo makubaliano hayo na kupeana
ushirikiano katika mambo yote na kuwashukuru wote waliohusika
kusuluhisha ugomvi huo hadi kufikia hatua hiyo.
Viongozi wengine walioshuhudia
makubaliano ya amani kwa Sudani Kusini ni pamoja na Makamu wa Rais,
Mohammed Gharib Bilal, Makamu wa Rais wa Afrika Kusini Cyril
Ramaphosa na mjane wa kiongozi wa kwanza wa chama cha SPLM John
Garang, ambaye ndiye aliyeongoza harakati za
kupigania uhuru, kuelekea kujitenga
kwa nchi hiyo, kutoka kwa iliyokuwa Jamhuri ya Sudan.
Katika vita hivyo zaidi ya watu
20,000 wamepoteza maisha katika mapigano yaliyozuka Sudani Kusini
mara baada ya nchi hiyo kujitenga na iliyokuwa Jamhuri ya Sudan mwaka
2011 na wananchi zaidi ya milioni moja hawana makazi ya kuishi
sababu ya vita hivyo.
Mazungumzo ya awali ya vikundi
vinavyozozana katika chama cha SPLM cha Sudan Kusini, yaliongozwa na
ujumbe mzito wa ngazi ya Juu wa Chama cha Mapinduzi ( CCM), ili
kutafuta suluhu ya mgogoro ndani ya chama cha hicho kinachotawala
nchini Sudani Kusini.
Ujumbe huo uliongozwa na Makamu
Mwenyekiti Mstaafu wa CCM Balozi John Samwel Malecela, Makamu
Mwenyekiti wa CCM Tanzania Bara Philip Mangula na Katibu Mkuu wa
Chama hicho Abdulraham Kinana.
Kwa upande wa SPLM, mazungumzo hayo
yaliongozwa na Taban Deng Gai,Daniel
Awet Akot, na Deng Alor Kuol.
Miongoni mwa makundi hayo ni kutoka
chama cha SPLM, Kundi kutoka kwa wafungwa wa kisiasa, pamoja na
kundi lililojitenga kutoka chama cha SPLM.
Chama hicho kiligawanyika makundi
matatu na kusababisha jeshi kwa upande wake, kumeguka katika makundi
hayo na kusababisha wananchi nao kugawanyika katika makundi hayo
matatu .
Mazungumzo hayo pia yalihudhuriwa na
wawakilishi kutoka EU, AU,Norway Egypt,Umoja wa Mataifa na Ethiopia.
Mwisho

Hakuna maoni :
Chapisha Maoni