.

.

.

.

.

.

.

.
KARIBUNI TUHABARIKE, TUELIMISHANE, TUPEANE HABARI ZA KUKUFANYA UTABASAMU KIDOGO NA MATUKIO YALIYOFANYIWA UCHUNGUZI WA KINA TOKA KILA PEMBE CONTACTS: +255 787 377 722 Email: drweyunga@gmail.com PIA UNAWEZA KUNI FOLLOW KUPITIA INSTAGRAM YANGU @drweyunga | TANGAZA NASI ILI UWAFIKIE WATU WENGI ZAIDI.

Alhamisi, 19 Aprili 2018

NGORONGORO HEROES KUWAFUATA DR CONGO,MAMLAKA YA HIFADHI YA NGORONGORO WAJITOKEZA KUIDHAMINI

Kikosi cha Wachezaji 21 na Viongozi 7 wa Timu ya Taifa ya Vijana chini ya miaka 20 Ngorongoro Heroes wanatarajia kuondoka usiku kuelekea DR Congo kwenye mchezo wao wa marudiano wa kufuzu fainali za Africa kwa Vijana dhidi ya Timu ya taifa ya Vijana ya DR Congo safari iliyodhaminiwa na Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro.

Ngorongoro Heroes inaondoka kwa kutumia Shirika la Ndege la Ethiopia ambapo kesho wanatarajia kufanya mazoezi kuelekea mchezo huo utakaochezwa Jumapili Aprili 22,2018.

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania(TFF) tunaishukuru Mamlaka Ya Hifadhi ya Ngorongoro kwa kujitokeza na kuidhamini timu yetu ya Taifa ya Vijana chini ya miaka 20 Ngorongoro Heroes jambo lililotupa faraja kubwa.

TFF imekuwa na mzigo mkubwa wa kuzihudumia timu za Taifa ambao imekuwa ikiubeba na Taasisi kama Mamlaka ya Ngorongoro inapojitokeza kutusaidia kupunguza mzigo huo ni jambo la faraja na jambo la kushukuru.

Bado tunaziomba Taasisi mbalimbali na Makampuni kuweza kujitokeza kudhamini timu zetu za Taifa na mashindano mbalimbali yaliyo chini ya TFF.

Wadhamini wa Safari hiyo ya Ngorongoro Heroes Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro kupitia kwa Kaimu Meneja wa Uhusiano Joyce Mgaya wamesema ni faraja kubwa kwao kuwa sehemu ya timu ya Ngorongoro ambayo wanaamini itafanya vizuri.

Bi Mgaya amesema huo ni mwanzo mwema kwao katika mahusiano hayo mapya na TFF kupitia timu hiyo ya Ngorongoro Heroes iliyobeba pia jina la Mamlaka yao ya Hifadhi.

“Tunaishukuru TFF katika mahusiano haya mapya ambayo yatatufanya na sisi kutoa mchango wetu katika timu hii ya Vijana ambao tunahakika wanakwenda kufanya vizuri katika mchezo huo na huu ni mwanzo tu kwa upande wetu” alisema Mgaya.

Naye Kocha Mkuu wa Ngorongoro Heroes Ammy Ninje amesema maandalizi yanaridhisha na vijana wamepokea vyema mafundisho yake ikiwemo mfumo mpya wa namna ya kucheza na DR Congo ugenini.

Ninje amesema wanafahamu kazi iliyopo mbele yao lakini kwa maandalizi yaliyofanyika imani ni kubwa ya kufanya vizuri wakichagizwa na udhamini wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro ambao wamejitokeza kuisafirisha timu hiyo jambo ambalo linawatia nguvu zaidi.

Nahodha wa kikosi hicho Issa Makamba amesema wachezaji wako tayari kwenda kuwakilisha vyema na wametiwa hamasa kubwa zaidi na morali kutoka kwa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro.

Amesema wao vijana kazi yao ni moja kufanya vizuri kwenye mchezo huo kwa kupata matokeo yatakayowapeleka kwenye hatua ya raundi ya pili.

RAIS WA TFF WALLACE KARIA AIPONGEZA YOUNG AFRICANS KUTINGA MAKUNDI KOMBE LA SHIRIKISHO BARANI AFRICA

Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania TFF Ndugu Wallace Karia ameipongeza klabu ya Young Africans kwa kufanikiwa kuingia kwenye hatua ya Makundi Kombe la Shirikisho Barani Africa.

Young Africans imefanikiwa kuingia kwenye hatua hiyo kwa ushindi wa jumla ya mabao 2-1 baada ya kushinda mchezo wao wa kwanza kwa mabao 2-0 kabla ya kufungwa bao 1-0 na timu ya Welaitta Dicha ya Ethiopia.

Rais wa TFF Ndugu Karia kwa niaba ya TFF ameipongeza klabu ya Young Africans kwa hatua hiyo kubwa iliyofikia ambayo inaakisi mpira wa Tanzania kiujumla.

“Mafanikio ya klabu ya Young Africans ni mafanikio ya Tanzania kiujumla na TFF ambao ni wasimamizi wa Mpira nchini tunajivunia mafanikio hayo ya Young Africans ambao tumekuwa tunashirikiana nao bega kwa bega kuhakikisha wanapeperusha vyema bendera ya Tanzania”amesema Karia.

Amesema anaamini watafanya maandalizi ya kutosha kuhakikisha wanafanya vizuri kwenye hatua hiyo ya makundi.

IMETOLEWA NA SHIRIKISHO LA MPIRA WA MIGUU TANZANIA TFF

Hakuna maoni :

Chapisha Maoni