.

.

.

.

.

.

.

.
KARIBUNI TUHABARIKE, TUELIMISHANE, TUPEANE HABARI ZA KUKUFANYA UTABASAMU KIDOGO NA MATUKIO YALIYOFANYIWA UCHUNGUZI WA KINA TOKA KILA PEMBE CONTACTS: +255 787 377 722 Email: drweyunga@gmail.com PIA UNAWEZA KUNI FOLLOW KUPITIA INSTAGRAM YANGU @drweyunga | TANGAZA NASI ILI UWAFIKIE WATU WENGI ZAIDI.

Alhamisi, 4 Desemba 2014

MUAFAKA WAFIKIWA BAINA YA MWEKEZAJI WA HOTELI YA KIMATAIFA YA SEA CLIFF ILIYOPO KATIKA KIJIJI CHA KAMA

Katibu wa Kamati ya Bandari ya Nyanjale Kiomba Mvua Bwana Moh’d Ali akitia saini makubaliano yaliyofikiwa baina ya Wanakijiji hicho na Uongozi wa Hoteli ya Kimataifa ya Sea Cliff iliyopo Kama nje kidogo ya Mji wa Zanzibar. Waliosimamanyuma yake wakishuhudia tukio hilo kutoka kulia ni Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kaskazini Unguja Nd. Haji Juma Haji, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi, Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Unguja Kana Mstaafu Juma Kassim Tindwa, Mwakilishi wa Jimbo la Kitope Mh. Makame Mshimba Mbarouk, Mwanasheria wa Makamu wa Pili Bibi Mwanaisha Shamte,Menaja Mkuu wa Sea Cliff Bwana Abre Esterhuizen na Mwanasheria wa Wizara ya Ardhi Nd, Khamis Faraji.
Wajumbe wawili wa Kamati ya Bandari ya Kiomba Mvua Bwana Othman Ashkina na Bibi Chiku Sheikh wakimwaga wino kwenye maridhiano waliyofikia na Hoteli ya Sea Cliff.Wajumbe hao wanashuhudiwa nyuma na Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Unguja. Kanal Mstaafu Juma Kassim Tindwa, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kaskazini Unguja Nd. Haji Juma Haji na Afisa Tawala Wil;aya ya Kaskazini B Nd. Juma Abdulla.
NI Sheha wa Shehia ya Kiomba Mvua Bwana Mzee Ramadhan Mzee akitia saini kama shahidi Makubaliano ya maridhiano kati ya Wananchi wa Kiomba Mvua na Uongozi wa Hoteli ya Sea Cliff.
Zamu ya Meneja Mkuu wa Hoteli ya Sea Cliff Bwana Abre Esterhuizen akimwaga wino kwenye maridhiano hayo ya makubaliano na wana Kijiji cha Kiomba Mvua.
Menaja Utawala na Uendeshaji wa Hoteli ya Sea Cliff Bwana Abdulmalik Mussa Kushoto na Meneja wa Mchezo wa Golf wa Hoteli hiyo Bwana Heirz Papenfus wakijumuika kutia saini Mkataba huop wa maridhiano.
 
Balozi Seif akishuhudiwa na Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Unguja Kanal Mstaafu Juma Kassim Tindwa Kulia yake na Mwenyekiti wa CCM wa Mkoa huo kushoto yake Nd. Haji Juma Haji chini ya usimamizi wa Mwanasheria wa Makamu wa Pili aliyesimama Bibi Mwanaisha Shamte akitia saini kama shahidi kwenye mkataba wa maridhiano hayo.
Balozi Seif akimpongeza Katibu wa Kamati ya Bandari ya Nyanjale Kiomba Mvua Bwana Moh’d Ali mara baada ya kumalizika kwa zoezi la utiaji saini mkataba wa maridhiano kati ya Uongozi wa Hoteli ya Sea Cliff na Wana Kijiji wa Kiomba Mvua.

Picha na Hassan Issa wa – OMPR – ZNZ.

Press Release:-

Hatma njema ya Kikao Maalum kilichotayarishwa kwa ajili ya utiaji saini makubaliano baina ya Muwekezaji wa Hoteli ya Kimataifa ya Sea Cliff iliyopo katika Kijiji cha Kama na Wananchi wanayoizunguuka Hoteli hiyo imefikiwa.

Utiaji saini makubaliano hayo ulikuwa ufanyike Tarehe 10 Mwezi Mei Mwaka huu lakini ulishindikana baada ya uamuzi wa wajumbe wa upande wa Kamati ya Bandari ya Nyanjale Kiomba Mvua kutokufika katika kikao hicho bila ya sababu zisizoeleweka.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akiwa pamoja na baadhi ya Viongozi wa Mkoa wa Kaskazini Unguja, Taasisi za Ardhi na Mazingira walishuhudia utiaji saini huo ambapo upande wa Hoteli ya Sea Cliff uliwakilishwa na Meneja Mkuu wa Hoteli hiyo Bwana Abre Esterhuizen,Meneja wa Mradi wa Mchezo wa Golf wa Hoteli hiyo Bwana Heirz Papenfus pamoja na Meneja Utawala na Uendeshaji wa Hoteli Bwana Abdullmalik Mussa.

Upande wa wana kijiji cha Kiomba Mvua ukaongozwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Bandari ya eneo hilo Nd. Mbwana Amour Khamis, Katibu wa Kamati hiyo Nd. Moh’d Ali Ameir pamoja na wajumbe wawili Bibi Chiku Sheikh Nd. Othman Ashkina.

Hafla hiyo ya utiaji saini Mkataba huo wa makubaliano ilifanyika katika ukumbi wa Hoteli hiyo ya Kimataifa ya Sea Cliff iliyopo Kama kilomita chache kaskazini ya Mji wa Zanzibar.

Mgogoro baina ya Muwekezaji huyo na Wananchi wa Vijiji jirani ambao ulihusu zaidi eneo la Bandari ya Madagaa pamoja na bara bara iendayo eneo hilo ulifikia makubaliano kufuatia vikao mbali mbali vilivyokuwa vikiendelea katika kutafuta maridhiano ya pande zote mbili.

Vikao vya pamoja kati ya Uongozi wa Hoteli ya Sea Cliff na Viongozi wa Kamati Nne za Vijiji vya Kiomba mvua vilikuwa vikifanyika kwa pamoja kupitia muongozo ulitolewa na Kamati ya Baraza la Wawakilishi kuhusu maridhiano ya pande hizo husika.

Mazingira halisi ya mgogoro wa Kiomba mvua na Muwekezaji wa Sea Cliff umefikia hatua nzuri ya maridhiano lakini kilichokuwa kikionekana wakati wa kufikia hatma yake ya mwisho ni baadhi ya watu kuanza kuhusisha mgogoro huo na masuala ya Kisiasa.

Akizungumza kwenye Kikao hicho Mwakilishi wa Mradi wa Hoteli ya Sea Cliff Bwana Yassir De Costa ameishukuru na kuipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa jitihada zake inazochukuwa katika kuunga mkono Taasisi za uwekezaji vitega uchumi hapa nchini.

De Costa alisema katika muelekeo wa kusaidia maendeleo ya wananchi wa vijiji vya jirani, Mradi wa Hoteli ya Sea Cliff umeamua kusaidia utunzaji wa mazingira ya Mikoko, kuwapatia Gari ya usafiri, kujenga mabanda ya wavuvi na vyoo vyake pamoja na ujenzi wa bara bara.

Alisema huduma hizo zitakwenda sambamba na wananchi hao kupatiwa Eka moja na nusu kwa ajili ya uanikaji wa dagaa, fedha taslim shilingi Milioni 11 zitakazohudumia bidhaa zao kuhamia eneo jipya pamoja na shilingi milionji 16 kwa ajili ya kuendeleza kamati hiyo.

Alieleza kwamba wakaazi wote wanaozunguuka mradi huo watakuwa na fursa ya kupatiwa huduma za Afya katika Kituo cha Afya cha Hoteli hiyo ambapo utaratibu utaandaliwa kwa mgonjwa atakayezidiwa maradhi kwa kupelekwa Hospitali ya Rufaa ya Mnazi Mmoja.

Akitoa nasaha zake mara baada ya zoezi hilo la utiaji saini makubaliano hayo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi aliwapongeza wananchi wa kiomba mvua kwa uamuzi wao huo na kuwataka waendelee kushirikiana na wawekezaji ili kusaidia kuimarisha uchumi wa taifa kupitia sekta ya uwekezaji.

Balozi Seif ambae pia ni Mbunge wa Jimbo la Kitope linalounda eneo hilo alisema Viongozi Wakuu wa Serikali wamekuwa wakisafiri nchi tofauti kujaribu kubembeleza wawekezaji wan chi hizo kuja kuwekeza miradi yao nchini ili kusaidia kunyanyua uchumi wa Taifa.

Hata hivyo Balozi Seif alionyesha masikitiko yake kutokana na kitendo cha kutiwa saini makubaliano hayo kuchelewa kwa karibu mwaka mzima kutokana na sababu za tatizo hilo kuingizwa siasa jambo ambalo linavuruga maendeleo ya jamii.

Mara nyingi nimekuwa nikialikwa kuzindua miradi ya wananchi katika Mkoa wa Kusini Unguja inayogharamiwa na wawekezaji. Hivyo ni vyema kwa wanakijiji cha Kiomba mvua na vijiji vyengine nchini wakaiga mfano huo wa wenzao wa Mkoa wa Kusini “. Alisema Balozi Seif.

Aliwaomba wananchi hao kuhakikisha kwamba yanapojitokeza matatizo baina yao na Taasisi au Makampuni yanayowekeza katika maeneo yao kwenda katika ngazi zinazohusika badala ya kukimbilia kupatuka kwenye vyombo vya Habari.

Mapema Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Unguja Meja Mstaafu Juma Kassim Tindwa alisema Taifa bado linaendelea kukabiliwa na tatizo la umaskini ambapo muhimili wa kusaidia mapato ya Nchi kwa sasa ni kukaribisha Makampuni na Taasisi katika sekta ya uwekezaji.

Kanal Mstaafu Tindwa alifahamisha kwamba Sekta ya uwekezaji hasa katika miradi ya Utalii Nchini hivi sasa imekuwa ikisaidia kwa kiwango kikubwa miraji ya Kiuchumi,kijamii kwa asilimia pana zaidi.

Mkuu huyo wa Mkoa wa Kaskazini Unguja aliiagiza Kamati ya Ulinzi na usalama ya Mkoa huo kuhakikisha kwamba inadhibiti na kuchukuwa hatua za kisheria kwa mtu au kikundi chochote kinachojaribu kuvuruga miradi ya uwekezaji na maendeleo ya wananchi katika Mkoa huo.

Mhe. Tindwa alikemea tabia ya baadhi ya watu walioamua kuiba tangi la kuhifadhia maji na baadhi ya milango kwenye soko lililojengwa na Hoteli ya Sea Cliff kwa ajili ya wananchi na wavuvi hao wa Kijji cha Kiomba Mvua.

Akitoa shukrani kwa niaba ya wananchi na wavuvi wenzake wa Kijiji cha Kiomba Mvua Katibu wa Kamati ya Bandari ya Kijiji hicho Bwana Mbwana Moh’d Ali Ameir alisema wananchi hao watakuwa tayari kushirikiana na uongozi wa mradi huo ili malengo yaliyokusudiwa yafikiwe.

Katibu Moh’d akiomba radhi kutokana na matokeo yaliyojitokeza kwenye mgogoro huo alisema moja kati ya jukumu walilokubali kulibeba wana kjijiji hao ni kuhakikisha suala la mazingira ya eneo hilo linalindwa na kuwa katika hali ya kuridhisha.

Mgogoro baina ya muwekezaji wa Hoteli ya Sea Cliff na wanakijiji wanaoizunguuka Hoteli hiyo ulikuwa ukivukuta katika suala la matumizi ya bandari, eneo la kuanikia madagaa pamoja na bara bara mambo ambayo muwekezaji huyo ameyakubali kuyatekeleza kwa mujibu wa makubaliano yaliyofikiwa.

Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
4/12/2014.

Hakuna maoni :

Chapisha Maoni