.

.

.

.

.

.

.

.
KARIBUNI TUHABARIKE, TUELIMISHANE, TUPEANE HABARI ZA KUKUFANYA UTABASAMU KIDOGO NA MATUKIO YALIYOFANYIWA UCHUNGUZI WA KINA TOKA KILA PEMBE CONTACTS: +255 787 377 722 Email: drweyunga@gmail.com PIA UNAWEZA KUNI FOLLOW KUPITIA INSTAGRAM YANGU @drweyunga | TANGAZA NASI ILI UWAFIKIE WATU WENGI ZAIDI.

Jumanne, 27 Januari 2015

DK. SHEIN ASEMA UTEKELEZAJI WA ILANI YA CCM UMEKUWA NA MAFANIKIO MAKUBWA

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema anafarijika kuona utekelezaji wa Ilani ya uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi katika kipindi cha miaka mine ya uongozi wa Serikali yake umekuwa wa mafanikio makubwa pamoja na kukabiliwa na changamoto kadhaa.

Amebainisha kuwa historia ya utekelezaji mzuri wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ambayo imezingatia malengo ya Mapinduzi ya mwaka 1964 umeendelea kuzidi kujenga imani ya wananchi kwa chama hicho.

Dk. Shein amesema hayo leo wakati akifungua Kongamano Maalum la Wana CCM wa Mikoa ya Pemba na Vijana Wasomi wa Taasisi za Elimu ya Juu ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Miaka 38 ya kuzaliwa Chama cha Mapinduzi liliofanyika ukumbi wa Skuli ya Sekondari ya Fidela Castro Pemba.

“Wananchi wana imani na CCM tangu wakati wa chama kimoja hadi sasa katika mfumo wa vyama vingi na ndio maana tumekuwa tukishinda katika chaguzi zote zilizopita hadi sasa” Dk. Shein alieleza.

Alifafanua kuwa hatua nzuri ya ukuaji wa uchumi wa Zanzibar kutoka asilimia 6.4 mwaka 2010 hadi asilimia 7.4 mwaka 2013 pamoja na ongezeko la makusanyo ya serikali kutoka shilingi bilioni 484 kwa miaka minne ya mwisho iliyoishia mwaka 2010 hadi shilingi bilioni 997 katika miaka minne ya Awamu ya Saba ni mafanikio ya kujivunia kwa wananchi wa Zanzibar.

“hatujafanya uganga bali ni hatua zetu makini katika kubana mianya, kuwahamasisha wafanyabiashara na walipa kodi wengine kulipa kodi zao pamoja na kuimarisha taasisi zetu za ukusanyaji wa mapato” Dk. Shein alisema.

Hata hivyo alifafanua kuwa hatua hiyo bado haijaiwezesha Zanzibar kutekeleza shughuli zake za maendeleo pasi na kupata misaada kutoka washirika wa maendeleo lakini alieleza kuwa jitahada zaidi zikiongezwa na ushirikiano zaidi ukiwepo miongoni mwa vyombo husika Zanzibar ina fursa ya kufanya vizuri zaidi.



Dk. Shein alizitaja baadhi ya changamoto ambazo Serikali yake ilipambana nazo katika miaka mine ya kutekeleza Ilani ya uchaguzi ya CCM kuwa ni pamoja na upya wa muundo wa serikali ambapo alitoa pongezi maalum kwa wasaidizi wake wakuu pamoja na mawaziri na wananchi kwa ushirikiano wao.

Alifafanua kuwa kufanya vizuri kwa Zanzibar kumechangiwa na hatua yake kupitisha sheria kwanza kabla ya kuunda Serikali ya Mapinduzi Zanzibar iliyo katika mfumo wa Umoja wa Kitaifa ambapo yeye amekuwa akitekeleza sheria hiyo katika uendeshaji wa serikali.

Aliongeza kuwa pamoja na kuwepo na changamoto za upungufu wa fedha lakini furaha yake ni kuona “watumishi wa serikali wanapata maslahi yao ikiwemo mishahara, viinua mgongo pamoja na pensheni zao kwa wakati” na kuwaahidi makubwa kadri hali itakaporuhusu.

Dk.Shein ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar, aliupongeza uongozi wa chama hicho Zanzibar kwa kuandaa kongamano hilo kwa kuwa lina umuhimu wa kipekee katika kujenga mustakala wa Zanzibar na pamoja na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa jumla.

“Kongamano hili lina umuhimu mkubwa kwa historia ya chama chetu, Mapinduzi yetu, Muungano wetu, Katiba iliyopendekezwa pamoja na mustakabala wa nchi yetu” aliwaeleza washirika wa Kongamano hilo.

Akitoa maelezo kuhusu Kongamano hilo, Katibu wa Idara ya Siasa na Uhusiano wa Kimataifa wa chama hicho Zanzibar, Masauni Yusuf Masauni, alieleza kuwa lengo la Kongamano hilo ni kutoa fursa kwa vijana kujifunza historia ya nchi, mafanikio ya serikali pamoja na suala la Katiba iliyopendekezwa..

Alifafanua kuwa kongamano hilo litakuwa na mada tatu ambazo ni historia ya Zanzibar na mchango wa ASP na TANU katika harakati za ukombozi wa Zanzibar na Muungano wa Zanzibar na Tanganyika. Mada nyingine ni Maudhui ya Katiba iliyopendekazwa na nyingine ni Mafanikio ya Utekelezaji wa Ilani ya CCM ya Uchaguzi wa 2010.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Vuai Ali vuai, akimkaribisha Dk. Shein kufungua kongamano hilo alisema kuwa kongamano hilo ni sehemu ya makakati wa chama hicho kuwaweka karibu vijana wa vyuo vya elimu ya juu ili kuwaandaa kushika nyadhifa mbali mbali za uongozi katika chama hicho.

Hakuna maoni :

Chapisha Maoni