


















Katika kusaidia uboreshwaji wa elimu ya Tanzania, Shirika la Kimataifa la ActionAid kwa kushirikiana na serikali ya Norway kupitia Wakala wa Maendeleo na Ushirikiano (NORAD) wamezindua mradi kuimarisha elimu kupitia vyanzo vya ndani vya mapato (Promoting Quality Education Through Progressive Domestic Resource Mobilization).
Akielezea kuhusu mradi huo, Makamu Mwenyekiti wa ActionAid nchini, Dkt. Azaveli Lwaitama alisema mradi huo unataraji kusaidia uboreshwa wa elimu nchini na zaidi maeneo ya vijijini sehemu ambapo zimekuwa zikionekana kuwa nyuma kielemu.
Alisema ili kupatikana kwa elimu bora kunahitajika uwekezaji wa kuboresha elimu kwa maeneo yote yanayohusika na elimu na inatakiwa kuanza na elimu ya shule ya msingi ili kuweza kumwandaa mwanafunzi kuanzia akiwa mdogo kwa kupata elimu bora inayokidhi viwango vya kimataifa.
“Elimu bora inataka kuwepo kwa uwekezaji kuanzia kwenye shule za msingi kwa kila jambo kama ni uniform, kalamu, uji, walimu kupatiwa stahiki zao na mengine yote yatimizwe,
“Ukitaka elimu bora lazima ujue inahitaji uwekezaji na mradi huu unataka kuongeza fursa kwa wanafunzi kwa kuanzia shule za msingi na zaidi tunaangalia vijijini,” alisema Dkt. Lwaitama.
Nae mgeni rasmi katika uzinduzi wa mradi huo, Balozi wa Norway nchini, Hanne-Marie Kaarstad alisema Norway na Tanzania wamekuwa wakishirikiana katika shughuli mbalimbali za maendeleo na ana furaha kuona mradi huo unafanyika kwa maendeleo ya baadae ya Tanzania.
Alisema Norway itaendelea kusaidia miradi mbalimbali ya elimu nchini katika kusaidia vijana kupata elimu kuanzia ngazi ya msingi hadi vyuo vya ufundi ili kuweza kuongeza wasomi ambao watasaidia ukuaji wa uchumi nchini.
“Nina furaha kuona mradi ambao utakuwa na mambo muhimu kwa ajili ya maendeleo ya sasa na baadae kwa Tanzania ninataraji kuona miradi inafanikiwa na ushirikiano wa Norway na Tanzania kwa miaka 50 sasa unazidi kuimarika na Tanzania inaushirikiano mzuri na Norway,” alisema Kaarstad.
Kwa upande wa Paul Mikongoti kutoka Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu alisema kupitia Katiba ya Tanzania ya mwaka 1977, ibara ya 11 (2) inaeleza kuwa kila Mtanzania anayo haki ya kujielimisha na kusoma ngazi zote za elimu hadi anapoamua kuacha kuendelea kusoma na hivyo mradi huo utasaidia watanzania kupata haki yao ya kikatiba.
Mradi huo unataraji kufanyika katika wilaya za Kilwa na Singida na utakuwa wa miaka mitatu ambao unataraji kuzifikia shule 60, 30 kwa kila wilaya.
Aidha unataraji kuwafikia wanafunzi wa kiume 7,758 na wakike 8,474 kwa wilaya ya Singida na Kilwa kuwafikia wanafunzi wa kiume 6,607 na wakike 6,546 lakini pia walimu 287 kwa Singida na 290 kwa Kilwa.
Hakuna maoni :
Chapisha Maoni