WANAWAKE kupitia Mfuko wa Wanawake Tanzania wamekutaka katika mkutano na kutoa tathimini ya mwaka mmoja wa Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais Dk. John Pombe Magufuli. Mkutano huo ulioshirikisha wanawake kutoka mikoa mbalimbali umefanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Mtandao wa Jinsia Tanzania, TGNP Mabibo jijini Dar es Salaam.
Akizungumza katika mkutano huo, Mwenyekiti wa mfuko huo, Profesa Ruth Meena aliipongeza Serikali ya Dk. Magufuli kwa mafanikio ilioanza kuonesha katika ukusanyaji na usimamizi wa mapato pamoja na mapambano dhidi ya vitendo vya rushwa huku akiiomba Serikali kutambua pia kwa vitendo mchango wa wanawake katika ujenzi na maendeleo ya nchini.
Alisema wanawake nchini watafurahia kuona Serikali ya Rais Magufuli inakisikia kilio cha wanawake juu ya vitendo vya udhalilishwaji katika mitandao ya kijamii, ikiwemo kuonesha uwajibikaji katika kushughulikia sheria kandamizi ambazo bado zinaibana jamii hiyo.
"...Tunaiomba Serikali ikemee suala la udhalilishaji wa wanawake katika mitandao ya kijamii, Sheria ziwekwe kuwalinda wanawake. Imefanya vyema kupiga marufuku nyimbo mbili na ngoma zinazikwenda kinyume na maadili yetu hivyo ikemee pia pale wanawake wanapodhalilishwa," alisema Profesa Meena.
Aidha mkutano huo ulipongeza mfumo wa elimu bure unaotolewa sasa na Serikali kwa kuwa unatoa fursa kwa familia maskini hasa za wanawake wajane kupata elimu jambo ambalo awali lilikuwa changamoto kwa jamii hiyo. Walipongeza pia uwajibikaji unaoendelea kusimamiwa na Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais Magufuli umeongeza nidhamu kazini pamoja na kuwajibika katika utoaji huduma.
Mkutano huo ulishirikisha wanawake wanaharakati ngazi za jamii kutoka mikoa mbalimbali ya Tanzania Bara na Visiwani ambapo walijadili masuala mbalimbali ikiwemo kushirikishana changamoto kutoka maeneo yalikotoka wajumbe wa mkutano na kuangalia mbalengo ya baadae.
Hakuna maoni :
Chapisha Maoni